Mbinu Nne za Kukuza Ubunifu wa Mtoto

Ubunifu ni uwezo wa kufikiri, kutafuta majibu au kutatua changamoto kwa namna isiyotarajiwa. Mtu mbunifu hufanya mambo kwa namna isiyo ya kawaida. Hafanyi vitu fulani kwa sababu ameona watu wakifanya. Hafuati mazoea wala uzoefu. Huwa tayari kufanya mambo mapya.

Ingawa kuna uhusiano mdogo kati ya ubunifu na uwezo wa jumla wa akili, kwa kawaida, mtu mwenye akili si lazima awe mbunifu. Unaweza kuwa na akili ya kuchambua, kuelewa, kukumbuka na kueleza mambo unayojifunza lakini usiweze kufanya mambo kinyume na mazoea.

Ubunifu unaonekana kwa namna mtu anavyoweza kufikiri na kupendekeza njia mbalimbali za kutatua tatizo. Kwa mfano, mtu mbunifu anapokutana na changamoto ya kukosa chakula, anaweza kufikiri mbinu mbalimbali za kumsaidia kupata chakula anachokihitaji. Mwenzake asiye mbunifu, huwa na mbinu moja na ikishindikana hana namna ya kujinasua.

Elimu rasmi inayopatikana darasani, kwa kawaida, haikusudiwi kumjengea mwanafunzi uwezo wa kubuni mambo mapya. Mitaala yetu inafundisha kufikiri kwa namna inayofanana, kutoa majibu yale yale na wakati mwingine kufumbua matatizo yanayoyofahamika tayari.

Mitihani inayopima uelewa wa mwanafunzi, kwa mfano, inatafuta majibu yanayotarajiwa. Kwamba mwanafunzi hatarajiwi kufikiri kinyume na matarajio ya mwalimu wake maana yake ni vigumu kwa uwezo wa kubuni kukuzwa kupitia mitaala rasmi.

Hata hivyo, ubunifu ni muhimu katika maeneo karibu yote ya kimaisha. Taaluma. Uhusiano. Kazi. Uongozi. Maeneo karibu yote yanahitaji majibu mapya yasiyotegemea uzoefu.

Ubunifu unamsaidia mtu kupambana na changamoto zake kwa namna nyepesi. Ubunifu si tu ni muhimu kwenye sanaa, lakini pia unayo nafasi yake katika kila nyanja ya maisha yetu ya kila siku. Bila ubunifu ni vigumu kwa mtu kuendana na mabadiliko tunayokabiliana nayo kila siku yanayohitaji majibu mapya.

Tafiti zinaonyesha kuwa ubunifu ni uwezo unaotegemea mazingira ya kimakuzi anayokutana nayo mtoto. Wazazi, kwa sababu hiyo, wanahitaji kujifunza namna ya kujenga uwezo huu. Vile watoto wanavyoelelewa, inaweza kudumaza uwezo wao kiubunifu au kuukuza. Makala haya yanapendekeza mbinu nne kubwa unazoweza kuzitumia kukuza ubunifu wa mwanao.
 
PICHA: pinterest.com

Mruhusu mtoto akutane na changamoto

Kwa kawaida, binadamu hatupendi changamoto. Tunazikwepa. Tunapopata mafanikio, hatutamani tukabiliane na changamoto. Tunayachukulia mafanikio kama hatua ya juu inayotunusuru na changamoto. Kwa hivyo, tunajitahidi sana kuwanusuru wanetu wasikutane na changamoto. Tunafikiri changamoto hazipaswi kuwa sehemu ya maisha ya mtu aliyefanikiwa.

Hata hivyo, kisaikolojia, changamoto zinahitajika. Changamoto zinajenga hamasa ya kufanya kitu. Changamoto zinaongeza uwezo wa kufikiri. Akili ya mtu mwenye uhitaji unafanya kazi kwa kasi na ufanisi kutafuta majibu. Mtu asiye na uhitaji hahitaji kutumia akili nyingi kutafuta majibu asiyoyahitaji.

Ni kwa sababu hiyo, mzazi unahitaji kuweka mazingira yanayomhamasisha mtoto kufikiri. Mfano, badala ya kumpatia kila anachokihitaji, mnyime baadhi ya vitu anavyofikiri ni vya muhimu kwake. Mpe fedha zisizomtosha. Punguza kumfanya ajione anaweza kupata chochote anachokihitaji.

