Jinsi matarajio yetu yanavyoathiri mitazamo na tabia za wengine

ILIKUWA ni mwaka 1968 Rosenthal na Jacobson walipogundua namna matarajio ya walimu yanavyoweza kusabisha matokeo yasiyotarajiwa kwa wanafunzi wao. Watafiti hawa walikwenda kwenye shule moja na kupima uelewa wa wanafunzi kwa kutumia mtihani maalum maarufu kama IQ test. Walimu wa shule hiyo walishuhudia zoezi hilo.

Basi, baada ya kuwapima wanafunzi, bila kujali matokeo ya kipimo cha uelewa, waliwagawa wanafunzi katika makundi mawili. Kundi la kwanza lilikuwa la wanafunzi waliopachikwa jina la 'wanafunzi wakali' hata kama haikuwa kweli. Walimu wao walipewa habari hiyo, kwamba wanafunzi hawa wamepimwa na wameonekana ni wazuri sana kiakili na wangeweza kufanya vizuri sana baada ya muda mfupi hata kama hawakuwa wakifanya vizuri kwa sasa. Lengo lilikuwa ni kutengeneza na kupandisha matarajio ya walimu kwa wanafunzi hawa. Kwenye kundi la pili la wanafunzi lililokuwa na wanafunzi wenye uwezo kama wenzao wa kundi la kwanza,  walimu hawakuambiwa lolote kuhusu uelewa wa wanafunzi hao. Kwa hiyo hapakuwa na matarajio yoyote.

Katika makundi yote mawili, Rosenthal na Jacobson waliwachagua wanafunzi kwa njia ya nasibu (randomly), kwa maana ya kwamba kila mwanafunzi alikuwa na nafasi ya kuwa katika kundi lolote kati ya hayo mawili.

Miezi nane baadae, wanafunzi wote walipimwa uelewa kwa mara ya pili. Matokeo yake ni kwamba, wanafunzi wa kundi la kwanza, walionekana kweli kuwa na uelewa wa juu kuliko wenzao wa kundi la pili, ambao kwa bahati mbaya walimu hawakuwa na matarajio yoyote kwao. Maana ya matokeo haya ni kwamba, imani na matarajio ya walimu kwa wanafunzi wao, yalisababisha kutimia kwa matarajio hayo.

Miaka kadhaa baadae, watafiti wengine walifanya utafiti unaofanana na huo kwa kutumia mazingira tofauti. Wanaume kadhaa waligawanywa kwenye makundi mawili na 'kuunganishwa' na wanawake kwa njia ya simu. Kundi la kwanza, waliaminishwa kwamba wanakwenda kuongea na wanawake warembo na mwenye haiba nzuri. Kundi la pili la wanaume, waliaminishwa kwamba wangeongea na wanawake wenye sura mbaya na haiba isiyopendeza. Ukweli ni kwamba wanawake wote walikuwa wamepatikana kwa njia ya nasibu (randomly) na walikuwa na nafasi sawa ya kuwa ama warembo au 'wa kawaida'. Lengo lilikuwa kutengeneza matarajio kwa wanaume hao yatakayoathiri namna watakavyohusiana na wanawake hao. Kwa siri, watafiti hao walihakikisha kuwa wanarekodi mazungumzo ya wanaume wa makundi yote mawili kuona namna mawaliano yote yalivyokuwa yakifanyika.

Matokeo yalikuwa kama ifuatavyo: Katika kundi la kwanza la wanaume walioamini wanazungumza na wanawake warembo, ilionekana kwamba wanaume walizungumza kwa bashasha na mvuto, hali iliyotafsirika kama jitihada za kuwavutia wanawake hao warembo. Jamaa walijikuta wakiwa na mengi ya kusema na mazungumzo yalikuwa ya muda mrefu na ya mara wa mara. Na matokeo yake hata kwa upande wa wanawake, mwitikio ulikuwa chanya, na majibu yalikuwa ya bashasha hali kadhalika. Na hatimaye walipopimwa kiwango cha kujiamini baadae, wanawake hao walionekana kuwa na alama za juu, ikimaanisha kuwa marajio ya wanaume wale yalitengeneza uhalisia kwa wanawake husika.

Katika kundi la pili la wanaume walioamini wanazungumza na wanawake wenye sura mbaya, mazungumzo yalikuwa mazito na yasiyo na msisimko wowote. Kwa hakika ni kama hapakuwa na jitihada zozote za wanaume wale kujaribu kuwavutia wanawake 'zao' na matokeo yake, hata wanawake hawakusisimshwa na 'mahusiano' na wanaume wale. Baadae wanawake wale walipopimwa kiwango chao cha kujiamini kama wenzao wa kundi la kwanza, walionekana kufanya vibaya. Hawakuwa wanajiamini kumaanisha kuwa matarajio ya wanaume wale yalitengeneza uhalisia kwa wanawake husika.

Katika maisha yetu ya kila siku je?
Chukulia mfano umesikia kuwa Wahaya ni watu wanaojisikia, wenye majigambo na dharau. Au umeonana na Rweyemamu, Mhaya mmoja anayetokea kwa bahati mbaya kuwa 'anajisikia, mwenye majigambo na dharau'. Habari hiyo hukufanya ujenge sura ya jumla kwa Wahaya. Ukifanya hivyo, maana yake utawakusanya Wahaya wote kwenye kundi linalofanana na watu wenye kujisikia, majigambo na dharau. Na kwa kuwa akili yako haina muda wa kuruhusu tofauti ndogo ndogo za 'wanachama' wa kundi kuu la Wahaya, kila Mhaya kwako anafanana na sifa kamili ulizonazo kwenye kundi hili.

Siku ukikutana na Rwechungura, mara moja akili yako inafungua faili la Wahaya. Na faili lenyewe lina matarajio yanayokuambia unapaswa kutegemea nini kwa Wahaya. Matarajio hayo ya jumla, yatakufanya ama uhusiane na Rwechungura, kijana wa kawaida, mchangamfu na mwongeaji kwa namna ya tahadhari ya kusikia yaliyomo kwenye faili lao la Wahaya au, uwe makini kupembua kila kinachosemwa na Rwechungura kwa kukilinganisha na 'dondoo' ulizonazo za faili la Wahaya.

Matokeo yake, unaweza kujikuta ukianzisha mazungumzo yanayoweza kumfanya Rwechungura akuambie mafanikio yake kama ambavyo kijana yeyote angefanya na wewe unakuwa na kazi ya kukithibitisha matarajio yako kuwa Rwechungura ni kijana anayependa kujisifu. Au basi, unaweza kuwa makini sana kufuatilia mazungumzo yake kubaini 'majisifu' yake, na hivyo kuthibitisha ulichonacho kwenye faili lako, na ukasahau kabisa kuwa mtu yeyote angeweza kufanya kama ambavyo Rwechungura amefanya.

Haya ndiyo tunayoyafanya kila siku, mara nyingine bila kujua. Unaanza kazi katika ofisi mpya. Ukiwa mgeni mgeni, wenyeji wako wanakukaribisha kwa kukufanyia orientation isiyo rasmi. Unaambiwa sifa za kila mtu ofisini pale. Na mara moja, unatengeneza mafaili kichwani kwako yenye sifa 'hewa' za kila mkuu wako wa kazi ofisini hapo pamoja na wafanyakazi wenzio. Na bahati mbaya ni sifa mbaya mbaya ndizo huchukua nafasi ya orientation. Katika kuhusiana nao, unajikuta ukiyafanya yale yale aliyofanyiwa kijana Rwechungura tuliyemwona hapo juu. Umeruhusu mtazamo wako kuathiriwa na mitazamo ya wenyeji, ambayo mingi huwa ni biases ambazo si lazima ziwe na ukweli wowote, na hatimaye unaathiri namna unavyohusiana na hao ulioambiwa habari zao, nao wanajikuta wakikuchukulia vinginevyo.

 Je, matarajio yana tatizo gani?
Matarajio yetu kwa watu hujenga tabia inayotarajiwa. Inavyokuwa ni kwamba, matarajio yetu kwa mtu hubadili namna tunamvyotazama mtu huyo. Na namna hiyo mpya ya mtazamo kwa mtu huyo, huathiri namna tunavyohusiana nae, ambayo nayo hubadili namna mtu huyo anavyoitikia (react) mahusiano yetu kwake. Je, hili ni tatizo kwani? Jibu ni ndio kwa sababu hata namna matarajio yenyewe yanavyojengeka kichwani ni mkanganyiko mtupu. Angalia inavyokuwa.

Akili ya mwanadamu kwa asili haipendi kujichosha kwa shughuli zisizo na uharaka wala umuhimu. Sababu ni kwamba dunia imejaa taarifa nyingi mno kiasi kwamba tungeumbwa kwa namna ambayo kila unachokiona unaki-analyze hatua kwa hatua, ingekuwa kazi kushughulia taarifa zote zinazotujia kupitia macho, masikio, na kadhalika. Kwa hiyo, tunajikuta kwa kawaida tunatengeneza short cuts za ku-manage taarifa hizi. Short cuts hizi ndio hicho tunachokiita matarajio yanayotumika kama reference katika kukielewa kile tunachokutana nacho, kinachofanana fanana na kile tunachokijua tayari. Lengo ni kurahisisha kazi ya kuutambua ulimwengu na walimwengu.

Sasa ilivyo ni kwamba taarifa zenyewe zinazotujia kila siku, mara nyingi huwa ambiguous yaani haziko wazi sana kiasi kwamba haiwezekani kuziingiza kichwani bila kwanza 'kuzishughulikia' kwa kuzichanganya na tafsiri zetu ili zilete maana. Zisipoleta maana hutaweza kuzikumbuka. Kwa hiyo inabidi uzifinyange zifanane fanane na reference ya kichwani. Matokeo yake, utakuta tunachokikumbuka huwa ni tulichokuwa nacho kichwani badala ya kile tulichokutana nacho. Na wakati mwingine unapokutana na kinachofanana na kile kinachofanana na kile ulichokutana nacho awali, unajikuta 'ukijikumbuka mwenyewe', yaani ukikumbuka matarajio yako, kuliko unavyokumbuka jambo halisi. Na kama tulivyosema, ni matarajio hayo ndiyo yanayoathiri mahusiano yako na unayekutana naye anayefanana fanana na yaliyotarajiwa.

Tunajifunza nini kwa ujumla?
Imani zetu, matarajio yetu, kwa watu wengine huwafanya watende kama tunavyotarajia. Na ilivyo ni kwamba, hata namna tunavyoingiza taarifa kwenye fahamu zetu, ni mkanganyiko mtupu. Kwanza, tunachagua cha kukumbuka. Pili, tunachokikumbuka kinaathiri tunavyokielewa tunachokutana nacho. Maana yake ni kwamba, pamoja na uzuri wa kuwatazama watu kwa matarajio fulani, ni vizuri kuwapa watu nafasi ya kuwa halisi. Wajitetee wenyewe, na sio watetewe na makundi yao uliyowapa wewe. Hakuna haja ya kupekua mafaili tuliyo nayo akilini, ili kuelewa tabia za watu. Ikiwa ni lazima kutumia matarajio, basi ni vyema matarajio hayo yakawa chanya, ili ikibidi, athari yake iwe chanya.

Si sawa ukitana na dada wa Kimachame, mara moja akili yako inawaza 'Mpalestina' huyu. Unajuaje kuwa huenda aliyekuambia hayo naye alisikia kwa aliyekuwa na mashindano ya kikabila na Wamachame? Ndio. Au unajuaje kuwa huenda aliyekwambia hayo alikuwa na bahati mbaya ya kukutana na dada mmoja wa Kimachame asiye na tabia alizozitarajia? Ni sawa na kumsikia mtu alilalamika talaka zimekuwa nyingi siku hizi, shauri ya kusikia rafiki zake wawili wameachana na wenzi wao.

Tunachokisema hapa ni kwamba Meneja mwenye imani ya jumla kuwa wanafunzi waliosoma chuo A wana uwezo kuliko wanafunzi waliosoma chuo B na C, hatimaye huweza kuwafanya wanafunzi hao wakafanya kama alivyotarajia. Yaani wale wa chuo B na C wakaharibu na wale wa chuo A wakafanya vizuri. Tunachomfahamisha meneja huyu, ni kuwa aachane na matarajio yake, na awape vijana hao nafasi sawa ya kufanya wanachoweza. Kisha aamue nani mwenye uwezo wa kazi.

Tunachokisisitiza hapa ni kwamba mzazi anayeamini kuwa mwanae wa pili amezaliwa na ugomvi wa asili, wakati mwanae wa kwanza ni mpole, hujikuta akihusiana nao kwa namna tofauti, na hatimaye watoto hao wawili huwa na tabia hizo hizo alizozitarajia na kisha yeye huhitimisha kuwa ni kweli wa kwanza ni mpole na wa pili ni mgomvi kwa asili, kumbe ni yeye amechangia hali hiyo kwa 1) kugeneralize tabia ya mtoto kwa kutumia tukio moja au vitukio kadhaa vya kigomvi 2) kuhusiana na mwanae huyo kwa mujibu wa generalization hizo ambazo kimsingi zilizokuwa na makosa. Tunampa ushauri wa bure mzazi huyu kufuta matarajio yoyote kwa watoto hao wawili na kuwapa treatment chanya tena iliyo sawa, na kama tulivyoona, uwezekano ni mkubwa watoto hao wakaathika chanya kwa kutenda sawa sawa na matarajio chanya ya mzazi.

Inawezekana ukielewa.

Maoni

  1. Hii makala ni murua. Mbali na uzito wa fikra, ambazo zinathibitishwa na watafiti mbali mbali, nafurahi jinsi unavyozielezea dhana husika kwa ki-Kiswahili.

    JibuFuta
  2. Asante sana kwa kupita huku Profesa Mbele.

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Pay $900? I quit blogging

Haiba ni nini?

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Heri ya mwezi mpya!