Tunavyoweza Kuacha Tabia ya Kuhukumu Wengine

Majuzi nikiwa kwenye mgahawa mmoja mjini, waliingia watu wawili wanaume waliokuwa wamevalia mavazi yanayoashiria imani yao ya kidini. Wote wawili walipamba vichwa vyao kwa vilemba nadhifu, mmoja wao akibeba mfuko mdogo mweusi. Nyuso zao, kwa hakika zilipambwa na tabasamu pana la kirafiki lililofanya ndevu zao ndefu ziwe na mwonekano wa kupendeza. Miguu yao ilivaa viatu vya wazi na juu yake zilining’inia suruali fupi mithili ya kaptula ndefu zilizojitokeza ndani ya kanzu fupi nadhifu.


Walipokuwa wakijongea kukaa kwenye meza mojawapo, kila mmoja aligeuka kuwatazama kwa wasiwasi. Mkahawa ulijawa hali ya tahayaruki fulani isiyotarajiwa. Macho yote yaliwaelekea vijana wale wawili. Ndani ya muda mfupi, wageni wasio wa-Tanzania, ambao ndio waliokuwa wengi kwenye mgahawa huo, walianza kuondoka mmoja baada ya mwingine. Ingawa nilikuwa mmoja wapo wa waliobaki, nami kama wengine nilikuwa na wasiwasi ya nini hasa kingeweza kutokea.

Tunahukumu kwa haraka

Wasiwasi wa sote tuliokuwa kwenye mgawaha ule ulinifanya nijiulize masuala mengi. Kwamba pamoja na kwamba hatukuwajua hata kidogo watu wale wawili, akili zetu zilituaminisha kuwa tunawajua vilivyo. Kila aliyeondoka kwa wasiwasi, huenda aliwahusisha watu wale na taswira fulani aliyokuwa nayo kabla ya kuwaona. Kwamba huenda watu wale walishabihiana na watu waliowahi kuhusishwa na matukio fulani yasiyo ya kawaida.

Hivi ndivyo tunavyofanya katika maisha yetu ya kila siku. Kila tunayekutana naye tunamweka katika kundi fulani tulilonalo tayari kichwani. Tunapokutana na mtu kutoka mkoa wa Mara, kwa mfano, tunamlinganisha na watu wa Mara tuliowahi kukutana nao kabla. Tunatumia kundi tunalolifahamu kumwelewa mtu huyo ambaye ndiye kwanza kumekutana naye.

Akili zetu zinaona chochote

Ukitazama picha hii hapa chini, unaweza kuona sura mbili. Waweza kumwona ajuza wa umri mkubwa aliyejifunika na blanketi zito shingoni na kuzizungushia ushungi kichwani. Lakini pia waweza kumwona binti mdogo akiangalia upande akiwa kajizungushia ushungi upande mmoja wa kichwa. Unachokiona kwenye picha hii kinategemea ama matarajio yako au vile akili yako inavyotafsiri kila kilichochorwa kwenye mchoro huu.

Unamwona bibi au binti? Picha: huria mtandaoni

Kwa mfano, pua ya ajuza yaweza kuwa mwonekano wa upande wa uso wa msichana anayetazama upande wa pili. Jicho la ajuza laweza kuwa sikio binti. Mdomo na kidevu cha ajuza vyaweza kuwa shingo ya msichana wakati mdomo wa ajuza ni mkufu wa binti. Hiyo ni mifano namna akili zetu zinavyoweza kuchakata taarifa ili kupata taswira inayoeleweka.

Katika kujaribu kuelewa kile tunachokitazama, mara nyingi akili zetu hazipendi kujitesa. Akili zetu hazitaki kujichosha kufanya kazi ya kufahamu kitu kimoja moja kwa kukichambua chenyewe bila kukihusisha na ama tunavyojijua tayari ama mazingira yake. Ni kama vile akili hutafuta njia rahisi ya kupunguza kazi ya kuwaelewa wale wanaotuzunguka.

Tunajikuta tunachanganyikiwa

Matokeo ya hulka hii ya kujaribu kuelewa kile tusichokifahamu wakati mwingine ni kutokuelewa kile tunachotaka kukifahamu. Kwa mfano, watu wale wawili walioingia kwenye mkahawa ule wanaweza kuwa watu wema, wacha Mungu, waliofika pale kufanya kikao cha kujadili mambo yao mema. Tuliokuwepo pale, tulitumia taswira tulizo nazo vichwani mwetu kuwaelewa. Ndio sababu wengine wetu waliondoka.

Katika maisha ya kawaida, kutumia uzoefu tulionao katika kuwaelewa watu na matukio tunayokutana nayo, hutufanya tuwe watu wa kuhukumu. Tunaamini, kwa mfano, watu wa makabila fulani, dini fulani, taifa fulani, kuwa wanayo tabia inayofanana. Matokeo yake ni kwamba tunawaonea watu wengi kwa kuwaweka katika mafungu ambayo wakati mwingine hayawastahili. Kwa mazoea haya, tumewahukumu wengi isivyostahili na wakati mwingine hata wanapofanya kinyume kabisa na matarajio yetu, bado tunashikilia sifa tuliyowapachika kabla hatujafahamu.

Tunaweza kubadilika

Tubadili fikra zetu kwa kuachana na mazoea ya kufikia mahitimisho haraka bila kuwa na taarifa za kutosha. Ni makosa, kwa mfano, kulielewa jambo kwa sababu tu tunaamini tumewahi kukutana nalo siku za nyuma. Tunahitaji kuyaona mambo katika upekee wake.

Kila mtu katika kabila, dini na hata familia anaweza kuwa na tabia zozote zisizo na uhusiano wowote na watu wengine wa kundi tulilomweka. Ubaya wa mtu leo, waweza kufuatwa na uzuri wake kesho. Uzuri wa leo, waweza kufuatwa na ubaya wa kesho. Tusihukumu mapema.


Mwandishi ni Mhadhiri wa Saikolojia, Chuo Kikuu cha Kikatoliki Mwenge (MWECAU). Anapatikana kwa bwaya@mwecau.ac.tz na 0754 870 815

Maoni

  1. Mwanafunzi wa wanafunzi wako, nakushukuru kwa kipande hiki elimishi.

    Ni kweli, mara nyingi tumekuwa wepesi kutoa hukumu kwa mambo tusioyajua kwa undani wake. Tumeshindwa kutoa faida ya mashaka kwa tusiowajua/tusioyajua matokeo yake tunapopata fursa ya kufahamu ukweli (baada ya hukumu) tunajikuta katika maisha ya kukuta.

    Ingawa katika mazingira hatarishi ni vema kuchukua tahadhari kwa kuhukumu hivyo ili mradi hukumu yako haina madhara kwa mhukumiwa. Falsafa ya askari ni kuwa tuhumu kila mmoja na usiamini hata mmoja (suspect everyone, trust no one), kwa kiasi fulani naweza kukubaliana na falsafa hii hasa katika mazingira hatarishi - mazingira ambayo usipochukua tahadhari kwa kuhukumu hivyo madhara yake ni makubwa kuliko madhara yatokanayo na hukumu yako.

    Aidha, wakati flani mkuu wangu wa kazi aliniambia. Unaposhughulikia masuala ya fedha ni bora kuwa na falsafa ya kuwa kila mmoja katika kampuni/shirika ni "mwizi" na kwamba wakati wowote mtu anapoleta madai yake mezani unapaswa kuangalia madai yale kwa jicho la shauku ya kumkamata mwizi - kuwa yeyote anaweza kuwa mwizi (everyone is potentially a thief).

    Sasa nikiangalia falsafa hizo mbili, nashawishika kuamini kuwa sio mara zote hukumu zetu huwa ni mbaya bali hutumika kama kinga (defence mechanism) na kama hukumu hiyo haina madhara kwa mhukumiwa ukilinganisha na madhara yanayoweza kujitokeza kwa kutojali viashiria vilivyoonekana, basi ni bora kuweka hukumu na kuchukua hadhari kuliko kuiishi hatari kwa hofu ya kutoa hukumu.

    Mpaka wakati mwingine.

    Maranya O'Mayengo

    JibuFuta
  2. Ubarikiwe....tuna kasumba ya kuwaweka watu katika mkundi ambayo tayali tunaya kichwani...kuna wakati pia makundi yetu yana toa majibu sahihi ama tofaut lakini tunakataa kukubali ukweli..nini tufanye kupokea mabadiliko tunapoona utofaut na matarajio yetu???

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Pay $900? I quit blogging