Usidanganyike. Wema huanzia nyumbani.


Umewahi kukutana na mtu mwema kiasi kwamba unawaonea ‘wivu’ familia yake? Unajiuliza, “kama huyu jamaa anaweza kuwa mkarimu hivi kwa sisi wapita njia tusiomhusu kivile, nyumbani kwake si watakuwa wanamfaidi sana?” Sasa usinielewe vibaya. Silengi kukukatisha tamaa. Ni vile tu nimeshangazwa hivi majuzi.

 

Godi ni rafiki yangu wa siku nyingi. Kwa hulka, ni mtu mchangamfu mwenye wingi wa bashasha. Kaa na Godi mzungumze utapenda namna yake ya kuzungumzia masuala. Godi anajua aseme nini wapi na kwa nani.

 

Halafu kuna wema. Godi hasubiri umtafute. Haipiti wiki hajakupigia na wala hatakuuliza kwa nini humpigii. Hivyo. Ukiwa na shida, Godi huyu hapa. Hana uwezo sana kifedha. Maisha yake ni haya haya kama ya wengi wetu. Sema ni ule utajiri tu wa roho ya mtu. Usha’nfahamu? Godi. Ukiniuliza mtu mwema nimewahi kukutana naye, nitakwambia Godi bila hata kupepesa macho.

 

Jamaa yetu mmoja aliwahi kumsifia kiutani lakini alikuwa sahihi. Kwa jinsi alivyo mwema, jamaa alisema, Godi anaweza asiwe na hata mia ya kukupa lakini akaenda kukukopea mahali kusudi akunusuru na dharura. Huyo ndio Godi. Mwema kupindukia.

 

Saa nyingine unajiuliza, mtu anaanzaje kuwa mwema vile? Dini. Wengine wanaziona dini kama vyama vya kujenga himaya kwa mwamvuli wa imani. Mie niko tofauti. Dini ni ule ucha Mungu unaojenga wema usiowa maigizo.. Ndio Godi huyo. Ukifungua kibegi chake hukosi machapisho ya dini. Hakosi ibadani. Halafu sasa sio tu ni mtu wa makanisa kanisa, Godi anachapa kazi. Naambiwa kazini kwake ukitaka shughuli iende na matokeo yaonekane mpe Godi. Nadhani umepata picha kidogo.

 

Sasa juzi mke wake kanitafuta analia. “Shemeji nini?”nikamwuuliza kwa wasiwasi. Kwikwi kwa mbali. “Ongea na rafiki yako Godi. Naondoka,” shemeji ananichanganya. “Unaondoka? Unakwenda wapi shemeji?” nauliza kama mtu nisiyejielewa. “Nimechoka shemeji. Bora nife.” Kha! Imekuwaje tena shemeji anathubutu hata kufikiria mambo ya kujitoa roho wakati hata matokeo ya sensa hayajatoka. Kuna nini?

 

Shemeji, mke wake na Godi, anafunguka. Nabaki kinywa wazi. Sijui nimwambie nini zaidi ya kuitikia. Mama kateseka sana yule. Nabaki kishangaa. Godi kawa lini mkatili vile nyumbani? “Nimechoka maisha ya maigizo shemeji. Nimeishi maisha ya ujane muda mrefu. Bora niende kwetu. Nimesema nimechoka.”

 

Godi huyu huyu? Naona aibu maana ni kama nimedanganyika muda mrefu: “Hatuongei miaka na miaka. Hatuwezi kutulia mahali tuzungumze kitu kinachoeleweka. Godi hakamatiki nyumbani. Hajali la mtu sio mimi sio mtoto. Juzi mtoto kaugua usiku. Baba ni kama hayupo. “Usipaniki homa itaka yenyewe?” Ndio kitu cha maana alichosema. Muda wote anacheka na watu kwenye simu. Hana habari na mtu humu ndani.”

 

Lahaula. Naogopa ninayoyasikia. “Shemeji, hatulali chumba kimoja muda mrefu.” Jamaa yangu amekuwaje tena? “Kutwa kusafiri utafikiri anafuatilia kitu cha maana. Kumbe ni wanamke.” Godi huyu huyu anayetembea na vitabu vya Tumwimbie Bwana kwenye mkoba?

 

Nikajifunza mambo mawili makubwa. Kwanza, tabasamu halisi la mwanaume linaanzia nyumbani. Usidanganywe na watu wachangamfu kwenye makundi sogozi mitandaoni. Bashasha la mwanaume wa ukweli linaanzia nyumbani. Uungwana wa halisi wa mtu sio huu tunaouona mitaani. Uungawana halisi wa mtu ni vile anavyoishi na watu wa nyumbani kwake. Hao ndio watu wanaomjua ndani nje. Hao ndio wanaweza kukwambia undani wa mtu.

 

Lakini kingine, nikagundua kumbe watu tunaishi kitalaam sana mjini. Si unajua dhana ya mtaji jamii? Nani atakuamini mjini usipovaa sura fulani? Unalazimika kuchekea mpaka wapitia njia, unagawa tipu kwa wahudumu, unajua usipofanya hivyo, wasifu wako mjini utajitia doa. Tunaishi kwenye dunia ya kibepari. Ukiharibu jina mjini utajikosesha vingi. Sasa hapo ndo’ unakutana na hizi sura ‘bora’ za watu zinazoonekana maofisini, makazini, ibadani. Lengo, mara nyingi, ni kuwezesha mipango yetu iende.

 

Nategemea kukutana na Godi nisikie anasemaje. Lakini wakati tunasubiri kumsikiliza Godi mwenyewe, nimegundua watu wengi hutafuta sana kuaminiwa na watu baki. Wanachasahau, masikini, imani inaanzia nyumbani. Unsha’nsoma? Ogopa sana mtu anayeweza kuumiza watu wa nyumbani kwake na wala haonekani kujali. Rudia sentensi hiyo.


Niandikie: bwaya@learninginspire.co.tz


Maoni

  1. Asante kwa darasa zuri

    JibuFuta
  2. Hii ni kweli kabisa, na inaumiza sana, kuna haja ya kujihoji na kubadilika

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Tumia Mbinu Hizi Kuelewa Unachokisoma -3

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia

Haiba ni nini?