Tunayopaswa Kuyafahamu Kuhusu Shule za Msingi za Bweni

Katika miaka ya hivi karibuni, shule za msingi za bweni zimekuwa maarufu. Kimsingi, si tu shule za msingi, lakini hata shule za awali za bweni. Hivi sasa, miji karibu yote katika nchi hii inazo shule kadhaa zinazopokea watoto wadogo na kuwasomesha kwa mfumo wa bweni.

Takwimu rasmi za hivi karibuni hazipatikani. Lakini kwa mujibu wa Wizara ya Elimu, mwaka 2012 nchi yetu ilikuwa na shule za msingi zipatazo 684 zenye huduma ya bweni. Shule hizi zinafahamika pia kama shule zinazotumia Kiingereza kama lugha rasmi ya kufundishia, yaani English Medium, zikimilikiwa na watu binafsi au taasisi zisizo za umma.

Kufikia mwaka 2013, mikoa yote kwa Tanzania bara, isipokuwa Lindi ilikuwa na shule hizi. Hata hivyo, mikoa inayoongoza kwa wingi wa shule za bweni ni Dar es Salaam, Arusha, Kilimanjaro na Mwanza.


Ongezeko kubwa la mahitaji ya shule hizi za bweni linaweza kuelezeka kwa sababu kadhaa. Mosi, ni matarajio makubwa waliyonayo wazazi kwa elimu ya watoto wao. Ukubwa wa matarajio hayo unachochea kufanyika kwa jitihada za kila namna katika kuhakikisha kuwa watoto wanapata elimu bora pengine kuliko ile waliyoipata wazazi.

Kwa kuwa mzazi angependa mwanae afanye vizuri kitaaluma, shule ya bweni inakuwa sehemu ya jawabu mujarabu. Kwa kumpeleka mtoto kwenye shule ya bweni, mzazi anaamini huko mtoto atajengewa mazingira ya kumsukuma kujifunza bila bughudha.

Aidha, kuna suala la changamoto za kimalezi wanazokabiliana nazo wazazi. Migororo ya kifamilia inayozorotesha mahusiano baina ya wazazi, huweza kusababisha uhitaji wa shule ya bweni kwa nia ya kumlinda mtoto na matatizo yasiyomhusu. Katika mazingira haya, inawezekana wazazi wasingependa kukaa mbali na watoto lakini wakijikuta hawana uchaguzi mwingine bora zaidi ya kumpeleka mtoto katika shule ya bweni.

Kadhalika, yapo mazingira ambayo wazazi hawawezi kuwa karibu na watoto wao. Aina ya kazi wanazofanya wazazi zinaweza kuwafanya washindwe kuwapa watoto huduma za karibu. Katika mazingira ambayo wazazi wanalazimika kuwa nje ya familia kwa muda mrefu kwa sababu za kikazi, shule ya bweni inakuwa mbadala wenye unafuu.

Shule hizi, hata hivyo, zimepigwa marufuku kwenye nchi nyingi ikiwemo Rwanda. Hata hapa kwetu, mwaka 2015, serikali kupitia Wizara ya Elimu iliwaonya wazazi juu ya hatari ya kuwapeleka watoto wadogo kusoma kwenye shule za bweni. Hoja ni uwezekano wa watoto hawa wadogo kiumri kupatwa na madhara anuai ya kitabia yanayotokana na mazingira ya bweni. Tamko hili rasmi lilizingatia ukweli kuwa katika siku za hivi karibuni kumekuwepo ongezeko kubwa la shule za bweni.

Tunapozungumzia shule za msingi za bweni, kimsingi, tunazungumzia shule zinazopokea watoto wadogo kuanzia miaka mitatu hadi 12 wanaotengwa na familia zao kwa lengo la kuwapatia elimu inayokwenda sambamba na malezi.

Mtoto huyu, kwa kawaida, hukabidhiwa kwa mamlaka za shule na hukaa mbali na familia yake kwa muda unaoweza kufikia na hata kuzidi miezi saba kwa mwaka. Katika kipindi chote hiki, mtoto huishi na watoto wenzake shuleni chini ya uangalizi wa walezi na walimu. Wazazi na ndugu wanaotambuliwa na uongozi wa shule ya bweni huruhusiwa kumtembelea mtoto.

Tafiti zilizofanyika

Hakuna tafiti nyingi zimefanyika kuchunguza shule hizi katika mazingira yetu. Hata hivyo, mwaka 2015 mwandishi wa makala haya alifanya utafiti katika shule hizi za msingi za bweni. Lengo la utafiti huo uliokuwa sehemu ya tunuku ya kitaaluma lilikuwa kulinganisha mazingira ya kimalezi katika shule hizo na yale ya nyumbani wanakoishi watoto.

Watoto waliokuwa wakisoma kwenye shule moja kwa mfumo wa kutwa na bweni wenye umri wa miaka sita kwa darasa la kwanza na miaka saba kwa darasa la pili walilinganishwa kwenye maeneo makuu manne kama ifuatavyo; umahiri wao kiakili na kitaaluma kama vile uwezo wa lugha, kuhesabu, kuandika; tabia mahususi za watoto mfano namna wanavyojiamini, mahusiano yao na wengine; aina ya malezi wanayoyapata watoto na namna mazingira hayo yanavyowasaidia watoto kujenga uwezo wa kujitegemea.

Itakumbukwa kuwa katika siku za nyuma hapakuwa na utamaduni huu wa kuwapeleka watoto wadogo kusoma mbali na familia zao. Tulizoea kuona watoto angalau wenye miaka kuanzia 13 na kuendelea wakipelekwa kwenye shule za sekondari za bweni. Mambo yamebadilika.

Kama tulivyokwisha kubainisha, pamekuwa na ongezeko la mahitaji ya shule hizi kwa ngazi ya chekechea na madarasa ya awali. Hata hivyo, hakuna ushahidi wa kiutafiti unaoweza kuwasaidia wazazi kufanya maamuzi sahihi wanapofikiria kuwapeleka watoto wao  kwenye shule hizi.

Utafiti uliotajwa ulilenga kuchunguza kwa kiasi gani mazingira ya bweni kwa watoto wadogo wa miaka sita na saba yanaweza kufanana au kutofautiana na mazingira ya nyumbani ambayo wengi tunayafahamu.

Mazingira sisimushi kitaaluma

Shule za bweni zilizohusishwa katika utafiti huo zilionekana kuwa na mazingira bora zaidi kitaaluma ukilinganisha na mazingira ya nyumbani wanakoishi watoto. Upimaji wa umahiri wa watoto kiakili na kitaaluma ulionesha wazi kuwa, kwa ujumla, watoto wa bweni walikuwa na uwezo mzuri wa kitaaluma.

Kwa watoto wa miaka sita, ilionekana kuna tofauti kubwa kati ya watoto wa bweni na wenzao wanaosoma kwa mfumo wa kutwa. Hata hivyo, tofauti hiyo ilikuwa ndogo kwa watoto wa darasa la pili mwenye miaka saba.

Katika kuchunguza sababu za tofauti hiyo, mambo kadhaa yalijitokeza. Kwanza, kuwepo ratiba isiyobadilika kwa watoto wa bweni. Mtoto anayelala shule, kwa mfano, alikuwa na uwezo wa kujua wakati upi anapaswa kufanya nini kuanzia anapoamka mpaka anapokwenda kulala. Mtoto anayejua utaratibu anaopaswa kuufuata kwa siku anakuwa na utulivu wa kiakili kuliko mwenzake asiyejua kitu gani kitafanyika wakati gani.


Inaendelea 

Maoni

  1. Ahsante sana Mr Christian Bwaya kwa makala hii

    JibuFuta
  2. Ahsante sana Mr Christian Bwaya kwa makala hii

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia