Maneno ya kuepa unapozungumza

Unaweza kuwa unaamini huna dharau. Lakini watu ndivyo wanavyokuona. Yaani vile ujichukuliavyo, sivyo wanavyokuchukulia wenzio.

Hali hii inaweza kuchangiwa kwa kiasi kikubwa na maneno unayotumia katika kuwasiliana na watu.

Maneno, hata yale madogo madogo, yana nguvu kuliko tunavyoweza kufikiri.

Hebu tuangalie mifano michache kuonyesha athari za maneno mawili, 'najua' na 'lakini'.

1. Najua:

Unapomjibu mtu anayekuambia jambo kwa neno 'najua', unatoa picha kwamba wewe ni 'machinoo'.
Hata kama ulishakijua kinachosemwa, si uungwana kusema '...hiyo nlishajua mbona...?' au '...ah, nshafikiri kabla...'.
Sema '...nafurahi kusikia hivyo..'
'Najua' inaleta picha kwamba unajidai kuwa na taarifa nyingi, mjuaji, usiyekubali kujifunza kwa wenzako, unawadharau wenzako na sifa nyingine mbaya mbaya.

2. Lakini:

Inakuwa pale unapoanza na kila namna ya sifa nzuri, halafu unaishia na 'lakini' kuonyesha upungufu uliouona katika hali husika. Mawazoni mwako unadhani zile sifa ulizoanza nazo zitamsaidia msikilizaji kukosolewa bila maumivu. Ukweli hii haileti picha nzuri. Neno lakini ni sawa na kusema '...yale yote ya mwanzo nimefuta, ukweli ni kwamba...' au '...zile sifa za mwanzo zilikuwa geresha, saizi yako ni...'

Maneno mengine kama 'hata hivyo', 'pamoja na hayo', 'ingawa', 'hata kama' yanasifa ile ile ya kuonyesha kwamba wewe ni mkosoaji, hukuwa na nia ya kushauri kama unavyotaka iaminike.

Ikiwa hutopenda watu wakuelewe usivyo, tumia maneno kwa tahadhari kubwa. Leo tumeanza na hayo mawili.

Maoni

  1. Bwaya, nadhani maneno uliyoyataja hapo yanaweza kuwa na maana nzuri ama mbaya kulingana na matumizi yake katika mtiririko wa maelezo anayoyatoa mtumiaji wa maneno yenyewe. Kwa mfano nikisema, '...hatimaye Sungura aliendelea kuzungukazunguka shambani kwa imani kuwa atapata majani siku hiyo ingawa alikuwa amevunjika mguu', au '...wazee walishindwa kuipata haki yao katika baraza ya Kijini, hata hivyo, waliazimu kufunga safari kufikisha madai yako katika ofisi ya Katibu Tarafa' ama, '...sitachoka kutafuta hata kama wataninenea mabaya' nk nk.
    Kwa hivi, maneno na kauli mara nyingi nadhani huendana na hali halisi ya wakati huo.

    JibuFuta
  2. Najua wajua lakini nahakikisha kuwa wajua ninachodhania wajua:)

    ...Lakini tena sina uhakika kuwa wajua ninachodhania wajua.

    Wiki njema:D

    JibuFuta
  3. Subi,
    Pengine ni kwa sababu ya jitihada za kuandika kwa ufupi.

    Nakubaliana na maoni yako.

    Maneno hayo, hayaleti picha mbaya ikiwa yatafuatiwa na maneno yasiyokinyume na pia yakiwa yanazungumzia nafsi ya mzungumzaji mwenyewe na si anayesikiliza.

    Serina, nakubaliana na wewe. Kumbe maneno hayo hayo yanategemea mukhtadha. Muhimu ni matumizi ya makini kwa maneno hayo katika mazungumzo. Ni sehemu muhimu ya kujielewa.

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Pay $900? I quit blogging