Saturday, July 2, 2011

CHANGAMOTO Insha za Jamii - Prof. Mbele



Natamani sana kukisoma kitabu hiki. Ninakitafuta kwa bidii. Unajua kinakopatikana?
Mwandishi Profesa Mbele anasema kakiandika kusahihisha majungu kuhusu Mwalimu Nyerere. Msome hapa halafu uone kama unaweza kujishindia Dola 100!

Waweza pia kusoma majadiliano katika Jamii Forums yanayodurusu ikiwa wanaomkosoa Mwalimu Nyerere wana hoja.

Friday, June 24, 2011

Take the Risk cha Ben Carson



Ndio kwanza nimeanza kukisoma. Take the Risk: learning to identify, Choose and Live with accepatable Risk. Kimeandikwa na Mganga Ben Carson kwa msaada wa Gregg Lewis na kuchapishwa na Zondervan Publishing House mwaka 2008.

Kitabu kinaanza na masimulizi ya upasuaji mgumu uliofanyika Julai 2003 kuwatenganisha Ladan na Laleh, mapacha waliozaliwa wakiwa wameungana sehemu ya vichwa vyao. Mapacha hao hata hivyo walifariki dunia wakiwa na umri wa miaka 29 wakati upasuaji huo ukiendelea huko Singapore. Katika kitabu hiki, mwandishi anajaribu kutupatia somo lilitokana na Upasuaji huo.


Ladan na Laleh raia wa Iran muda mfupi kabla ya upasuaji huo uliofanyika Julai 2003.

Saturday, June 4, 2011

Elimu pasipo maandishi inawezekana?







Pamoja na ukweli kuwa wengi wetu tunayakwepa maandishi, lakini hiyo haimaanishi kuwa hatuna kiu ya kujifunza. Pichani, wananchi wa mjini Moshi wakionekana kuvutiwa na matumizi ya video katika kuelimika. Picha: Sayuni Philip

Sunday, May 29, 2011

Kuwa mwenye furaha ni uamuzi wako mwenyewe!

Ni mara ngapi umewahi kukutana na mtu aliyekukwaza kiasi cha kumtupa katika kapu la “watu wa hovyo” wasiostahili heshima kama binadamu? Umewahi kupatwa na tukio ambalo lilibadili kabisa mtazamo wako kuhusu maisha, watu na maisha kwa ujumla? Kwa nini watu kukata tamaa? Umewahi kuwaza kwa nini kinachomkwaza huyu si lazima kimkwaze yule?

Umewahi kuonana na mtu anayeshangaa inakuwaje “huyu bwana achukue uamuzi wa ajabu namna ile” wakati kilichotokea kinachukuliwa na wengi kuwa “ni jambo la kawaida”?

Natamani ukimaliza kusoma hapa uelewe kwamba sehemu kubwa ya matatizo tunayokabiliana nayo kama binadamu kila siku, tunayasababisha wenyewe. Na kwa yale tusiyo naudhibiti nayo, tunaweza kubadili mtazamo wetu kwayo, na hilo linaloonekana kuwa tatizo ama likawa si tatizo au likabadilika kuwa changamoto.

Wengi wetu tunapokumbana na vikwazo (ambavyo mara nyingi huwa ni watu, vile mambo yalivyo na matukio yanayokuwa katika namna tusiyoitegemea) hujenga mawazo kwamba vitu hivyo vi vibaya. Matokeo yake tunatumia muda mwingi sana kusononeka na hivyo kujikuta tukijiumiza sisi wenyewe zaidi na/au kuwaumiza wengine. Tunajikuta tukizalisha matatizo mengine ambayo kimsingi hatukuwa na sababu ya kuwa navyo, kwa sababu tu ya mtazamo.

Hasira, kukata tamaa, kuvunjika moyo, msongo wa mawazo na yote yanayofanana na hayo yanatupa ujumbe kwamba mwenye hayo anaamini kwamba yupo mtu, ama tukio, ama hali imemkosea! Hayo niliyoyataja huja kama matokeo ya mtazamo hasi. Huja kama matokeo ya tatizo letu wenyewe.


__________________________________________________
Mwanamke akifarijiwa baada ya tukio baya lililopoteza maisha ya watu kadhaa. Hapa tunaona tukio hilo hilo linapokelewa tofauti na watu hawa wawili. Picha: AP│Ilitumiwa mwanzo na telegraph.co.uk


Sijui kama unajua kuwa matukio yote yatokeayo katika uasili wake hayana uzuri ama ubaya? Una habari kwamba mengi kama sio yote anayoyafanya mwanadamu katika asili yake hayana uzuri ama ubaya? Unajua kuwa jinsi mambo yalivyo/situations katika uasili wake hayana ubaya wowote ama uzuri?

Pengine utaniuliza swali la kifalsafa: uzuri ni nini na unatofautianaje na ubaya? Ni bahati mbaya kwamba mazungumzo yetu ya leo hayana mwelekeo huo. Hata hivyo katika mipaka ya mazungumzo ya leo, uzuri tutaufafanua kama hali ya kupendeza wakati ubaya ni kinyume chake.

Kwa hiyo, hakuna kilicho katika uasili wake chenye uzuri ama ubaya. Naipenda kanuni hii, kwamba jinsi mambo yalivyo, watu, na matukio vyote hivyo ni neutral, havina uzuri wala ubaya! Uzuri ama ubaya wake hututegemea sisi! Hiyo ina maana kwamba ni mtazamo wetu sisi ndio huyageuza matukio, watu ama vile mambo yalivyo (situations) kuwa ama mabaya ama mazuri.

Nikifikiri kwa mtindo huo (kwamba uzuri ama ubaya wa lolote unanitegemea mimi na na sio kitu ama tukio) sikosi kugundua kuwa vingi vya vile vinavyonikesesha raha, utulivu na amani yangu vingeweza kabisa kufanya kazi tofauti kama ningebadili tu namna ninavyovichukulia.
Hebu fikiria ni misongo mingapi ya mawazo tunaisababisha wenyewe? Mara ngapi tumekosa amani na kukata tamaa kwa sababu tu “ya mtazamo wetu wenyewe”?
Mara ngapi tumejiumiza wenyewe kwa kuwawazia wapendwa wetu “ubaya” wasiokuwa nao kwa sababu tu tulijipa kazi ya “kuwabandika lebo ya ubaya”?

Najua yapo matukio ambayo kwa hali ya kawaida yanaweza kubadili kabisa “sripti” ya sehemu ya maisha yetu yaliyobaki. Matukio kama ya kufiwa na watu tuwapendao, kufukuzwa kazi na kadhalika. Lakini tunapotulia na kujibidiisha kubadili mitazamo yetu kwayo, twaweza kabisa kubaki na amani ya mioyo yetu na maisha yakaendelea!


Watoto wadogo huonekana kuwa na furaha kuliko watu wazima kwa sababu nyingi. Moja wapo ni kutokujua ubaya wa vingi vinavyowazunguka.

_______________________________________________________________________
Ipo orodha ndefu ya watu wanaotukosesha amani, tunaokosana nao kirahisi ama kukaripiana na kuvunjia heshima hadharani, ambao (kwa kubadili tu mitazamo yetu) tungeweza kabisa kuwapenda na kuishi nao kwa namna inayoweza kutushangaza sisi wenyewe!

Niliwahi kuishi na rafiki yangu mmoja siku za nyuma aliyekuwa na tabia za kunikera. Vingi vya alivyovipenda vilikuwa kinyume na yale yanayoitwa “maadili” yaani ethos. Majaribio ya mara kwa mara kuzungumza naye hayakusaidia kumbadili. Kila siku tuliyoishi naye ilioongezea hasira.

Ilinichukua muda kukubali kuwa yule rafiki yangu hakupenda kuwa vile alivyo. Kwamba alichokuwa akikifanya kilikuwa msukumo ulio nje ya uwezo wake mwenyewe. Hakupenda kuwa vile na hata kuamini alikuwa sahihi. Ni kwa kutambua hivyo, nikabaini kuwa kujaribu kumbadili hakutawezekana. Nikabaini kuwa anayo haki ya kuwa yeye. Na ni makosa mimi kujaribu kumgeuza yeye awe mimi.

Tangu kipindi kile, nilichokuwa nakiona awali kuwa kero kikabadilika kuwa sehemu ya maisha. Hatimaye nakumbuka ilikuja kuwa huzuni sana kuachana na rafiki yangu huyo tulipolazimika kutengana kimakazi. Kwa nini? Nilifanikiwa kubadili mtazamo wangu kwake na kusitisha “jaribio” la kumbadili yeye!

Huo ni mfano mdogo sana kutosha kukuelewesha namna ambavyo mara nyingi tatizo huwa kwetu tunaokwazwa, kuchukizwa na kuumizwa na wengine. Kwamba namna tunavyoyachukulia mambo huathiri sana “ubaya na uzuri wa jambo”.

Anza kuona uzuri wa watu wanaokuzunguka (hata kama itakubidi uutafute sana). Anza kuuchukulia udhaifu unaouona kwao kama tofauti baina yenu. Utashangaa.

Ni salama zaidi kuelewa kuwa mara nyingi watu hufanya mambo fulani kwa msukumo ulio juu ya uwezo wao. Msukumo huu ndani yetu hujengwa na vingi, kikubwa kikiwa ni mazingira tunayokutana nayo tangu dakika ile tunapozaliwa (malezi, dini/imani, marafiki nk) mpaka pale msukumo huo unapoota mizizi minene kiasi ya kutuongoza kutenda vile vinatenda!

Chukulia kuwa tofauti zetu si za hiari. Chukulia anayekuchukia hajapenda kukuchukia. Chukulia mengi ya yanayotokea kwa sababu ya uzembe wako, unayo nafasi ya kuyarekebisha.

Kumbuka amani na furaha yetu vyatutegemea sisi. Tusiwategemee wengine kutufanya tufurahi. Tupunguze matarajio kwa wengine. Tusiruhusu watu wengine kutunyima amani. Wajibu wa kujipa ama kujioondolea amani hauko kwa mwingine isipokuwa sisi. Uamuzi ni wetu wenyewe.

Monday, May 16, 2011

Wanablogu wanasemaje kuhusu utaratibu wa "Kutuzwa"?


Tangazo lilianzia hapa kwamba kuna mwuungwana -japo hakuwa anafahamika jina lake wala mahali aliko- kapata wazo la kutunuku kazi za wanablogu. Huenda hili bado halijulikani kwa wanablogu wengi kama ilivyokuwa kwangu kabla ya kusoma posti ya mwanablogu matata, Bw. Mubelwa Bandio juma lililopita.

Blogu ya mwandaaji wa Tuzo hizo inajinadi kwa maneno haya:

"...Our wish is to help bloggers to success, beat the odd and push past their limitation. We believe bloggers can play an important role keeping their places, villages, towns, cities or countries visible.
Tanzanian Blog Awards is another opportunity to showcase your blog to the world and get some free traffic and subscribers..."


Pamoja na kupongeza wazo hilo (la kuandaa tuzo kwa wanablogu), Mubelwa Bandio alionyesha wasiwasi wake ikiwa zoezi hilo litafanyika katika mazingira ambamo masuala ya msingi kuhusu blogu hayajafanyiwa kazi. Kwamba blogu zinaeleweka vyema kwa wadau (wateuzi na wateuliwa), hilo lilimtia mashaka. Je, ni kweli blogu pamoja na malengo yake, zinafahamika? Je, wanaouchagua "ubora" wa blogu, wanatumia tafsiri gani? Umaarufu ama maudhui?

Hoja nyingine ya Mubelwa ni ushirikishwaji wa walengwa. Mubelwa anashauri ingelikuwa bora kila mwanablogu angelijulishwa kinachoendelea:

"Ni vibaya kusema ni tuzo za blogu bora ilhali wapo wanao-blogu na hawajui kuwa kuna tuzo. Kwa hiyo waandaaji watafute orodha ya blogu zote ili kuhakikisha mnazijua.
Ninalopendekeza ni kuwa bloggers wote waandikiwe emails na kuuliza kuhusu CATEGORIES za blogu zao ili kuhakikisha kuwa kila blog inatambulika kuwa iko kwenye CATEGORY gani na kama itapendekezwa katika category isiyo, basi irekebishwe. Ni lazima blogs ziwekwe kwenye sehemu husika ili thamani ya tuzo iendane na category yake."


Zaidi ya hayo, Ndugu Mubelwa alihoji nafasi ya umoja katika zoezi hili. Soma zaidi hoja hizo kwa kirefu hapa.

Pamoja na maoni hayo, Mubelwa anaamini ikiwa ipo haja basi ya kutoa tuzo kwa mwanablogu yeyote Tanzania, ni vema kumpa heshima anayostahili Bw. Ndesanjo Macha, mwasisi wa blogu nchini. Itakumbukwa kwamba Ndesanjo Macha ndiye Mtanzania aliyetia kiberiti cha kwanza kuwasha moto wa blogu unawaka hivi sasa (kiasi cha wengine wetu kufikiria "kuzitunuku") kupitia jikomboe.blogspot.com aliyeianzisha mwaka 2004. Heshima kwa kwake.

Akijibu baadhi ya hoja zilizotolewa na Bw. Mubelwa Bandio, mwandaaji wa Tuzo hizo alianza kwa kubainisha kwamba hakubaliani na hoja zote hizo.

Kuhusu kushirikisha wadau wa zoezi lake, mwandaaji anasema:

"...unavyosema sijui tuwaandikie watu watueleze blog zao zinahusu nini. Kwa taaarifa yako kuna watu wengi wanablog lakini hawajui hata blog zao zinaelekea wapi. Kuna maswali tumetuna na kuna wengi wamesharudisha lakini nakwambia ni kama 50% ya waliorudisha mpaka sasa hivi hawajui blog zao zinahusu nini au wasomaji wa blog zao ni nani...Hivyo baada ya watu kuwakilisha blog zao tutakaa chini kuona kama kila blog iliyopitishwa inastahili kuwekwa katika hiyo category.".

Kuhusu umuhimu wa wahusika (wateuzi na wateuliwa) kuzifahamu blogu na dhima yake kwa jamii, mwandaaji anasema:

"
...unavyosema kabla ya tunzo kwanza tufundishane umuhimu wa blog kwa jamii…hilo sitakubaliana na wewe kabisa kwa vile mpaka leo kuna filamu hazina maudhui yeyote katika jamii zaidi ya kufurahisha tu. Na hilo utalikuta kwenye blog nyingi tu, sio zote zitakua za kufundisha jamii kuna blogs ambazo zitakua zinafurahisha tu lakini zote zitashirikishwa katika mashindano... Na sisi hapa hatutalazimishwa na mtu yeyote ni wajibu wetu kuiweka award yetu katika kiwango cha juu. Na uzuri wa award yetu ni kuwa watu wanaosoma hizi blogs ndio watakao chagua wenyewe... hapa kwetu ni people’s choice hata yule mtu ambaye amejitahidi sana kujitangaza na hakuonekana tunampa jukwaa la kuonekana."


Zaidi bonyeza hapa kusoma majibu hayo neno kwa neno.

Baada ya kukutana na habari za harakati za kuandaa tuzo hizo kwenye blogu ya Ndg. Mubelwa Bandio na ukurasa wake wa Facebook, baadhi ya wadau walikuwa na maoni yafuatayo:

Ndugu Baraka Mfunguo anashuku harakati hizi za kuandaa Tuzo na kuziunganisha na dalili za ufisadi:

"...Nadhani hajatoa majibu zaidi ya kuitetea hoja yake(yuko zaidi defensive). Kiukweli wazo la kuwa na tuzo ni zuri lakini ni vyema kila mtu akashirikishwa. Na pia ni vizuri kitu kama hicho kikawa wazi. Hata hivyo hoja ya kusema kwamba ni tuzo ...hilo zimetolewa kulingana na matakwa ya kundi fulani (wanabloga wanaokutana Dar) Si la msingi. Na hapa ninaamini kuna mbegu ya ufisadi inayopandikizwa ambayo inakuja kuleta mgawanyiko. Wapo wale wenye pesa ambao wanautumia mwanya huo kuwalaghai baadhi ya watu na baadaye kuwagawa na kundi lingine la watu. Matokeo yake ni chuki dhidi yetu lakini yeye anajua alichopata kwa makusudi anayoyajua."

Mfalme Mrope, mwendeshaji wa blogu ya Je, huu ni uungwana anahoji mchakato mzima:

Nani yuko kwenye kamati ya kuteua hizi blogs na ni nani mpiga kura na pia mpendekezaji ni nani na tangazo la hii kampeni lilitolewa lini? na ati? Michuzi iko kwenye best designed blogs?? HUH?

Yasinta Ngonyani, baada ya kunukuu kauli mbiu ya mwandishi wa makala hiyo, anahoji ni akina nani walifikia uamuzi huo:

Naungana na kaka Mrope nani alipiga kura? na nani aliamua kila kitu?...

Sophie Kessy anadhani wanablogu hatupendani na ndio maana tumeshindwa kuwa na umoja:

"Ni kweli hatuna umoja wana blogger hatupendani twachukiana na kupigana vikumbo ufanyike mkutano wa kuelimishwa kuwa wa moja mengine baadae kama imeweza kufika mahali wakateuliwa wana blog bora bila wengine kufaham lolote katika jambo hili kubwa linalo wahusu? mpaka hapo hakuna umoja wala ushirikiano hamuoni kuwa dalili ya mvua ni ma wingu?...cha msingi ni kwamba vigezo gani vinatumika washiriki wanatambuliwaje? wanachaguliwa kwa mtindo gani mpaka kushinda. ndugu zangu waandaaji ni vyema kujenga msingi ulio imara na bora wa umoja na ushirikishwaji tusije onekana wale wale ni mtazamo wangu mniwieradhi."

Prof. Masangu, mchambuzi mahiri wa masuala ya kijamii na kisiasa alikuwa na haya ya kusema:

Mimi nilipoona tangazo hili wala sikutaka kusema cho chote. Ingekuwa vizuri hao waandaaji wakajaribu kuwasiliana na wanablogu wote ili tukashirikishwa.


Kamala Lutanisibwa anashuku zoezi hilo analodhani linafahamika zaidi kwa watoa fedha kuliko walengwa (wanablogu):

"...wafanye wafanyavyo. sina cha kusema. Tanzania tuna utaratibu wa kutumia watu kupta miradi yetu. Angalia hata NGOs. Ziko NGOs za kushughulikia watu kibao lakini zinajulikana zaidi kwa watoa fedha kuliko walengwa. haka ni kaujanja ka wajanjakujinufaisha..."

Malkiory Matiya, mwanablogu wa Sauti ya mnyonge alifikia kutilia shaka malengo ya tuzo hiyo:

...Inashangaza kuona blogs ambazo ni chachu katika kuelimisha watanzania popote pale duniani, ndizo zimepigwa chini. Na zaidi ya yote zile blogs ambazo hufanya uchambuzi yakinifu katika masuala ya siasa, utawala bora nazo zimepigwa chini. Kuna kila sababu ya kutilia shaka Lengo, nia, madhumuni na vigezo vya tuzo hii.

Sambamba na Mubelwa Bandio, mwanablogu mwingine mkongwe Bw. Kamala Lutatinisibwa naye anaandika waraka mzito akiuelekeza kwa muandaaji wa tuzo hizo. Katika maandishi hayo, mwananablogu huyo anaonyesha mashaka yake kuhusu nia hasa ya hao wanaoandaa tuzo hizo kimya kimya pasipo kuwashirikisha wadau. Kamala anaenda mbali kwa kuhisi kwamba wanablogu sasa wanaanza kutumika kama daraja la watu kufikia malengo yao!

Kamala ana wasiwasi na namna blogu mpya zinavyochukua nafasi kuliko inavyotarajiwa.
Anasema:

"
sasa wamegroup bloggs vile waonavyo wao ndivyo visitahirivyo awards na sio kiuhalisia. blog mpya zimeshika nafasi nyingi za awards, sijui ni watu gani walikaa na kuamua walivyoamua. ni awards, ni tunzo 'kwetu ma-bloggers' japo kuwa hatujui hasa ni nani kapangilia na kuamua kutoa hizo tunzo"


Bofya hapa kusoma post hiyo.

Naye mwanablogu Yusuph Mcharia wa blogu ya Mtayarishaji, aliweka ufafanuzi alioupata kutoka kwa muandaaji huyo.

Alihoji ikiwa blogu ambazo ndizo msingi wa Tuzo hizo zinafahamika kwa anayeratibu zoezi hilo na ikiwa ipo nafasi ya Jumuiya ya "ma-blogger" katika zoezi hilo.

Majibu ni haya:

Blog zinazowekwa hapa tunaletewa na watu na zingine tunatafuta wenyewe. Hili shindano ndio limeanza na tuna kama week tatu tu. Hivyo bado tunajitahidi kutafuta blog ambazo hatujaweza kuzipata basi tuziweke humu. Na blog hizo sio lazima ziandikwe kwa kiswahili bali ziwe zimeandikwa na Mtanzania yeyote pale alipo ulimwenguni.

Kuhusu nafasi ya umoja wa blogu hizo wanazozishindanisha;

"...Sisi hatupo katika umoja wowote na wala hatujapata mwaliko wa umoja wowote. Hivyo kujibu maswali yako sitaweza kwa vile hatupo kwenye umoja wowote wa bloggers wa kitanzania wowote ule."

Unaweza kusoma majibu kamili ya mwandaaji huyo hapa kwa hisani ya Mtayarishaji.

Una maoni gani na zoezi hili kwa ujumla? Kuna tunachoweza kujifunza namna wenzetu wa hapo Kenya wanavyoweza kuendesha zoezi kama hili?

Tazama namna walivyoendesha zoezi lao mwaka 2006, ambapo Mtanzania mwenzetu, baba wa blogu za Tanzania Ndesanjo Macha alishinda Tuzo hizo. Je, kuna ladha ya wanablogu wenyewe kupitia Jumuiya inayotambulika ili kuendesha zoezi hilo kwa uwazi unaotakikana na hivyo kuondoa hisia zisizo za lazima kwamba "kuna jaribio la kutaka kuwatumia wanablogu kuijipatia kipato"?

Jielewe, usisubiri Kueleweshwa!

Sunday, April 3, 2011

What religion really means



Kimeandika yaliyo kinyume na imani yangu. Nakisoma. Mwandishi Karen Armstrong na kuchapishwa na Vintage 2010. Kinauzwa kwa Tsh 19,500.

Friday, March 11, 2011

Wakubwa wetu huko Ufaransa



Picha hii imechukuliwa kwenye ukumbi wa mijadala wa Jamii Forums ikiwaonyesha watawala wetu walipohudhuria mkutano huko Ufaransa.