Soma maoni ya msomaji: Uislamu ulikuwepo tangu mwanzo

Namshukuru msomaji(ambaye hakutaja jina lake) kutupa maoni yake kuhusu hoja ya lini hasa Uislamu ulianza. Ikumbukwe, lengo hasa ni kujadiliana na si mabishano kama baadhi ya wasomaji walivyofikiri (Poleni nyote mliolalamika kwa SMS na e-mail).

Hapa ni majibu ya msomaji huyo katika suala hilo:

"...Salamu(amani) juu yenu. Naomba watu wafahamu ya kuwa uislamu si dini iliyopewa jina na muasisi fulani na kusema kuwa wafuasi wake waitwe waislamu, la hasha, bali Uislamu jina hili ukilitafsiri kwa lugha ya kiswahili ni amani, kujisalimisha, kunyenyekea ndiyo maana yake.

Mtume Muhammad (S.A.W) si muanzilishi wa dini hii, na emeeleza wazi kuwa uislamu upo yaani (kujisalimisha kwa Mungu) toka kuumbwa kwa ulimwengu. Allah aliumba ulimwengu ili vitu vyote vimtii na kujisalimisha kwake, lakini viumbe hawa wawili (majini na watu) walipewa khiari na matamanio, na huo ndiyo mtihani wenyewe tulioumbiwa nao, ambao watu tunaelekezana, kuelimishana, kujadiliana, kuzozana mpaka tunafikia hata kugombana na kutoana roho katika mambo hayo.

Ni kwamba watu walioishi mwanzo walikuwa na mfumo wao wa maisha walipewa muongozo wa kuishi na Muumba kwa kuwapelekea mjumbe kutoka kwake, hivyo basi kutokana na vitabu vya dini havipingani kabisa kuwa Adam na Hawa(Eva) walipewa muongozo na Allah na kuambiwa wasiukaribie mtu huo walioukatazwa, kwa kuwa walikuwa na khiari na matamanio ndiyo yaliyowafanya walikhalifu amri hiyo na kutokea yaliyotokea kwa kuwa walikuwa wanyenyekevu wakaomba msamaha na hatimaye wakasamehewa, siyo kama Ibilisi(Shetani) ambaye hakuwa mnyenyekevu na kuangamia.

Watu wasifikirie Uislamu ni dini ya Muahammad (S.A.W) na kwa ajili ya waarabu tu, hapan kwani tukisoma historia ya kiislamu tunamkuta Bilal (R.A) muadhini wa mtume ambaye alikuwa muahabesh(muafrika), tunamsoma Salman Farsi (R.A) ambaye ni mfarsi(Muiran), kuna wakina Bukhari watu kutoka sehemu za Urusi na Mayahudi wengi tu waliosilimu. Mtume alilingania dini hii kwa wafalme wengi tu wa pande za ulimwengu. Kwa hiyo Uislamu ulikuwepo kutoka kuumbwa kwa dunia na mpaka mwisho wake.

Dini nyingine huenda zilikuwa ni za usahihi kutoka kwa Allah ila baada ya kupita muda baadhi ya watu waliharibu dini hizo ikiwa kwa ujinga au maslahi yao binafsi. Ikiwa Allah kaumba ulimwengu na vilivyomo ndani yake hivyo hahitaji chochote kutoka kwetu, isipokuwa unyenyekevu wetu tu, na huo ndiyo Uislamu wenyewe, na kitu kikubwa ni kumpwekesha yeye tu bila ya kumfanyia ushirika. Na huo ndiyo ulikuwa ujumbe wa mitume wa Mungu.

Uislamu si jina la mtu au mahala au kitu bali ni kitendo cha mtu kujisalimisha, kunyenyekea kwa Muumba na haikuanzishwa na mtu bali ni mfumo wa Allah aliouweka kwa waja wake ambao wanataka kufaulu duniani na akhera. Shukrani..."

Nakushukuru sana kwa maoni yako.

Maoni

  1. Alichokifanya msomaji wako ni kuchezea maneno ili kuufanya Uislam ueleweke vinginevyo.Uislam unabaki kuwa dini ya waarabu kwa ajili ya waarabu.

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Pay $900? I quit blogging

Haiba ni nini?

Heri ya mwezi mpya!