Hisia Zilizojeruhiwa Zinavyoweza Kujenga Ukatili Usiotarajiwa

PICHA: Pride News Magazine



Baraka amekuwa akilalamikiwa kwa tabia yake ya udokozi tangu akiwa darasa la tatu. Ingawa alikuwa mdogo kwa umbo, jina lake maarufu lilikuwa ‘Baraka kibaka.’ Mbali ya kuwa kibaka, baraka alikuwa mgomvi aliyepambana na karibu kila mwanafunzi shuleni.

Akiwa darasa la sita, Baraka alisimamishwa shule kwa kosa la kumshambulia na kumwuumiza mwanafunzi wenzake. Baadae, Baraka aligundua kuwa aliyesababisha afukuzwa ni mwalimu wa Hesabu aliyepeleka taarifa za tukio hilo kwenye uongozi wa shule. Mara moja Baraka alimfuata mwalimu huyo ofisini na kumpiga makonde. Lilikuwa ni tukio baya la mwanafunzi kumdhalilisha mwalimu ambaye si tu anamfundisha, lakini pia ana umri wa mzazi wake.

Nilimfahamu Baraka kama jirani yangu. Maisha yake ya nyumbani yalitawaliwa na ghasia tupu. Mbali na kuwa mgomvi kwa karibu kila mtu, Baraka alikuwa na uwezo wa kujibizana na wazazi wake na hata ikibidi kukabiliana nao pale walipotaka kumuadhibu. Ilikuwa kawaida kumsikia Baraka akipiga mayowe saa za jioni. Wakati mwingine yalikuwa ni majibizano makali ya maneno kati yake na kaka zake, baba au mama.

Nakumbuka si mara moja Baraka alijikuta akilala barazani akiwa amefungwa mikono na miguu kwa kamba. Ilikuwa ni adhabu kali yenye udhalilishaji mkubwa kwa mtoto mwenye umri mdogo kama Baraka. Ingawa wazazi wake walifikiri wanatumia njia sahihi kumrekebisha, ni dhahiri walijeruhi moyo wake kuliko kumsaidia. Kadri walivyomdhalilisha, ndivyo Baraka alivyozidi kuwa ‘gaidi.’

Majuzi nilisikia Baraka amekuwa kilema. Jicho lake moja limeng’olewa, hana mkono moja, usoo umejawa makovu shauri ya vipigo vya ‘wananchi wenye hasira kali.’ Baraka anadaiwa kuwa jambazi sugu, anayetishia usalama wa watu.  Kwa miaka mingi, Baraka anadaiwa kushiriki matukio mengi ya kihalifu ikiwa ni pamoja na ubakaji, unyang’anyi wa kutumia mabavu na matumizi makubwa ya madawa ya kulevya.

Kwa haraka haraka tunaweza kumbebesha lawama zote Baraka. Tunaweza kusema yeye ndiye aliyechagua maisha ya ukatili na kutokuwa na huruma na watu. Lakini uwezekano ni mkubwa kuwa ukatili wa Baraka umetengenezwa na mazingira ya malezi yasiyojali hisia zake.

Tafiti zinaonesha kuwa majambazi wengi na watu waliowahi kufanya matukio ya kikatili, walizaliwa na wazazi wakali, wenye kutumia mabavu na wasiojali hisia za watoto hao. Wengine wao huwa na historia ya utoto wenye maumivu makubwa ya kihisia. Aidha, baadhi yao huwa hawajawahi kuelewa maana ya upendo wa wazazi kwa sababu ya kuwa watoto wanaoitwa ‘wa mitaani’.

Ukweli ni kwamba hakuna binadamu anayependa kudhalilishwa. Kila mtu tangu akiwa mdogo anatamani kuishi na watu wanaomwelewa na kujali hisia zake. Inapotokea mtu anakuwa katika mazingira yanayomwuumiza kihisia na watu aliotegemea wangemjali, hali hiyo hujenga kisasi ndani yao kama ilivyokuwa kwa Baraka.

Ukorofi wa mtoto mara nyingi ni ujumbe. Ni muhimu wazazi kuuelewa ujumbe huu kabla hawajafanya maamuzi ya aina gani ya adhabu waitoe. Ukorofi, mathalani, ni lugha ya mtoto kusema ndani yake anajisikia utupu. Hisia zake hazijapata mtu wa kuzisikiliza. Anapofanya ukorofi wake, kimsingi anatuambia kwamba sisi tunaomzunguka hatujatambua hisia zake. Ndani yake mna sauti inayomwaminisha kuwa hatambuliki. Imani hiyo potofu huchochea jitihada za kutafuta kutambulika kwa namna isiyokubalika.

Ugomvi, udokozi na ghasia nyingine anazofanya –wakati mwingine bila hata yeye kung’amua anachokifanya– ni namna ya kujirudishia mamlaka anayoamini hana. Anapobishana na mzazi, anapogombana na wenzake, kama alivyofanya Baraka, kimsingi anajaribu kujiliwaza kuwa na yeye bado anauwezo wa kupambana kama wengine.

Mtoto wa namna hii, kama ilivyokuwa Baraka, huishia kuwa na hisia zilizokufa hali inayoweza kumfanya awe tayari kufanya chochote bila kujali maumivu anayoyasababisha kwa wengine. Bahati mbaya, kadri anavyowaumiza wengine, ndivyo anavyojisikia unafuu ndani yake kwamba na wengine nao wanaumia kama anavyoumia yeye.

Matukio ya ukatili yanayoendelea kwenye jamii yetu, yanaweza kuwa na mzizi kwenye aina ya malezi tunayowapa watoto wetu. Matumizi ya mabavu kupita kiasi, adhabu kubwa zinazoumiza mno hisia za watoto, zinaweza kuwa mbegu mbaya itakayozalisha watu wasiojali hisia za wengine, watu watakaokuwa tayari kuumiza wengine na hata ikibidi, kuwatoa roho ili tu kuridhisha nafsi zao kwamba nao wana uwezo wa kufanya matendo ya ‘kishujaa’ yatakayowanyoosha wengine.

Tunahitaji kutambua kwamba watoto, bila kujali makosa yao, wanaelewa vizuri zaidi lugha ya upendo inayojali hisia zao kuliko adhabu kubwa tunazowapa. Tukijenga mazoea ya kuumiza hisia za mtoto, tunatengeneza kizazi cha watu watakaofurahia kuwaumiza watu wengine wakiamini kufanya hivyo ni ushujaa.


Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia