Fikiria Yafuatayo Unapoomba Nafasi ya Kujiunga na Chuo Kikuu

  PICHA: HuffPost


Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) imeviruhusu vyuo vikuu hapa nchini kuanza zoezi la kupokea maombi ya wanafunzi kwa mwaka wa masomo wa 2017/2018. Katika kufanikisha zoezi hilo, tume imewaelekeza wanafunzi wanaofikiri wana sifa za kujiunga na elimu ya juu, kutuma maombi yao kupitia vyuo husika tofauti na ilivyokuwa awali. Kabla ya utaratibu huu mpya, wanafunzi walituma maombi kupitia mfumo wa udahili wa pamoja uliokuwa ukiratibiwa na tume yenyewe.

Kwa hakika mchakato huu wa udahili una umuhimu mkubwa kwa wanafunzi. Maamuzi ya aina ya programu ambayo mwanafunzi ataichagua na kisha kuisomea endapo atapata nafasi, kwa kiasi kikubwa, inaamua mustakabali wake wa kazi na ajira.

Bahati mbaya maamuzi haya muhimu, mara nyingi, hufanyika bila tafakari ya kina, pupa na kufuata mkumbo. Hatima ya yote ni mwanafunzi kuwa kwenye hatari ya kupoteza ndoto zake za maisha.

Naelewa changamoto hii kwa sababu na mimi yalinikuta. Nilipokuwa nafikiri nikasome nini chuo kikuu, nilipata shida ya kujua ninataka nini. Niliongozwa na maoni ya marafiki, walimu na watu wa mitaani. Matokeo yake hayakuwa mazuri. Baada ya miaka kadhaa ya kusoma nilichokisoma, bado nilijisikia kama mtu aliyepotea. Ilinilazimu kufanya maamuzi magumu kurudi kwenye njia yangu nilipopata fursa ya kusoma shahada ya shahada ya pili.

Kwa vijana wengi, kama nilivyokuwa mimi, maamuzi ya nini akasome chuo cikuu hutegemea maoni ya watu ambao wakati mwingine hawana taarifa za kutosha kumsaidia kufanya maamuzi sahihi. Makala haya yanalenga kumsaidia kijana, na hata mzazi, anayejiandaa kwenda kusoma. Tunaangazia mambo manne makubwa ya kuzingatia katika mchakato huu.

Una nini ndani yako?

Kila mtu ameumbwa kwa upekee wake. Ndani ya kila mtu kuna uwezo unaomtofautisha na binadamu wengine. Uwezo huu ndio unaobeba mafanikio ya mtu. Ni muhimu uwe na hakika kitu gani hasa ambacho Mwenyezi Mungu amekihifadhi ndani yako. Maamuzi yoyote unayoyafanya hivi sasa ni vyema yahakikishe elimu utakayoipata inakuza kitu hicho kilichomo ndani yako.

Bahati mbaya vijana wengi huwa hawatumii muda wa kutosha kujitambua wana kitu gani ndani yao. Kutokujua wao ni akina nani kunawafanya watumie muda mwingi kusikiliza maoni ya watu, kujua nini kinalipa vyuoni, soko linataka nini na matarajio ya jumla ya jamii.

Sababu hizi ni za muhimu lakini haziwezi kukusaidia. Ingawa kwa sasa unaweza kuwa na msisimko wa kusoma fani unayofikiri itakuletea heshima kwa jamii, baada ya muda hutaona faida yake. Sababu kubwa ni kwamba elimu isipokuza kile kilichomo ndani yao, haiwezi kukusaidia. Jitahidi kujitambua kabla kujafanya maamuzi ya nini ukasome.

Changamoto, hata hivyo, ni kwamba wakati mwingine kile tunachofikiri kiko ndani yetu kinaweza kuwa kimeumbwa na matarajio ya watu. Ni muhimu kutafuta ushauri makini kwa wataalam wakusaidie kujitambua.

Unataka kufanya nini baadae?

Sambamba na kujua kuna nini ndani yako, ni muhimu kujua kwa nini unataka kusoma. Usisome tu kwa sababu na wewe unataka uonekane msomi. Fahamu kwa yakini lengo lako la kwenda chuo. Je, unataka kuajiriwa baada ya masomo au unalenga kujiajiri?

Ukweli ni kwamba tunatofautiana. Ni makosa kufikiri watu wote wanaweza kujiajiri. Kwa wakati wowote, kokote, bado watakuwepo watu ambao mafanikio yao yatapatikana kwenye ajira. Hawa, hata ungewawekea mazingira ya kujiajiri, bado furaha yao inatimilika kwa kufanya kazi chini ya watu wengine. Hakuna ubaya kutaka kuajiriwa na usikatishwe tamaa na watu.

Ikiwa unataka kuajiriwa baada ya masomo, lazima ulenge kusoma fani zinazokuelekeza kwenye kazi mahususi. Ningependa kuziita fani hizi ‘kozi za kazi,’ mfano sheria, uinjinia, ualimu, uhasibu, uandishi wa habari, udaktari na nyinginezo. Ukisoma ualimu, unasomea kazi kuliko kusoma program za jumla ambazo wakati mwingine hazieleweki zinakuandaa kufanya kazi gani hasa.

Pia, ikiwa lengo lako ni kujiajiri, lenga kusoma fani itakayokusaidia kupata maarifa yatakayokusaidia kusimama kwa miguu yako kukujengea uwezo thabiti wa kutatua matatizo fulani kwenye jamii.

Soma kozi zinazokujengea ujuzi fulani utakayokuwa na tija kwenye shughuli zako. Mfano, ukisoma fani kama uendeshaji wa biashara, ufundi wa kompyuta, utunzaji wa mazingira, lugha, kilimo, sosholojia, uwezekano ni mkubwa utaandaliwa kuwa mjasiria mali kuliko kusomea fani zinazokuandaa kufanya kazi ofisini.

Pamoja na hayo, ieleweke kwamba elimu ya chuo kikuu hailengi kukuandaa kujiajiri moja kwa moja. Kazi ya kuyageuza maarifa unayoyapata darasani yewe ufanisi wa kazi inabaki kuwa ya kwako mwenyewe. Unahitaji kuwa na mtazamo mpana tangu unapoanza chuo ili upate kile unachokihitaji kulingana na mahitaji yako.

Umaarufu wa shahada

Kuna rafiki yangu mmoja aliwahi kuomba kusoma shahada moja kwa sababu tu ilikuwa na jina zuri kutamkika. Alipomaliza wiki ya kwanza darasani, akagundua haimfai. Alijaribu kufanya mipango  ya kubadilisha, lakini haikuwezekana.

Fikiria mwanafunzi kama huyu anayesoma kitu asichoona kinahusianaje na maisha yake ya baadae. Kwanza, hatakuwa na bidii, hatajituma na hatakuwa na ubunifu wowote kwenye fani husika.

Mtu kama huyu akimaliza chuo anaweza kuulalamikia mfumo wa elimu kwa sababu ni kweli kile alichokisoma hakijamnufaisha kibinafsi. Atajikuta ametumia muda mwingi kusoma mambo yasiyohusiana na wito wake, ambayo kwa bahati mbaya hayawezi kusaidia kutatua tatizo lolote kwenye jamii, na mbaya zaidi, hayawezi kumpa ajira. Mtu huyu anaweza kuishia kuwa mchuuzi wa bidhaa mitaani, na kuyalaani madarasa kwa kosa alilolifanya yeye mwenyewe.

Naelewa yapo mazingira ambayo mtu anaweza kujikuta akisoma kitu ambacho hayawahi kukifikiri. Kuna shinikizo la wazazi, kuna shinikizo la kupata mkopo na sababu nyinginezo. Katika mazingira kama haya, ni vyema kuelewa kwamba bado unaweza kutumia shahada usiyoipenda kufikia kile unachokipenda. Ndivyo maisha yalivyo nyakazi nyingine.

Ukasome chuo gani?

Nimebahatika kusoma na kufanya kazi kwenye vyuo vikuu tofauti. Nilichokibaini ni kwamba si kila king’aacho ni dhahabu. Vipo vyuo vinasifika kwa majina lakini sifa hizo hazitafsiriki kwenye ubora wa kile wanachokipata wanafunzi. Usiongozwe na historia ya vyuo vilivyowahi kuwa bora kwa siku za nyuma.

Jina la chuo linaweza kuwavutia watu, na wakati mwingine kukujengea ufahari mtaani lakini kamwe halitakuhakikishia utendaji bora wa kazi. Katika siku za leo, ujuzi ni jambo la maana zaidi. Kazini watu hawatajali ulisoma wapi. Watataka kuona matokeo ya kile ulichokisoma. Hilo ndilo la muhimu. Usipumbazwe na mashindano ya chuo gani ni bora kihistoria.

Pia, ni muhimu kuelewa kuwa kila chuo kina fani inayokitambulisha vizuri kuliko fani nyinginezo. Chuo kinaweza kuwa maarufu katika kuwaandaa wanasheria mahiri, lakini kisiweze kuwaandaa walimu bora. Ni muhimu kufanya utafiti kwa kuongea na watu wanaoaminika ili ufanye maamuzi sahihi.


Hata hivyo, bado ubora wa jumla wa chuo ni jambo la muhimu. Hakikisha chuo unachokwenda kusoma, mbali na kuwa na wahadhiri wa kutosha na wanaojituma, miundomsingi, ubora wa afunzo kwa vitendo, usimamizi wa karibu wa wanafunzi, hakikisha pia kinaweza kukupa mazingira ya kukulea kimaadili.

Makala haya yalichapishwa kwenye gazeti la Mwananchi, Ijumaa ya tarehe 4 Agosti, 2017.

Maoni

  1. Daah hakika yame tukuta wengi,

    JibuFuta
  2. Haya mambo mwalimu Yametukuta wengi na bila shaka kila makala unayoandika Mr Christian Bwaya huwa nakuwa nishakurupuk kwa hulka za Wanajamii,,,,, na kumbuka kuna makala ushawahi eleza kuhusu Mambo ya kuzi gatia kabla ya kuacha kazi nilijikuta nimefanya makosa kibao zaidi Ahsante kwa hilo ngoja niwape sharing watanzania wengine

    JibuFuta
  3. Haya mambo mwalimu Yametukuta wengi na bila shaka kila makala unayoandika Mr Christian Bwaya huwa nakuwa nishakurupuk kwa hulka za Wanajamii,,,,, na kumbuka kuna makala ushawahi eleza kuhusu Mambo ya kuzi gatia kabla ya kuacha kazi nilijikuta nimefanya makosa kibao zaidi Ahsante kwa hilo ngoja niwape sharing watanzania wengine

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia