Unajua kugombana bila kufukua makaburi?

Picha: pixabay


“Msitumie vibaya elimu zenu bwana,” Godi anaanzisha sogo kijiweni. Unamkumbuka? Kaona kukaa haitoshi. Kasimama kabisa. Mikono inapepea hewani kusisitiza hoja, “Haya mambo yameanza leo? Ndoa zilikuwepo tangu enzi na enzi na hapakuwa na shida. Sasa nyie leo mnasema eti sisi wanaume ndio hatujui mahitaji ya wanawake? Mbona wazee wetu hawakujua hayo yote na bado ndoa zilidumu.”

 

Siku hizi ukitaka kuwachokoza wanaume ongelea matukio ya wanawake kunyanyasika. Salu kakaa pembeni anausoma mchezo. Tabasamu lake linaunga mkono hoja.

 

Hata hivyo, naona naye uvumilivu umemshinda. Kaamua kuulinda uanamue, “Hizi harakati zenu za kuwabeba wanawake zitatuharibia ndoa. Mie nawaambieni. Mnawatetea sana wanawake na watapata vichwa kweli. Wakitushinda tuwaleteeni basi.” Joto limepanda. Hisia hizi za akina Salu si za kupuuza. Mgogoro unapotokea kwenye ndoa, anayebebeshwa mzigo wa kutokufanya wajibu wake, mara nyingi, ni mwanamke. Msikilize Peki anavyogongea muhuri dhana hiyo:

 

“Biblia imeshaeleza wazi. Enyi wanawake watiini waume zenu. Hakuna kisichoeleweka hapo. Ukishakosekana utii hakuna muujiza. Tena kuna mahali imesema mwanamke mpumbavu hubomoa ndoa yake kwa mikono yake mwenyewe. Sasa nyie ndio mnataka ionekane upumbavu wote ni wa mwanaume.”

 

Peki amesimika mtazamo wake kwenye imani. Tunamchokoza aseme anavyoelewa kifungu cha wajibu wa mume kumpenda mke wake. “Kwani yeye hajui nampenda? Niache hela nyumbani, nilipe bili zote na bado aseme simpendi? Tusichoshane bwana!”

 

Tunamwuuliza Peki ikiwa yale mapenzi ya uchumba bado anayo. Peki anashusha jazba kidogo. Dalili kuwa kakumbuka alivyobadilika. Enzi hizo anaanzisha uhusiano na dada aliyekuja kuwa mke wake asingeyasema hayo anayoyasema. Simu hazikuwa zinakatika kirahisi. Mitoko sana. Kwa kifupi, muda wote alipambana kiume kuonekana anajua mapenzi. Nini kimebadilika baada ya ndoa?

 

“Saa nyingine ni kwa vile ukishakuwa na mtu ndani unamzoea na unaanza kumchukulia poa,” Peki anajibu kinyonge. Majid anafafanua zaidi mabadiliko hayo, “Ni kwa vile tu hawa wanawake hawajisumbuagi kuelewa hali halisi. Ukishaoa kuna kuongezeka kwa majukumu. Fahari kubwa ya mwanaume inakuwa kuona familia haidhaliliki. Mwanaume wa ukweli anaelekeza nguvu kupambana kuweka chakula mezani. Sasa unategemea nini mambo yakiwa mengi hivyo?”

 

Godi kachangamka sasa. Majid kausemea moyo wake. Hajali anatafuna nyama. Maneno yanamponyoka, “Huo sasa ndio ukweli kabisa. Sasa mbona hamuwaambii wake zetu waelewe? Mtu unapambana kutwa nzima na kazi unapata wapi muda wa zile meseji za uchumba? Usipofanya hivyo wanaanza kusema unachepuka. Tuteteeni.” Kijiwe kinapooza kidogo. “Haya mabadiliko yanayoendana na umri yakieleweka vizuri migogoro itapungua.”Agenda imeungwa mkono.

 

“Lakini tusisahau. Hata mwanamke akielewa una majukumu mengi, hiyo haimfanyi asahau yale mahitaji yake ya kike. Njaa ya mwanamke kupendwa haiishi.”

 

“Hapo sasa nakubaliana na wewe. Hata ukijua huna ‘afu tatu mfukoni, bado njaa itauma. Njaa na kinachoendelea mfukoni havina uhusiano,” Peki analegeza msimamo na kuendelea, “Ujue hawa wake zetu nao saa nyingine ni kama watoto. Ukiacha kumdekeza dekeza basi anasahau mazuri yote unayoyafanya.”

 

“Kingine labda tujifunze kuwasiliana,” sehemu ya pili ya hoja inaanza. “Unaongeaje unapokuwa na hasira? Usiruhusu mazungumzo na mke wako ukiwa umekasirika. Hasira haina hekima. Ukikasirika unakuwa mbinafsi. Unajifikiria mwenyewe tu. Ukiona umekasirika, nyamaza. Huwezi kunyamaza ondoka.”

 

“Hiyo ngumu. Mimi huwa nikikasirika raha yangu ni kuongea ili uumie. Nikishaona umeumia natulia.” Tunacheka wote. Majid amekuwa mkweli. “Ukishafahamu hasira hukuchochea umwuumize mtu, unajifunza namna ya kumudu hasira zako.”

 

Hii kitu ilikuwa inanisumbua sana mwanzoni. Nikishakasirika ni kushambulia tu. Hasira ikiisha ninakuja kujuta nilichokisema. Niliharibu sana familia yangu kwa kulopoka maneno makali. Lakini baada nilitafuta msaada. Siku hizi angalau najua namna ya kugombana.

 

“Kwanza ninaelezea hisia zangu zaidi. Badala ya kumwekea mwenzangu maneno mdomoni mwake, ninaelezea namna jambo lilivyoniumiza mimi. Najielekeza kujisemea mimi na sio kushambulia.”

 

Lakini pia situmii maneno makali yanayoonesha kuwa aliyekosea hiyo ndio tabia yake. Maneno kama, ‘ndio tabia yako,’ ‘nakufahamu wewe’, ‘hii sio mara ya kwanza, ‘huniheshimu,’ huwa yanachochea huyo unayetaka akuelewe naye ajihami kwa kujibu mashambulizi. Hamuwezi kufika mwisho. Nimejifunza kutumia lugha inayoelezea kile tu kilichotugombanisha. Sifukui makaburi hata kama ningetamani niyafukue yanisaidie kujibu mapigo. 


“Kweli hatuachi kujifunza. Hivi kumbe sikuwa najua kugombana?” Peki anachomekea. Wote tunaangua kicheko. Majid kapaliwa. Hajui kucheka akiwa kagida.


Niandikie: bwaya@learninginspire.co.tz

 

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia