Faida, Hasara za Vituo vya Kulea Watoto

TUMEKUWA tukijadili changamoto zinazowakabili wazazi wanaofanya kazi mbali na nyumbani. Njia kadhaa zinatumika kukabiliana na changamoto hizi. Moja wapo, ni kuwaajiri wasichana wa kazi kwa lengo la kusaidia kuwalea watoto.
Tulipendekeza kuwa msingi mkuu wa kupunguza changamoto za huduma hizi zinazotolewa na wasichana wa kazi ni kujenga nao mahusiano mazuri ya kifamilia na kikazi. Mahusiano haya yanawajengea motisha ya kufanya kazi kwa uadilifu na moyo wa kujituma.

Hata hivyo, pamoja na jitihada hizo za kujenga uhusiano wa kifamilia, bado ni vigumu kujihakikishia huduma bora kwa kuwa mara nyingi huduma hizi zinatolewa katika mazingira yasiyo rasmi.
Kwa mfano yamekuwepo matukio ya wasichana hawa kuwatendea watoto vitendo visivyokubalika vinavyoathiri tabia na uelewa wa watoto. Matukio haya yanafanyika katika mazingira ambayo wazazi wamejitahidi kufanya wajibu wao kuhakikisha kuwa msichana anafanya kazi katika mazingira rafiki.
Kufuatia changamoto hizi, zipo familia zenye uwezo zinazoamua kutumia malezi rasmi ya watoto kupitia vituo maalumu vya kulelea watoto, day care. Vituo hivi hupokea watoto wa majuma kadhaa hadi wa umri wa kuanza shule kwa lengo la kuwalea kwa muda ambao mama anakuwa kazini.


Aina za vituo vya malezi
Mara nyingi, katika vituo hivi watoto wa umri unaokaribiana kati ya umri wa majuma kadhaa hadi miaka sita hulelewa kwa pamoja. Tofauti na kuwatumia akina dada wa kazi, huduma hii hutumia watu wenye ujuzi wa malezi ya watoto, waliofunzwa namna ya kumhudumia mtoto kulingana na umri wake.

Huduma za malezi kituoni zinatofautiana kulingana na umri wa mtoto. Katika umri wa kuanzia mtoto kuzaliwa mpaka miaka miwili, huduma kuu huwa ni sawa na ile inayotolewa na mama au msichana wa kazi. Mkazo ni kumpa mtoto chakula bora, kumtunza mtoto kimwili, kwa maana ya kuhakikisha anakuwa safi na salama. Hakuna mkazo katika mtaala wa elimu.
Kuanzia miaka miwili au mitatu, walezi wa vituo hivi huanza kudokeza kidogo mambo ya elimu kumkuza mtoto kiufahamu. Kwa baadhi ya vituo, mtoto huanza kufundishwa kuhesabu, kuandika na kusoma.

Katika umri wa miaka minne hadi sita, vituo hivi huanza kufahamika kama shule ya awali, kwa kwa kuwa pamoja na kukutana na mahitaji ya msingi ya mtoto, lengo kuu linakuwa kumpatia mtoto elimu. Katika hatua hii, walezi hufanya majukumu ya walimu.

Aidha, baada ya mtoto kutimiza miaka sita na kuanza shule, mfumo wa malezi huweza kufanyika kwa mtindo wa aina mbili; kuhudhuria masomo kwa mtindo wa kurudi nyumbani jioni; au kuondoka nyumbani kwa miezi kadhaa kwenda shuleni, mbali na nyumbani, akilelewa na kufundishwa na walimu kwa ushirikiano na walezi wasio walimu.

Huduma hizi hazikuwa maarufu sana siku za nyuma, lakini kwa sasa uhitaji wake umeanza kuwa mkubwa. Jijini Dar es Salaam, kwa mfano, vituo hivi vya aina zote hizo tulizozitaja vipo katika maeneo mengi. Miji mingine kama Arusha, Mwanza na Moshi, huduma hizi zina umaarufu mkubwa.

Sambamba na vituo hivi, shule za msingi za kulala zimekuwa maarufu. Pamoja na lengo la kumpatia mtoto elimu bora, shule hizi humpa mzazi nafasi ya kujikita na kazi nyinginezo bila wasiwasi wa namna watoto watakavyolelewa.

Faida za malezi ya vituoni

Malezi ya watoto katika vituo maalum hufanyika katika mfumo wenye namna fulani ya urasmi kuliko nyumbani. Ushindani huwalazimisha wafanyabiashara wanaoanzisha vituo hivi kuweka mazingira bora yanayowavutia wazazi na watoa huduma. Mazingira hayo ya kimalezi yanapoboreshwa humnufaisha mtoto kwa namna kadhaa.
PICHA: childminder.ng

Kwanza, yanamsaidia mtoto kuchangamka kiakili ukilinganisha na watoto wanaolelewa nyumbani. Tafiti zilizofanywa katika nchi zilizoendelea zinathibitisha kuwa watoto waliopelekwa kwenye vituo vya malezi mapema wanakuwa wachangamfu kiakili kuliko wenzao wanaolelewa nyumbani.

Sababu kubwa ni kuwa katika kituo mtoto anakuwa na fursa ya kuchangamana na wenzake wanaotoka kwenye familia nyingine. Kucheza, kuzungumza, kuwasiliana na wenzake humfanya ajifunze mambo mapya kwa wepesi kuliko kama angekuwa mwenyewe nyumbani.

Lakini pia, malezi haya hufanyika kwa mfumo wa shule zisizo rasmi. Mtoto hupatiwa vifaa vya kujifunzia na kucheza vinavyolingana na mahitaji yake. Shughuli zake hufanyika kwa kufuata mtiririko maalum tangu anapowasili mpaka anapoondoka. Wakati mwingine mtoto hulazimika kuvaa sare za shule na hivyo kujisikia yuko shuleni.

Kwa sababu hiyo, vituo hivi hujenga daraja muhimu kati ya maisha ya nyumbani na shule. Mtoto huwa katika mazingira ya kishule shule ambayo hata hivyo hayamshinikizi kujifunza kusoma, kuandika na kuhesabu. Hali hii humfanya mtoto azoee mazingira ya shule mapema kuliko anapopelekwa shuleni akitokea nyumbani moja kwa moja.

Vile vile kutokana na ukweli kuwa malezi haya hufanywa kibiashara (wakati mwingine) na watu wenye uelewa wa makuzi ya watoto, mzazi anakuwa na uhakika na huduma anazopatiwa mwanae. Kwamba mwanae yuko kwenye mikono salama humfanya mzazi aendelee na kazi zake kwa utulivu kuliko anapomkabidhi msichana wa kazi.

Changamoto za malezi ya vituoni

Hata hivyo, penye faida hapakosekani changamoto. Manufaa ya huduma hizi mara nyingi yanategemea zaidi ubora wa huduma zinazotolewa. Vinginevyo, changamoto kadhaa zinaweza kujitokeza.

Mosi, tafiti zilizofanyika katika nchi  zilizoendelea zimebaini uwezekano wa kuzorota kwa uhusiano kati ya mzazi na mtoto anayehudhuria vituo hivi tangu akiwa mtoto. Kwa mujibu wa tafiti hizi, mtoto anayeanza kuhudhuria malezi ya vituo katika umri mdogo anakuwa kwenye hatari ya kuwa na uhusiano hafifu na wazazi wake.

Pia, katika vituo hivi mara nyingi walezi huwaangalia watoto wengi kwa wakati mmoja. Malezi haya ya kimakundi humfanya mtoto mmoja moja kukosa mtu wa kushughulika na mahitaji yake binafsi.

Kwa mfano, mtoto wa umri wa mwaka mmoja kwa kawaida ana madai mengi. Anapohitaji kitu, anahitaji awepo mtuanayeweza kumsikiliza kwa wakati. Wingi wa watoto usioendana na idadi ya kutosha ya walezi huweza kufanya hili lisiwezekane.

Katika mazingira ambayo mtoto hapati usikivu wa mlezi, anakuwa kwenye hatari ya kutafuta mbadala kwa lengo la kupata usikivu huo kama vile kulia bila sababu, ubinafsi na ugomvi.

Mbali na hayao, upo uwezekano wa mtoto kuanza kujifunza tabia zisizotarajiwa. Kukaa muda mrefu na watu wengine mbali na familia yake katika umri ambao bado hajajifunza lolote kutoka kwenye familia yake, hukaribisha uwezekano wa kujifunza tabia ngeni zinazoweza kumstua mzazi.

Vile vile, zipo tafiti zinazohusianisha huduma hizi na matatizo ya afya kwa watoto. Kwamba wanapolelewa katika mazingira ya pamoja bila uangalizi makini, watoto huwa kwenye hatari ya kuambukizana magonjwa.


Inaendelea

Fuatilia Safu ya Uwanja wa Wazazi kwenye gazeti la Mtanzania kila Alhamisi kwa makala kama hizi.

Maoni

  1. Asante sana kwa kutupa tafiti nzuri kuhusu watoto na makuzi yao.
    Taiga ili liendelee lazima Lowe na misingi mizuri tokea makuzi awali ya mtoto kwenye familia.

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia

Uislamu ulianza lini?

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)