Kuyamudu Mafanikio Yako...


Fikiria umehitimu masomo kwenye chuo maarufu; umepata alama nyingi kwenye mtihani mgumu; umepata kazi yenye heshima; umejenga nyumba nzuri; umenunua gari la ndoto zako; umesafiri kwenda mahali wanakotamani kwenda watu na hawawezi au basi tu umekutana na mtu fulani maarufu.

Unajisikiaje kama watu hawatafahamu? Kwa nini watu wakifahamu unajisikia vizuri zaidi?

Kwa wengine wetu, mafanikio yetu yasipofahamika kwa wengine haturidhiki. Tunapima thamani ya tulichonacho kwa kuangalia wengine wanavyokikubali. Ndani yetu unakuwepo msukumo wa kutamani wengine waone mema yanayotutokea. Furaha ya binadamu ni kufanikiwa. Hakuna asiyependa kufanikiwa na ni vigumu kuficha mafanikio. Ukifanikiwa watu wataona na wataambiana.

Hata hivyo, hali hii ya kupenda mafanikio, inaweza kuchukua sura ya mashindano. Mtu anaweza kushindwa kuvumilia mafanikio yajitangaze yenyewe. Anaweza kujikuta akitumia nguvu nyingi kutangaza. Anatamani kila anayekutana naye asikie. Bahati mbaya kufanya hivyo huleta matokeo hasi kama nitakavyofafanua.

Binadamu (kwa asili yake) ni mtu wa mashindano. Kimya kimya, tunashindana sisi kwa sisi. Nani ana nini na mimi nina nini. Tunajilinganisha. Ukiwa na kizuri wasichonacho, unajihesabu umefanikiwa. Ukikosa kizuri walichonacho wengine, unanyong'onyea. Sehemu kubwa ya maisha yetu ni KUJILINGANISHA. Hulka hiyo ya kushindana hutufanya tuwaonee wivu (na hata ikibidi kuwachukia) wale wanaoonekana kutuzidi.

Unapotangaza mafanikio yako zingatia hilo. Asiye na hicho ulichonacho, hatakuwa mwepesi kukupa heshima unayoitarajia. Sababu? Anatafsiri heshima yako kama udhaifu kwake. Hatakubali ajione dhaifu kirahisi. Ndio maana atakusema, atakupinga na ikibidi kukudhalilisha. Kwa nini? Mashindano.

Ni vizuri kabla hujawaambia watu mafanikio yako jiulize, 'Hivi ni lazima wajue? Wakijua watanufaika? Kama ni muhimu wajue, je siwezi kuwaacha wakajua wenyewe? Hadhi yangu inategemea namna watu wanavyoniona?'

Pengine tunahitaji kujifunza kumudu mafanikio. Kama si lazima, usiwaumize watu kwa kuwaonesha kile unachojua hawana. Waache waone wenyewe na ikibidi waambiane wenyewe. Unapotumia mikakati kuwajulisha, inakuwa kama mtu anayekwenda kula keki katikati ya watu wenye njaa. Hawataelewa mantiki yake, hata kama wanaweza kutoa pongezi kwa maumivu. Uzuri ni kwamba anayejitambua, hawaumizi wengine kihisia.

Maoni

  1. Ni kweli kabisa hiyo ndio tabia yetu binadamu na kutokana na hii tabia ya kutaka kujionyesha tumempa Markzagart faida ya kuuunda facebook ambapo humo kazi yetu n kuonyesha mafanikio,
    kwa nn tusiache watu wayaone wenyewe live mpaka tu post mitandaoni...
    tubadilike jamani

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia