Kipimo cha Kujitambua ni Tunavyowatendea Tusiowajua, Wasioheshimika

Mjema anaandika ripoti inayohitajiwa na mkuu wake wa kazi. Wakati muda wa kukabidhi ripoti hiyo ukikaribia, anapigiwa simu na mtu asiyemfahamu. Mjema hajui ni nani hasa anayemtafuta muda huo hivyo anaamua kupokea simu. Bahati mbaya aliyempigia simu hasikiki vyema. Mjema anahisi labda ni tatizo la mtandao, anaamua kuikata mara moja.

Baada ya dakika moja, namba ile ile inampigia tena. Mjema anapokea simu. Kwa mara nyingine anayeongea upande wa pili wa simu hasikiki vyema. Mjema anajisikia kusumbuliwa na anakasirika. Anakata simu kwa hasira. Mara ya tatu, namba ile ile inaita tena. Mjema anaudhika na kupandwa na hasira. Mara hii, anaipokea kwa hasira na kuporomosha matusi ya nguoni mfululizo na kukata simu mara moja.

Baada ya dakika tatu, Mjema anapokea ujumbe mfupi wa maandishi kutoka namba hiyo hiyo. Mara hii mhusika anajitambulisha na kuomba msamaha kwa kumsumbua na kukata simu. Mjema anagundua kumbe aliyekuwa anamsumbua muda wote huo alikuwa ni Mkurugenzi wa kitengo anachofanyia kazi. Mjema anachanganyikiwa na kuhaha asijue la kufanya. Huku akijutia kitendo cha kumtukana mkuu wake wa kazi (bila kujua), anaamua kupiga simu haraka kuomba msamaha kwa kitendo chake hicho.

Kwa nini Mjema anasikitika kumtukana mkuu wake wa kazi bila kujua? Je, kama Mjema angegundua kuwa huyo aliyemtukana bila kujua alikuwa ni mtu asiye na hadhi yoyote katika jamii na asiyeweza kuathiri maisha yake kwa namna yoyote, angesikitika kwa kiwango hicho hicho? Kwa nini?

Kulazimika kuwa vile tusivyo?

Tukio kama hili hutukuta wengi wetu katika maisha yetu ya kila siku. Tunapokuwa na watu tunaowaheshimu, kama wazazi wetu, wapenzi wetu, viongozi wa dini, wakuu wa kazi, tunajiweka katika sura inayoheshimika. Tunafanya jitihada za kuonekana wanyenyekevu ili kupata heshima yao. Tunaogopa kudharauliwa na watu hao na hivyo tunajitahidi kujiweka katika hali wanazozitarajia kwetu.

Wakati mwingine tunafanya kinyume. Tunapokuwa na watu tunaodhani ni wa hadhi ya chini, wasioheshimika, hatuoneshi heshima. Kwa mfano, tunapoongea na wahudumu wa migahawa ya chakula ni rahisi kuonesha dharau ambazo kwa hakika tusingethubutu kuzionesha kwa watu tunaowaheshimu. Tunafanya hivyo kwa sababu tunajua hata wanapojisikia vibaya, hatupati hasara yoyote.

Kadhalika, tunapokwenda mahali tunapojua hatufahamiki tunabadili tabia zetu. Tunageuka kuwa watu wengine kabisa kiasi kwamba kama angetokea anayetufahamu angeshangaa. Kubadilika huku kwa ghafla ni kujaribu kuwa vile tulivyo katika uhalisia wetu kwa sababu kufahamika hutufanya tulazimike kuwa tusivyo.

Kujenga taswira inayotarajiwa?

Kuna ukweli kuwa mwanadamu anayo kawaida ya kujenga taswira anayojua wengine wanaitarajia kwake. Tunaweza kuwa na sura fulani tuwapo wenyewe lakini tunapokuwa katikati ya wengine tunavaa sura nyingine na kufanya vinginevyo. Uwepo wa watu wengine hutulazimisha kubadili tabia zetu ili kukidhi matarajio ya watu hao.

Marafiki hujua kujenga taswira zinazotarajiwa. PICHA: HONGQI ZHANG
Wakati mwingine tunavuka mipaka na kujikuta tunaigiza tabia zisizo halisi ili kuzidi uhalisia wetu. Tunalazimika kujibadilisha badilisha kama kinyonga kama jitihada za kutengeneza hadhi bandia tunazozihitaji kwa wengine.


Hadhi, hata hivyo, si jambo baya wakati wote. Kujenga taswira chanya kwa wengine hutusaidia kujua namna bora ya kuenenda mbele za watu. 

Mathalani, ni kawaida tunapojiandaa kwenda kukutana na watu wengine tunajitazama kwenye kioo kuhakikisha tunaonekana vyema. Tunakuwa makini kuhakikisha tunakuwa na taswira chanya hata ikibidi kwa kufikiria  namna gani tutatabasamu, tutakavyokaa na hata ikibidi badili kidogo mwonekano wa nywele, tunavyoa ndevu na kadhalika. Hizo zote ni jitihada za kujenga taswira inayotarajiwa na wengine.

Aidha, tunajitahidi kuvaa mavazi ya kupendeza kwa lengo la kukidhi hadhi tunazotaka kuwa nazo katika jamii. Tunavaa tai, makoti, nguo za rangi na mitindo mbalimbali kuongeza kukubalika kwetu, jambo ambalo, kwa hakika, si baya linapofanyika kwa nia njema. Ndio kusema kuyasoma mazingira ya kijamii yanataka nini ili tutende yapasayo ni sehemu ya busara ya kawaida ya kibinadamu.

Ulaghai wa taswira chanya?

Lakini kwa upande mwingine, kudhibiti namna watu wanavyotuona kama mbinu ya kuwafanya waone uzuri tusiokuwanao yaweza kuwa tatizo. Kwa mfano, kuongea kwa staha na mtu tunayemheshimu haiwezi kuchukuliwa kuwa ni tabia yetu halisi ikiwa tunaweza kuonesha dharau kwa mtu tunayemwona kama asiyestahili heshima. Kuonesha staha kwa tunayemheshimu inaweza kuchukuliwa kuwa mbinu tu ya kuipata heshima yake.

Wakati mwingine tunaweza kushangaa iweje, kwa mfano, binti anayeongea kwa adabu na nidhamu ya hali ya juu kwa kijana aliyeonesha nia ya kumchumbia akawa na dharau zilizopitiliza kwa wahudumu wa mgahawa wa chakula. Ukweli ni kwamba tabia halisi ya binti huyu ni dharau kwa sababu kwa mhudumu wa mgahawa halazimiki kujenga taswira fulani. Hivyo anapozungumza na mhudumu huyu huo ndio unakuwa uhalisia wake. Nidhamu anayoionesha kwa kijana yule mwenye matazamio fulani kwake ni mbinu tu ya kujenga hadhi  inatakayomwezesha kukubalika.

Tabia zinazokubalika huanzia ndani

Tunaweza kusema kubadilika badilika kwa lengo la kuendana na mazingira ya kimahusiano yaweza kuwa dalili ya kutokujikubali na hata kutokujitambua. Mtu anayejielewa na kujikubali halazimiki kubadilika kilaghai kukidhi matarajio yasiyokuwepo. Kwa lugha nyingine, tabia zake njema huanzia ndani na kujidhihirisha nje kwa namna ile ile kwa watu wote bila kujali mazingira ya kimahusiano.


Ili kupima tabia zetu halisi na kujitambua kwetu, ni muhimu kuangalia tunavyowatendea watu wasioheshimika; tunavyoongea na watu tusiowafahamu; tunavyowajibu makondakta wa daladala; tunavyowasemesha wahudumu wa mikahawa. Tukitaka kujua tabia ya mtu, pa kuanzia ni kuangalia anavyowatendea watu wa chini yake na wasiomsaidia. Kwa sababu kujitambua ni kuelewa binadamu wote wanastahili heshima yetu ya dhati bila kujali nafasi na hadhi walizonazo. Unakubaliana na hitimisho hili? Udhani inawezekana? 


Kwa mijadala zaidi fuatilia safu ya Saikolojia katika gazeti la Mtanzania kila Alhamisi.


Barua pepe: bwaya@mwecau.ac.tz

Maoni

  1. Ndg Bwaya, kwanza nikupongeze kwa makala nzuri, bila shaka wengi watajifunza kupitia makala hii kama nilivyojifunza mimi.

    Binafsi nina maoni ya ziada juu ya badiliko la tabia kwa watu mbali mbali kulingana na mazingira. Tabia tofauti kwa watu (mazingira) tofauti yaweza kusababishwa na mambo mengi. Jambo la kwanza ni kama ulivyolieleza kwa kina katika makala hii.

    Jambo la pili ni kuwa inategemea na mahusiano baina ya muonyesha tabia na muonyeshwa tabia. Mfano, kama tumezoea kutaniana, basi kila tunapokutana tabia ya kutaniana haiwi mbali. Habari Njema ni kwamba, wawili hao kwa muda wote watakaokuwa pamoja wanajua ni wapi walitania na ni wapi walimaanisha walichokifanya ama kusema.

    Lakini kama mahusiano yetu hayako katika mazingira ya kutaniana, utategemea mawasiliano ya mwelekeo huo. Hii ni kusema kwamba, mara nyingine tunaweza kutoa hukumu isiostahili juu ya tabia za watu kama "hukumu" yetu haikuzingatia muktadha wa mawasiliano yao.

    Maranya O'Mayengo

    JibuFuta
  2. Ndugu Maranya, asante sana kwa maoni yako makini. Naamini wasomaji wa blogu hii watajifunza kwa uliyoyaandika pia.

    Ni kweli kama unavyosema, hukumu ya kwa nini tunatenda tuyafanyayo inategemea sana na namna mwonesha tabia anavyohusiana na mwoneshwa. Msingi wa hoja ya makala haya ni kwamba tabia halisi ni zile tunazozionesha kwa wale tusiowachukulia kwa uzito katika maisha yetu na hivyo hatulazimiki kujenga taswira chanya kwao.

    Nadhani utani wa kirafiki ni suala tofauti kidogo na linahitaji mjadala unaojitegemea. Hata hivyo, ni kweli kwamba huwa hatutaniani na kila mtu. Na tunapotaniana mara nyingi malengo yetu huwa si kujenga taswira fulani chanya kwa tunayetaniana naye. Kwa hiyo, ni vigumu maudhui ya makala haya kujibu suala hili ipasavyo.

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia