Tabia zetu zimekosewa

Juma lililopita tulijaribu kuona athari za malezi katika ujenzi wa tabia zetu. Tuliona namna ambavyo matendo yanayofanywa na wazazi wetu kwa kujua kwao ama kutokujua kwao, yanatusababisha tuwe hivi tulivyo. Tukasema kuwa tulivyo, ni matokeo ya walivyo/walivyokuwa wazazi wazazi wetu.
Leo ningependa tuangalie ukweli mmoja kuwa asilimia kubwa ya watu unaowaona barabarani, unaofanya nao kazi, unaosoma nao na pengine wewe mwenyewe, wamekosewa. Kukosewa ninakokuzungumzia hapa ni katika ujenzi wa tabia ama haiba yetu. Sina neno zuri kushika nafasi ya “Personality”. (Pengine Mwalimu wangu Makene atanisaidia)
Kila binadamu anayo haiba/tabia yake—yaani namna anavyofikiri, anavyojisikia, anavyofanya mambo yake, anavyovaa, anavyoonekana na vilevile anavyohusiana na watu wanaomzunguka.
Makosa ya tabia zetu yanahusisha matendo ambayo yanakinzana na iliyokawaida ya utamaduni wetu na matarajio ya wanaotuzunguka. Hata hivyo si kila afanye kivyume na matarajio ya watu ana kilema cha tabia. Na wala haiwezi kuwa kweli tukiamini kwamba kila anayefanya yaliyo matarajio ya jamii yake kuwa hawana tatizo hili. Tunalenga hasa katika zile tabia zinazoonekana zaidi na watu. Mathalani, watu wengi wanatarajia kuwa mtu ajiamini lakini asiwe na kiburi wala majigambo. Awe na msimamo lakini pia asikilize na wengine wanasemaje. Awe mpole na sio zuzu na kadhalika.
AINA ZA VILEMA VYA TABIA
Ukisoma vitabu vya Elimu-nafsi (Kama kile cha Diagnostic and Statistical Manual of Mental Disorders Toleo la IV) utakutana na aina nyingi za vilema vya tabia. Hapa tutajadili kwa uchache:
1. Kilema cha kukushindwana na watu
Watu wenye kilema hiki kufanya mambo bila kuangalia hisia na haki za watu wengine. Watu hawa huvunja sheria, huweza kuwatumia watu wengine kwa faida zao wenyewe. Ni waongo, wakali na mara nyingi hupigana pigana bila sababu ya msingi. Ndio hawa wanaogombana na wapenzi wao mara nyingi, hudharau na kuwatendea jeuri watoto wao, wakiwa ni mabosi basi watataka kuwanyonya watumishi wao kupindukia. Huweza hata kujikuta wakiwatoa uhai watu wanaowaudhi.
Watu wenye tatizo hili huwa hawajijui kuwa wana kilema kwa sababu huwa hawajisikii tena kuhukumiwa na nafsi zao wala kuona aibu wanapokosea. Ujue ndugu msomaji, ingawa kujisikia hatia ama kuona hata aibu ni hisia tusizozipenda, lakini ni za msingi sana katika maisha ya kawaida unapoishi katikati ya watu.
Watu wenye kilema hiki mara nyingi hujikuta wakifa mapema sana ama kuuawa au kujeruhiwa, wakiishia jela, wakifukuzwa kazi, au hata mara nyingine huwa walevi wa pombe au “lile jani” na vilevile hujikuta katika migogoro endelevu katika masuala ya mahusiano.
2. Kilema cha kujitenga na watu
Watu wenye kilema hiki, hujihisi- hisi wanapohusiana na watu wengine. Mara nyingi hufanya jitihada sana kujiondoa dhana fulani fulani vichwani mwao ambazo mara nyingi zaweza kuwa hazipo. Hawa jamaa huyachukulia mambo madogo kwa mtizamo wa tofauti na kuweza kusababisha varangati. Huweza kuwa na hasira na wala usigundue, kwa hiyo kuweza kudhihirisha hasira hizo kwa kujining’iniza ama kujiumiza. Husemekana kuwa wenye shida hii huwa hawana ile hali ya kujiamini na kujikubali (self-concept and self-esteem).
Wakiwa wadogo, watu wa jinsi hii, walikuwa watoto waoga wasiojiamini, wenye uchungu na ghadhabu,ingawa inawezekana waliionesha onesha enzi zao za shule na kujiundia umaarufu katika masuala kadhaa. Ingawa watu hawa huweza huweza kuwa wachangamfu na wenye kufurahisha kuwa nao, lakini bado uhusiano wao hauaminiki sababu unaweza kulipuka ghafla kama bomu la Mpalestina.
Watu hawa ambao asilimia kubwa huwa ni wanawake, huwa katika uwezekano wa kuwa na matatizo ya msongo wa mawazo, walevi, na kujiua kabla ya umri wa miaka 30. Hawa jamaa ni wagumu sana kutibu kwa njia za ushauri nasaha wa kitabibu (psychotherapy) kwa sababu hujenga uhusiano usioaminika na wataalamu wa tiba hizi za kisaikolojia.
3. Kilema cha kukwepa watu
Walemavu hawa huwa na aibu sana. Hujihisi kuwa hawapendwi na kwamba kila anayewaona anawakosoa tu. Hugoma kujichanganya na wengine labda kama watahisi wanapendwa kwa namna moja ama nyingine. Hujihisi kuwa watu wasio na lolote la kusema wakijilinganisha na wengine.
4. Kilema cha utegemezi
Hawa hawajiamini hata chembe. Hawawezi kufanya kitu wala kuamua jambo bila msaada wa mtu kwa karibu. Husubiri washauriwe hata katika mambo ambayo hayana haja ya kushauriwa sana. Hutafuta kuhakikishiwa sana katika mambo ambayo yako wazi. Mfano, kama ni mwanamke basi atapiga simu kwa mpenzi wake mara mia akitaka kuhakikishiwa kuwa anapendwa. Halafu kama vile haitoshi, hukaa mkao wa tayari-tayari wakitafuta uhusiano mpya unaohitimisha ule uliopo. Ni watu wasiojisikia kuridhika na amambo yanavyowaendea.
5. Kilema cha kutafuta sifa (Histrionic)
Ni watu wanaofanya kila liwezekanalo waonekane. Hawajiamini na pengine wanaona hawana eneo lolote la kujidai isipokuwa kulazimisha sifa zisizo haki yao. Furaha yao ni pale wanapokuwa gumzo kwa mambo yanayoweza kuonekana ni ya kijinga. Kwa hivyo, huweza kufanya vituko mbele ya watu almuradi tu waonekane na wao. Huweza kuvaa namna ambayo itawavuta watu kuwaangalia wao. Ndio hawa ambao huweza hata kukoleza chumvi lafudhi zao kwa madoido basi tu ujue wamo. Hawa ni wapenda sifa lakini wasiojiamini.
6. Kilema cha majivuno (Narcissistic)
Hawa ni wale wanaojiona kuwa ni wa maana kuliko wengine. Wanatafuta kukubaliwa kulikopita kiasi kwa kuonyesha walivyo bora, wenye mafanikio kuliko wengine wote. Wanaamini wao ni watu maalumu, nadra kuwapata, ama wa juu kuliko wengine. Wanajiamini lakini wamepita kiasi. Hugeuka kero mara nyingi wanapokuwa na watu kwa sababu hawaishi kusema mazuri yao tu. Jinsi walivyosoma sana. Walivyotembea sana. Walivyomaarufu na kadhalika.
7. Kilema cha kuzidi kiasi (Obsessive-Compulsive)
Ni watu ambao wanapenda sana kuchimbua mambo kwa kina na mpangilio, kwa usahihi uliopindukia. Wenye kilema hiki huweza kutumia masaa mengi wakifanya kazi wanazoona ni za maana huku wakisahau kupata muda wa kupumzika na marafiki. Ni wagumu, “makompliketa” wenye mipangilio isiyoweza kutikiswa na yeyote, wakaidi na mara nyingi hawacheki-cheki, wanauwezo wa kutengeneza tabasamu bandia ukadhani wamependezwa na wewe kumbe wapi bwana. Obsessive. Watu wa tafakuri lakini mpangilio mbovu.
8. Kilema cha kutokuamini watu(Paranoid)
Hawa ni watu wa kushtukia wengine, hawawaamini watu wakidhani kuwa wengine wako kinyume nao na mara nyingi hutafuta sababu ya kuthibitisha madai yao hayo. Ni watu wa ugomvi na uadui, na hupambana kwa hasira pale wanapohisi kuna mtu kawasema vibaya ama kawashushua. Si wavumilivu kama utasema kinyume na wanavyofikiri wao. Kwa mfano, ukiingia kwenye blogu zao na ikatokea ukaacha maoni yanayokinzana na wanayofikiri, basi moja kwa moja hukuchukulia kama adui. Adui kama Nduli miaka ile. Kwao rafiki ni yule anayekubaliana na wanavyofikiri.
9. Kilema cha ukiwa (Schizoid)
Ni watu wasiotaka kuwa na mahusiano ya karibu na watu, aghalabu wale wa jinsia tofauti. Hupenda kuwa pekeyao na kujiona kama watu wasiotakikana na kutengwa na watu. Hata ukiwasifu hawakuelewi, kwa sababu hawathamini sifa. Ukiwakosoa unafanya kazi bure, kwa sababu hawahitaji mawazo yako kwa namna yoyote. Hawahitaji uhusiano wowote na watu.
10. Kilema cha utawala (Schizotypal)
Ni wale jamaa mafundi wa mawazo tofauti na watu wengine, wenye kuongea habari za “Utopia” ambao huweza kutumia silabi na sentensi kwa namna inayoshangaza. Schizotypal. Walemavu kwa sababu wanajiona kuwa wanayo miujiza ya kuwatawala wenzao kimawazo. Wanawaza namna ya kuwateka wengine katika falsafa zao. Lakini hawataki uhusiano wa karibu kwa sababu wanawahisi- hisi wanaowazunguka.
******************************************
Baada kuangalia aina hizo za ulemavu wa kitabia kwa ufupi, swali la kujiuliza: Nini sababu yake? Kwa haraka haraka, jibu ni malezi ya wazazi. Nakaribisha mawazo mbadala kabla ya kuanza kuchambua sababu ya kilema kimoja kimoja. Lengo la mada hizi ni kujaribu kubainisha nafasi ya malezi ya nyumbani na jinsi malezi hayo yanavyoathiri mustakabali wa binadamu yoyote bila utashi wake mwenyewe iwe kwa namna chanya ama hasi. Na baada ya hapo kujadili namna tunavyoweza kuuondoa ulemavu tulionao. Siku njema.

Maoni

  1. Karibu tena ulipotea kidogo.Hicho kilema cha utegemezi ni kibaya sana.Hata yaliyo katika uwezo wako unataka msaada.Hii ya utegemezi inaweza kuonekana kwa wasomi wetu?
    Wanategemea kila kitu wakati uwezo wakupambanua mambo tayari wanao

    JibuFuta
  2. Mada kali hiii Bwaya!Nitapita tena kuijadili!

    JibuFuta
  3. Nakubaliana na wewe Egidio. Kwamba wasomi wanaweza kuwa na kilema hiki. Utegemezi hata katika mambo ambayo wanayaweza. Swali linakuwa: Je, wanapenda kuwa hivyo, ama kuna kilichowafanya wawe hivyo walivyo bila utashi wao? Hilo ndilo lengo la mada hizi.

    Kitururu, karibu tubadilishane mawazo. Baada ya siasa, muziki, dini na mengineyo, si vibaya sasa tukizungumza elimu-nafsi.

    JibuFuta
  4. Naamini malezi ya mtoto yanamsaidia sana kuwa alivyo.Lakini pia naamini sio malezi tu mazingira pia yanamjenga mtoto.Mzazi yeyote hata awe anamiujiza kuna mpka atafikia ambapo hawezi tena kuyakabili makuzi ya mwanaye.Kwanza kila mtoto ni tofauti.Hivyo katika familia moja , malezi ya mtoto wa kwanza yanaweza yakawa hayamfai mtoto wa katikati au wamwisho.Pili kuna swala la ubinadamu.Binadamu hata uwe umebobea vipi ni vigumu kuwa nauhakika wa hatua uzichukuazo kwamba zina leta matunda asilimia mia moja. Mtoto akuaye na kucheza na watoto wajirani , kutazama katuni kwenye TV, kusimuliwa hadithi na bibi, nk yote yanaathiri mtazamowake wa dunia na nafasi yake katika dunia.Anaye chapwa chapwa na kugombezwa anaweza akakua asiwe muoga na wala kuhisi alionewa na wazazi kama akina Michael Jackson walivyodai.Anaweza akakua nakuchukulia kuwa zile fimbo ndio zilimfanya awe makini.Aliyeachwa akue kivyake na kudekezwa anaweza vilevile akakua nakuwa yule aliyekuwa muoga wa maisha.Lakini pia aliyedekezwa anaweza akawa ndio jasiri naaliyechapwa hata kutetea hoja yake anaogopa kutokana na trauma za utotonin.Hili swala ni gumu kweli!

    Lakini nachoamini ni kwamba wazazi wengi hawawachukulii kwa makini watoto wao na kuwajua ni staili gani ya kudili nao ilikupata the best of them.Wengi utasikia tu, unajua baba yao mkali kweli!Lakini kumbe ule ukali haufanyikazi ipaswayo kwa watoto wake. HIvi vilema naamini vitaendelea kujitokeza mpka binadamu watakapo toweka ulimwenguni.Kwa sababu kama mzazi huna uwezo wa kuyajua mazingira ya mtoto wako kwa asilimia mia.Kwanza haiwezekani kwa mtu yeyote kumjua mwingine kwa asilimia mia.Kuna kiasi tunakijua halafu tunakuwa comfortable.Kunamafanikio tunayajua amabyo yanatupeleka mpka pale kwenye comfort level halafu tunatulia.Mzazi wa baba yangu alikuwa anamlenga baba kuwa mchungaji au mwalimu.Kwani yeye kwa ujuaji wake aliona akiwa katika fani yeyote katika hizo mbili ndio kufanikiwa.Mzazi wangu yeye alikuwa ananilenga niwe daktari, kwani anaaminin kuwa ukiwa daktari haliharibiki jambo.
    Lakini je, hivi kwanini mafanikio yasiwe tu kuwa mtu ana furaha na amani maishani mwake?

    Wote tunajua haitatokea binadamu asiye kuwa na kilema chochote.Sasa je, ni muhimu kujaribu sana kupata binadamu anaye karibia u perfection wa malaika?

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Uislamu ulianza lini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia