Mahusiano yenye ‘utulivu’ bila amani

Chanzo: stock.adobe.com
Hivi umewahi kutaka kumwambia mtu jambo unaloona ni muhimu lakini ukakosa namna nzuri ya kumwambia?Unatamani ujumbe ufike lakini maneno sahihi ya kuubeba huna. Unafanyaje?

Wengine huamua kuacha. Kuliko kumwuumiza mwenzako, huona bora mtu uugulie maumivu ndani kwa ndani. Mwingine hajali. Huamua bora ‘kutema nyongo’ hivyo hivyo bila kujali maumivu yatakayoyasababishwa na ujumbe. Wanachosahau, matokeo yanayotokana na kujiumiza kwa kuuzuia ujumbe yanaweza kuwa sawa na madhara ya kuuachia ujumbe kiholela bila kujali maumivu ya atakayeupokea.

 

Mawasiliano ni sayansi yenye nafasi nyeti katika mahusiano. Ukikosea kanuni, mawasiliano yana nguvu ya kuleta uharibifu mkubwa unaoweza kugharimu afya ya mahusiano. Mawasiliano ni sanaa pia. Namna unavyosema jambo ni muhimu wakati mwingine kuliko hata ujumbe wenyewe. Ukishindwa kuchagua maneno sahihi na mazingira sahihi ya kusema jambo unaweza kufubaza uzito wa ujumbe wako. Thamani ya unachokisema inabebwa pia na namna unavyochagua kukisema.

 

Fikiria mazingira ambayo mke anatamani mumewe afahamu mahitaji yake fulani fulani lakini hawezi kusema waziwazi. Saa nyingine sijui ni namna tulivyolelewa? Huenda. Kueleza hisia zetu waziwazi kwa wazazi wetu kulituingiza matatizoni. Tukajifunza kumbe usalama ni kuwaachia wengine kazi ya kujua tunachokihitaji. Ukubwani matokeo yake ndio haya sasa. Mke anamlaumu mumewe kimya kimya kwa kutokufanya kitu ambacho hata hivyo hakumwambia. Kwa nini mke hasemi anachokitaka? Anaamini, “Sitakiwi kujieleza. Mwanaume anayenipenda lazima ajue mahitaji yangu bila kumwambia!” Hatukufundishwa mawasiliano nyumbani.

 

Ukichunguza migororo mingi ya ndoa hukosi kuona namna inavyochipukia kwenye mzizi mnene wa uwezo hafifu wa wapenzi wawili kuwasiliana. Hatujui sayansi ya mawasiliano katika ngazi zake mbili. Kwanza, ni namna ya kufikisha ujumbe kwa anayekusudiwa. Hili ni gumu kweli. Ugumu wake ni hofu ya uwezekano wa kumwuumiza mlengwa. Mifano unayo. Sivyo? Una kitu unataka kusema lakini unaogopa matokeo yake. Unaogopa namna kitakavyopokelewa. Mazingira magumu kweli. Kama ulilelewa kujali hisia za wengine unaamua bora kunyamaza. Lakini kadri unavyoshindwa kuusemea moyo ndivyo unavyozidi kuwa mpweke na kulimbikiza matatizo yasiyotatuliwa.

 

Lakini pia wapo wanaojali ujumbe kuliko anayeupokea ujumbe husika. Hawajali utajisikiaje. Ukitema ukimeza shauri yako. Muhimu kwake kasema. Ujumbe unakuumiza hajali. Kwa nini inakuwa hivi? Tunarudi kule kule. Malezi. Mtu aliyelelewa kwenye mazingira yasiyojali hisia zake, huwa hapati shida kuumiza hisia za mtu. Nafsi nyingi zimeumizwa kwa tabia hii ya kutokujali hisia za anayeupokea ujumbe huo. Hiyo ndio ngazi ya kwanza ya mawasiliano.

 

Ngazi ya pili inamhusu anayefikishiwa ujumbe. Mwenzako akikuambia jambo unalichukuliaje? Sasa hapa pia kuna mengi. Mwingine utamwambia jambo na ataishia kulidogosha, kulipuuza, au basi tu kukuhukumu. Bila shaka una uzoefu na kauli kama hizi, “Usijisikie vibaya bwana. Usiogope bwana. Hili jambo dogo sana!” Mtu unajiuliza, “Mwenzio tayari najisikia vibaya. Unaposema nisijisikie vibaya una maana gani?” Kumbe badala ya kumwelekeza mwenzio namna ya kujisikia, ungeanza na kuelewa hisia zake pengine ungemsaidia.

 

Hapa pia hatukwepi athari za malezi. Wengine wetu tumelelewa kuamini kwamba hasira, hofu, wasiwasi, hatia hizi ni hisia mbaya na hivyo hatutakiwi kuwa nazo. Tulikemewa na kuchapwa kwa kuonesha hisia hizi. Ukubwani tunajipa kazi ya kuhakiki hisia za watu badala ya kujitahidi kuzielewa. Mzizi mwingine wa migogoro.

 

Mke, mathalani, anajisikia mpweke mume wake anapokuwa nje usiku. Kusema hisia zake kunatafsiriwa kama kulalamika. “Kwa nini ujisikie mpweke na unajua ninachokifanya ni kwa faida yako?” Kuambiwa hivi, mke naye ananyong’onyea, “Najisikia upweke kweli. Kwa nini hutaki kunielewa?” Mume anafura, “Nikuelewe nini? Kwani hujui ninachofanya huku niliko?”

 

Haya mazoea ya kuwanyima watu kusema vile wanavyojisikia ni sehemu ya tatizo katika mahusiano. Badala ya kuzipokea hisia za mtu vile zilivyo, tunakuwa wepesi kuzichambua na kuonesha kuwa hazina mashiko. Tunapofanya hivi, saa nyingine bila kujua, yule mwenye hisia hizo anajisikia kutokueleweka. Unapojisikia kutokueleweka, mara ya kwanza, mara ya pili, mara ya tatu, unaanza kusita kusema hisia zako. Unagundua kumbe hata ukisema ni kazi bure. Kusema ni kujisumbua na utaishia kuzodolewa. Ufumbuzi ni kujijengea handaki lako. Unatulia.

 

Mazingira haya ya watu kuamua kutulia hutengeneza utulivu usio na amani. Watu hawagombani lakini mioyo yao imevurugika. Hawawezi kuongea, hawawezi kuusemea moyo, kwa sababu jaribio lolote la kuzungumza litawasha moto. Nani anataka moto? Bora kunyamaza. Mkifikia hapo, sasa sisi washunuzi letu kwenu huwa ni neno moja tu. Tafuteni msaada wa namna ya kuwasiliana kwa utulivu.


Niandikie: bwaya@learninginspire.co.tz


Maoni

  1. win9999 คาสิโนออนไลน์ โด่งดังที่ได้รับการยินยอมรับและก็โด่งดังเป็นเว็บไซต์ pg slot ที่ไม่ผ่านเอเย่นต์ มีระบบระเบียบการดูแลรักษาความปลอดภัยและก็ระบบการทำงานอย่างมือโปรของเรา

    JibuFuta
  2. ทาง เข้า pg soft ออนไลน์ สำรวจโลกของความบันเทิงออนไลน์ที่น่าตื่นเต้นกับ เปิดเผยเกมแพลตฟอร์มนี้อย่างละเอียดและเป็นเอกลักษณ์ PG ค้นพบแนวทางที่ครอบคลุมทุกสิ่งที่คุณต้องรู้เกี่ยวกับเว็บไซต์

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Tumia Mbinu Hizi Kuelewa Unachokisoma -3

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia

Haiba ni nini?