Tumeiachia teknolojia itulelee watoto wetu?

 

Picha: reviewed.com

Jijini Dodoma. Jioni ya Jumatano. Kikombe cha kahawa kinanikutanisha na maswahiba Gwamaka na Dk Mugisha. Tumezungumza mengi. Kisha mada inabadili uelekeo, “Unajua nikiangalia namna hawa wadogo zetu wanavyoyachukulia mahusiano sipati picha itakuwaje kwa watoto wetu.” Mada mpya ya malezi inachukua nafasi yake. Dk Mugisha anakiita kizazi hiki generation X, kumaanisha kizazi kilichozaliwa kwenye teknolojia.


Kawaida, kila kizazi huona kilikuwa afadhali kuliko kizazi kinachofuata. Hata wazazi wetu, kimsingi, walikuwa na wasiwasi na sisi. Lakini ni ukweli pia kuwa mabadiliko makubwa ya kiteknolojia tunayoyashuhudia hivi sasa yamebadili kabisa namna tunavyoishi na kuchukulia mambo.


Gwamaka anaona huu urahisishwaji wa kupata taarifa umeunda tatizo jipya tunalohitaji kulitazamwa. “Teknolojia imerahisisha mno watu kuyatangaza maisha yao mitandaoni. Tunajilinganisha mno na kuyatazama maisha kwa mizania ya vitu. Hili linaweza kuwasumbua sana vijana wanaochipukia hivi sasa.”


Tafiti zinasemaje? Upo uhusiano mkubwa kati ya utumiaji wa mitandao na ongezeko la maradhi ya sonona. Mitandao ya kijamii, mathalani, inaongeza uwezekano wa watu kujilinganisha na watu ambao, wakati mwingine, hawawafahamu. Maendeleo haya yanatengeneza changamoto mpya kama anavyoeleza Gwamaka,

“Nafasi ya mzazi kuwa mtu pekee anayesikika zaidi mwanzoni mwa maisha ya mtoto imeanza kupotea. Mtoto anakutana mapema na watu wengi maarufu wanaomvutia na kuathiri mitazamo yake kuliko hata mzazi wake.”


Hoja nzito hiyo inamfanya Dk Mugisha aweke kikombe cha kahawa mezani. Kakumbuka jambo. “Juzi nilitaka kujua katuni zinawafundisha nini watoto wangu. Nikawadadisi. Hutaamini. Ule uwezo wa kuwachambua wale characters (wahusika) wa katuni ulinishangaza. Watoto walielezea characters wanaowapenda na wasiowapenda na wakatoa sababu.”


Siku hizi si ajabu watoto wa miaka miwili kulilia simu za wazazi wao. Kwa vile saa nyingine tunaepuka ule ‘usumbufu’ wa kushiriki shughuli zao hatusiti kuwapa.  Gwamaka, kwa upande wake, anaona ni muhimu kuanza kudhibiti taarifa zinazomfikia mtoto mapema akiwa bado mtoto. “Nimeweka televisheni nyumbani mwaka jana. Muda mrefu hawakuwa na cha kuangalia.” Tunacheka kwa mshangao kidogo. 

Kwa siku za leo, familia za mijini kutokuwa na luninga si jambo linaloweza kueleweka. Kwa nini Gwamaka alifikia uamuzi huo? “Najijua. Sina huo muda wa kujua chaneli gani inawafaa watoto. Nikaona bora isiwepo. Huwa natamani tungekuwa na chaneli halal zinazowafaa watoto. Tungekuwa na watu wanaofanya kazi ya kuhakiki na kukusanya vipindi vinavyowafaa watoto ili hata usipokuwepo nyumbani unakuwa na uhakika watoto wanaangalia vitu sahihi.”


Utoto ndio msingi wa tabia nyingi za ukubwani. Kuna vitu vikishaingia kwenye ufahamu wa mtoto inawezekana ikawa kazi ngumu kuvitoa baadae. Mtoto hujifunza zaidi kwa kuiga kuliko mafundisho ya maneno. Kwa msingi huo teknolojia inaweza kuwa nyenzo ya kuwarahisishia watoto kuiga uangamifu wao.


Dk Mugisha, kwa upande wake, anafikiri ni muhimu mtoto kujifunza mapema kuchagua kilicho sahihi. “Kwangu watoto wana uhuru. Ninavyoona muhimu zaidi si kuwanyima taarifa bali kukuza uwezo wao wa kuchambua maudhui wanayokutana nayo. Kwa nyakati zetu mtoto asipopata ujuzi huu nyumbani akienda shule atapata tabu.”


Siku hizi mtoto wa miaka mitatu tayari kavaa sare za shule na ana begi mgongoni. Mengi anayokutana nayo kule yana nguvu ya kufuta chochote cha maana alichojifunza nyumbani. Sijui kama wazazi wengi wanapofikiri mtoto aende shule gani huwa wanatazama zaidi ya matokeo ya mitihani.


Gwamaka na mke wake walifanya maamuzi magumu, “Unajua utoto ni umri wa kutengeneza operating system (mfumo wa kufikiri).  Mtoto anasoma shule gani hili sio jambo la kuchukuliwa kirahisi. Sisi tunatofautiana na wazazi wengi wa kisasa. Tuliamua malezi yawe kazi rasmi kwa mke wangu. Ilibidi yeye abaki nyumbani tuwe na uhakika mmoja wetu yupo nyumbani kufuatilia kwa karibu ukuaji wa watoto.”


Dk Mugisha anakuna kichwa. Haamini anachosikia. Mke wa Gwamaka kasoma. Katunukiwa Shahada yake Mlimani. Kwa nini waliamua abaki nyumbani? “Kwetu malezi sio kazi ya kumwachia dada wa kazi. Ofisi ya mke wangu tuliamua iwe nyumbani. Shughuli zake haziwanyimi watoto haki ya kuwa na mtu wa kumwiga.” Katika nyakati hizi za usawa wa kijinsi(a) hili la mmoja kubaki nyumbani si jambo jepesi kufanyika. Tutaanzia hapa Jumapili.


Niandikie: bwaya@learninginspire.co.tz

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia