Urembo kikwetu, unakuwaje hasa?

Nilipodokeza kuhusu suala la mahangaiko ya akina mama na nywele, msomaji mmoja aliniandikia: " Mwanamke gani utaoa mwenye asili kamili ya uafrika?...". Nilimjibu.

Katika kumjibu lilinijia swali kubwa: hivi mwanamke mrembo hasa ni yupi? Mrembo/mzuri kwa macho ya kiafrika yukoje?

Ukisikiliza maoni ya wanaume wengi utaona namna ambavyo tumeathirika kufikiri kwetu. Utaona namna tusivyoipenda aisli yetu hata kama tunadai kuupenda uafrika kwa maneno yetu.

Kwa wengi, mwanamke mrembo ni lazima awe mweupe kadiri iwezekanavyo. Awe mweupe peee hata kama ni kwa kulazimisha. Ndio maana kwa baadhi ya makabila mwanamke mweupe hulipiwa mahari kubwa zaidi ya mweusi.

Mwanamke mrembo ni lazima awe mwembamba iwezekanavyo. Ndio maana wengine wanajikondesha sio kwa sababu wanaelewa umuhimu wa kupunguza mafuta mwilini, la hsha. Ni kwa sababu wanadhani ili wavutie ni lazima wakondeane.

Kwa lugha rahisi mwanamke mrembo, ionekanavyo, ni yule awezaye kujipamba kwa kila kiwezekanachoo alimradi aonekane kimagharibi magharibi. Hapo weka lipstiki, mawigi, poda, mihereni, jichorechore macho, nyoa nyusi na kadhalika.

Na ukiangalia kwa jicho kavu, hukosi kubaini kuwa sifa zote hizo zinazotajwa zinalenga kumfanya mwanamke wa kiafrika ajione duni. Aisusie asili yake inayomtambulisha barabara kwamba yeye ni mwafrika. Kumtaka mwanamke wa kiafrika asiyefanya marekebisho yoyote ya msingi, kuhusu mwili wake, ajione kwamba hajawa mrembo bado.

Huku, ndugu zangu, ni kujikataa. Na mawazo kama haya, ni hatua ya mwisho kabisa ambayo mwanadamu anaweza kufikia katika kujionea kinyaa yeye mwenyewe. Hata kama unapinga, lakini ndivyo ilivyo. Nukta.

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia