Mbinu za Kutafuta Ajira Mtandaoni

Changamoto kubwa inayoweza kukukabili unapotafuta kazi, ni taarifa zitakazokusaidia kujua uelekeze wapi maombi ya kazi. Zamani, ili kupata taarifa za kazi, watu walitegemea radio, magazeti, televisheni na taarifa za marafiki wanaofahamiana nao. Mambo yanazidi kubadilika kwa kasi. Sasa hivi, kwa mfano, matumizi ya mtandao yamerahisisha namna tunavyoweza kupata taarifa hizi.

Hata hivyo, pamoja na uwepo wa mtandao, bado kuna changamoto ya wapi hasa waweza kupata taarifa sahihi. Mbinu zifuatazo ni matokeo ya uchambuzi wa tafiti mbalimbali na zinaweza kukupunguzia changamoto ya kupoteza muda na nguvu nyingi kutafuta kazi mtandaoni.

Picha: Makala hii kwenye gazeti la Mwananchi
Hakikisha unaonekana mtandaoni

Kuna faida kubwa ya kuonekana mtandaoni. Kwanza, inakuwa rahisi kwa waajiri kukuona wanapotafuta ‘kimya kimya’ mtu mwenye sifa wanazozihitaji. Aidha, inakusaidia kufuatwa na taarifa za nafasi za kazi pale zinapopatikana bila wewe kutumia nguvu kubwa kuzitafuta.

Ili kupatikana mtandaoni, kwa mfano, waweza kujiunga na mtandao maarufu wa LinkedIn unaotumika kama wasifu huru wa mtandaoni kwa watu wanaotengeneza mitandao ya kikazi. Fikiria kujiunga na mtandao huu.

Unapokuwa kwenye mtandao huu wa LinkedIn ni vyema kuweka taarifa zinazokusaidia kukukutanisha na watu unaowalenga na jitahidi kushiriki mijadala inayoendana na malengo yako. Kufanya hivi  kutakusaidia kufahamika na watu wanaoweza kukuunganisha na nafsi za kazi pale zinapotokea.

Kadhalika, upo mtandao mzuri wa kijamii uitwao Twitter. Faida ya mtandao huu ni utamaduni wa watumiaji wake kuufanya kuwa wa kikazi zaidi na hivyo unatumiwa na wataalam wa kada mbalimbali. Unapoweza kuutumia vizuri kujadili masuala unayoyaelewa vyema na uliyo na utaalam nayo, itakuwa rahisi kuonekana na watu ambao katika hali ya kawaida usingeweza kukutana nao.

Tafuta tovuti zinazoaminika

Si kila tovuti zinazotoa taarifa za kazi mtandaoni zinaweza kuaminika. Kama  ilivyo kwenye maisha halisi, mitandaoni pia wamo watu wenye nia ya kutumia shida za watu kujitafutia kipato. Utakumbuka hivi majuzi zilienezwa taarifa potofu kuwa serikali ilikuwa imetangaza nafasi nyingi za kazi. Ilibidi mamlaka zinazohusika kukanusha taarifa hizi.

Mambo kadhaa yanayoweza kukusaidia kufahamu ikiwa taarifa za kazi unazozipata mtandaoni ni sahihi ama la. Kwa mfano, hakikisha tovuti ya taasisi au kampuni inayodaiwa kutangaza nafasi za kazi kweli inapatikana mtandaoni na inalo tangazo hilo. 

Haiwezekani idara au taasisi makini itoe tangazo la kazi na ifanye kosa la kutokuweka taarifa hizo kwenye tovuti yake. Matangazo ya kazi yenye kuweka tovuti za waajiri zisizopatikana, mara nyingi huwekwa mtandaoni na watu wenye nia mbaya.

Hakikisha taarifa unazotaka kuzifanyia kazi ni rasmi kabla kujaamua kuchukua hatua yoyote ya kuomba kazi husika. Usifanye haraka kuamini na kufanyia kazi taarifa zinazopatikana kwenye tovuti/blogu zisizothibitishwa. Kazi zinazotangazwa na idara na mashirika ya umma, kwa mfano, ni lazima zipatikane katika tovuti rasmi za serikali.

Jambo la pili, hakuna taasisi inaweza kutangaza nafasi za kazi mtandaoni na zikudai fedha ili uitwe kwenye usaili. Unapokutana na madai yoyote ya ada, elewa kinachoendelea. Aidha, wakati mwingine, si tu waweza kuombwa kiasi cha fedha, lakini pia waweza kuombwa taarifa zako binafsi na nyeti kwa madai ya kuwezesha mchakato wa kuomba kazi.

Vile vile, ni lazima tangazo la kazi lioneshe mawasiliano yanayoeleweka kama vile barua pepe rasmi zenye ‘domain’ zinazofanana na majina ya taasisi husika. Unapokutana na taarifa muhimu zisizoambatana na mawasiliano yasiyo rasmi, mfano barua pepe ya ‘gmail’, ‘yahoo’, ‘hotmail’ na nyinginezo, fikiria mara mbili.

Ingawa ni kweli katika mazingira yetu taasisi na idara nyingi zinaweza kutumia barua pepe zisizorasmi, ni muhimu, hata hivyo, kuhakiki mambo mengine muhimu kama namba za simu, nukushi na anuani ya posta. Hayo yote ni kujaribu kujiridhisha kabla hujawekeza nguvu zako kuomba kazi isiyokuwepo.

Fahamu unataka nini

Mtandao wa intaneti una kila aina ya taarifa. Unapotafuta kitu usichokuwa na uhakika nacho mtandaoni ni rahisi kuchanganyikiwa na hivyo unaweza usifikie malengo yako. Ni muhimu kuamua unatafuta kazi gani kutoka kwa waajiri gani na wapi ili uweze kuelekeza nguvu zako kwenye lengo mahsusi.

Kwa mfano, kama unatafuta kazi ya Uhasibu, usitumie muda wako kutafuta taarifa zisizohusiana na Uhasibu. Jikite kutafuta taarifa zinazohusiana na wasifu (ujuzi) wako.

Kadhalika, unapojua unahitaji kazi gani, itakuwa rahisi kwako kutafuta taarifa za taasisi au idara zinazoweza kukuajiri. Tembelea tovuti za waajiri unaowafikiria kujua ikiwa wameweka tangazo la kazi.

Kwa mfano, kama una lengo la kupata kazi katika kampuni za habari, unahitaji kuwa na tabia ya kufuatilia tovuti zao mara kwa mara. Maana, huko kwenye tovuti zao ndiko zinakopatikana taarifa rasmi.

Chukua tahadhari

Unahitaji kuwa makini na taarifa unazoweka mtandaoni. Fahamu kuwa mara unapoweka taarifa zako mtandaoni, unapoteza udhibiti wake na watu usiowafikiria wanaweza kuzitumia kwa malengo yoyote.


Kadhalika, taarifa zinazojenga taswira isiyokubalika katika jamii zinaweza kukuathiri katika safari yako ya kupata kazi itakayotimiza ndoto zako. Wapo waajiri wengi, kwa mfano, huchunguza taarifa za waomba kazi mtandaoni ili kufanya maamuzi.  Tafiti zinaonesha zaidi ya nusu ya waajiri hujaribu kupekua wasifu wako mtandaoni kabla hawajakuita kwenye usaili. Ndio kusema, ni bora usipatikane mtandaoni kuliko kujenga taswira itakayokuletea hasara.

Fuatilia Jarida la Kazi na Ajira ndani ya gazeti la Mwananchi kwa makala kama hizi.

Maoni

  1. Habar naitwa eddy Thomas natafuta ajila ya udereva ni mzowef sana hii kazi napatikana tabata atakyonihitaji namba zangu za simu number ni 0748657118 makubaliano yako nipigie mda wowote

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia

Pay $900? I quit blogging