Unapofanya hivyo, unamjengea kiu ya kutafuta mbinu za kutumia kisichomtosha. Changamoto, kwa maana hiyo, zinamfanya atafute majibu yasiyotarajiwa. Huo ndio ubunifu.

Mpe uhuru, punguza ukosoaji

Ni kawaida kwa wazazi kujaribu kuwadhibiti watoto. Kuna namna fulani ya hofu kuwa unapompa mtoto uhuru basi anaweza kuutumia vibaya au kupata matatizo. Kwa sababu hiyo, tunapenda kuwalinda watoto kupita kiasi.

Tafiti, kwa upande mwingine, zinaonesha kuwa watoto wanaobanwa sana hawawezi kufikiri vizuri ukilinganisha na watoto wanaokua bila kudhibitiwa. Kubanwa kuna maana ya kuongozwa kupindukia katika maeneo mengi ya kimaisha.

Mruhusu mtoto  kuwa huru. Mpe nafasi ya kuchagua kufanya mambo mapya. Sambamba na uhuru, unashauriwa kupunguza ukosoaji. Usiwe mwepesi wa kuhukumu na kurekebisha mawazo yake isipokuwa anapofanya makosa ya wazi. Mwache akosee.

Wakati mwingine, makosa yanaweza kuwa kichocheo kikubwa cha kujifunza kwa urahisi. Mtu asiyeamini anaweza kukosea, huogopa kujaribu mambo mapya. Huna sababu ya kumnyima mtoto fursa ya kujifunza kwa vitendo.


Mpe vifaa changamshi

Mtoto anahitaji vifaa kujifunza ubunifu. Hata hivyo, wazazi wengi huwanunulia watoto vifaa ambavyo tayari vimeshatengenezwa. Kazi ya mtoto inabaki kuwa kuvitumia vivyo hivyo vilivyo, bila kuvifanyia mabadiliko yoyote. Mfano, mtoto ananuliwa ‘gari’ ambalo tayari lina matairi na kila kitu. Kumpa mtoto vifaa hivi vilivyotengenezwa tayari ni kuviza ubunifu.

Aidha, wazazi wengine huwapatia watoto vifaa vya kiteknolojia vinavyojenga utegemezi usio wa lazima. Michezo hii, mbali na kujenga tabia zisizofaa kwa mtoto, inatekeleza muda.

Katika kukuza ubunifu wa mtoto, inashauriwa kumpatia mtoto malighafi atakazozitumia kutengeneza vifaa vinavyokidhi mahitaji yake. Badala ya kumnunulia gari lililotengenezwa tayari, mtafutie vipande vya maboksi, gundi, nyaya, kamba, vizibo vya chupa, misumari, mbao na vifaa vingine vimsaidie kuunda kitu kinachokuza uwezo wake wa kufikiri.

Mruhusu kufikiri tofauti na wewe

Wazazi tunapenda watoto wafikiri kama sisi. Hatupendi wafikiri kinyume na sisi hata kama kufanya hivyo hakuleti madhara yoyote. Wakati mwingine tunawaadhibu watoto kwa kosa la kutofautiana misimamo na sisi kwa mambo ya kawaida. Kwa kufanya hivi, tumewakuza watoto kuogopa kufikiri kwa uhuru. Tumeua ubunifu.

Unashauriwa kuwapa watoto fursa ya kufikiri tofauti. Inapobidi waruhusu kupingana na wewe. Kwa mfano, hata kama ungetamani mwanao avae nguo fulani uipendayo, huna sababu ya kumlazimisha kufanya hivyo. Mpe nafasi ya kuchagua akipendacho almuradi hakiathiri mamlaka yako kama mzazi. Unapofanya hivyo, unamjenga kuwa mtu mbunifu asiyetegemea uzoefu kufanya mambo yake.


Kadhalika, mpe mtoto nafasi ya kuyatazama mambo kwa sura tofauti. Kutafuta majibu tofauti kwa matatizo anayokabiliana nayo. Anapofikiri amepata majibu, mpe nafasi ya kufikiri majibu mengine kwa tatizo alilonalo. Anapopata majibu yasiyotarajiwa, tambua bila kumpa motisha. Ubunifu haupaswi kutegemea motisha kutoka nje. Ubunifu unaanza ndani ya mtoto mwenyewe.

Fuatilia Jarida la Maarifa ndani ya gazeti la Mwananchi kila Jumanne kwa Makala kama hizi.

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Uislamu ulianza lini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia