Unavyoweza Kumrekebisha Mtoto Mjuaji Anayejiona Bora

PICHA: Psychology Today


Kujiona bora ni kujiamini kupindukia. Mtu anayejiamini kupita kiasi, mara nyingi, anaamini anazo sifa ambazo watu wengine hawana. Unapoamini unazo sifa za ziada kuliko wengine ni rahisi kuwa na kiburi. Kuamini watu wengine hawawezi kuwa bora kama wewe kunakufanya uwadharau.

Mtu mwenye kiburi na dharau hupata shida kuishi na watu. Kwa kawaida, huwaona wengine kama watu wasiojua, wanaopungukiwa kile alichonacho yeye. Mtazamo wa namna hii humtenga na watu kwa namna mbili.

Kwanza, huwapuuza wengine. Huamini anaweza kufanya mambo yake mwenyewe bila kupata msaada wa watu. Pili, hana uwezo wa kujua mahitaji ya wengine. Kutokujua wengine wanajisikiaje inaweza kuathiri namna mtu anavyoishi na watu.

Kuishi vizuri na watu kunategemea uwiano wa hali ya kujiamini na kuwaamini wengine. Tunahitaji kujiamini lakini sio kwa kiwango cha kuwa kiburi. Tunahitaji kujiamini bila kuwapuuza wengine. Ili kujiamini kwetu kuwe na maana lazima kwende sambamba na kuona thamani ya watu wanaotuzunguka.

Kama ilivyo kwa tabia nyingine nyingi, hatuzaliwi na tabia ya ujuaji na kujiona bora. Malezi ndiyo yanayotengeneza hali ya kujiona watu bora kuliko wengine.  Namna gani wewe kama mzazi unamlea mwanao inaweza kuumba kiburi na dharau ndani yake. Katika makala haya tunaangazia viashiria vya tabia hii, aina ya malezi yanayochangia tabia hii na hatua za kuchukua kumrekebisha mambo.

Viashiria

Kiashiria cha mwanzo kabisa kwa mtoto mdogo ni namna mtoto anavyoitikia pale anapoachwa na mzazi wake. Akiwa na miezi michache pungufu ya mwaka, mtoto wa kundi hili anapoachwa na mzazi wake, asubuhi kwa mfano, hulia lakini huwa haoneshi msisimko mzazi wake anaporudi baadae. Tabia hii ikikomaa, mzazi unaweza hata kuondoka na bado mtoto asilie na ukirudi anaweza asiwe na habari kama umerudi. Maana yake ni kwamba ameamua kujiondolea ‘presha’ kwa ‘kukupotezea.’

Pili, ni tabia ya kutokuwa tayari kurekebishwa hasa anapofikia miaka mitatu. Mtoto asiye na kiburi ni mwepesi kukubali makosa yake. Mtoto wa kundi hili anapoambiwa jambo asilolipenda ni mwepesi ‘kuzira’ kuonesha kuwa hapendi kuambiwa makosa yake. Pia ana imani kuwa anastahili zaidi ya wengine. Hutarajia upendeleo maalum na hutamani kupata zaidi ya wengine. Ni mtoto asiyejali wengine kwa sababu kwake kile anachohitaji yeye ndicho chenye umuhimu.  

Katika michezo, mtoto huyu hapendi kuongozwa. Ingawa si mgomvi kama mtoto mkorofi, lakini hujikuta matatani kwa sababu anapenda ‘kuwapelekesha’ wenzake. Furaha yake ni kuonekana mjuaji wa karibu kila kitu na hapendi wenzake wanapojua kuliko yeye. Huamini kile anachokijua yeye ndicho bora na wengine wana kazi ya kufuata kile anachokijua yeye.

Kadri umri unavyoongezeka, anaweza ‘kujichanganya’ na watu, lakini lazima watu hao waheshimu uwezo na uwezo alionao. Hapendi kuambatana na watu wanaothubutu kumwambia kile asichotaka kusikia. Kwa hiyo anapojikuta kwenye mazingira ya ‘wajuaji’ wenzake, huwa ni mtu mkimya anayependa kufanya ‘shughuli’ zake bila kuingiliwa.

Anapofikia umri wa utu uzima, anakuwa haoni haja ya urafiki wa karibu na watu. Kwake, rafiki ni yule anayemnufaisha. Kimapenzi, huyu si mtu mwenye uwezo wa kuelewa hisia zake wala kuthamini hisia za mwenzake. Kukosa hisia humfanya awe mwepesi kuwaumiza wengine na bado akashangaa inakuwaje mtu anaumia.

Malezi yanavyochangia

Wapo wazazi wasiopenda ‘kelele’ za watoto. Tuchukulie mfano mtoto analalamika kuwa amejikwaa na anaugulia maumivu. Mzazi asiyependa kusumbuliwa anaweza kumnyamazisha mtoto, ‘Hujaumia bwana jikaze!’ ‘Mtoto mzuri haliagi!’ Lengo ni kutuliza ‘kelele’ za mtoto.

Lakini kwa upande wa mtoto, maneno hayo yanamaanisha kupuuza maumivu yake. Moyoni anajua anaumia lakini anaambiwa, ‘Mtoto mzuri hatakiwi kulia!’ Kwa kuwa mtoto angependa kuwa ‘mtoto mzuri’ hupata wasiwasi na hisia zake. Anajua anaumia lakini kukubali ana maumivu aliyonayo maana yake anakuwa mtoto mbaya.

Mzazi akifanya hivi mara nyingi, mtoto hujifunza kukana hisia zake. Mtoto huanza kuamini kuelezea hisia ni kosa na ni udhaifu. Hali hii hujenga tabia ya ‘usanii’ wa kuonesha hisia tofauti na vile wanavyojisikia ndani. Mfano, mtoto anaweza kucheka kwa nje wakati ndani anaumia. Lengo ni kumfurahisha mzazi.

Lakini kwa asili watoto wanapenda ukaribu na wazazi. Inaposhindikana kupata ukaribu huo kwa kueleweka hisia zao wanajifunza ‘kupotezea’ ukaribu na watu. Hali hii inaweza kuwafanya wawe watu wasiohitaji ukaribu sana na watu. Mtoto anajua kile anachojua ni sahihi hakieleweki kwa wengine, huanza kujifariji kwa kujidanganya kuwa anajitosheleza hata akiwa peke yake. Hisia za kujitosheleza zinaanza kujenga ukuta wa kihisia na watu wengine.

Sambamba na mtoto kuanza kuamini anajitosheleza jambo la pili linaweza kutokea. Kwa kawaida, wazazi wasiopenda kusumbuka na kelele ‘huwatuliza’ watoto kwa kuwapa vitu. Mtoto anapolia, kwa mfano, anapewa midoli na vifaa vya kuchezea badala ya kupewa usikivu. Mtoto hujifunza ‘kuhusiana’ na vitu kuliko watu. Katika mazingira hayo, ili ‘kumpata’ mzazi mtoto hulazimika kuonyesha alivyo mjuzi. Ujuaji hubaki kuwa fahari pekee ya mtoto badala ya urafiki wake na mzazi.

Kwa kuwa ni rahisi mzazi kumsifia mtoto kuliko kushughulika na usumbufu wake, mzazi anaweza kukosa kiasi anapomsifia mtoto. Ikumbuke kuwa mtoto tayari anaamini hakuna mtu anajali hali yake. Faraja yake inakuwa kusifiwa kwa kuonesha uwezo na ujuzi. Sifa zinakuwa ndio utumwa wake.

Taratibu anaanza kuamini thamani ya mtu ni ujuaji wake. Anapofahamu kitu wasichokijua wengine, hujichukulia kama mtu wa thamani kuliko wengine. Ujuzi huwa mtaji wa kukubalika kuliko namna wanavyoishi na watu.

Unachoweza kufanya

Jenga urafiki na mtoto badala ya kuwekeza kwenye matarajio. Urafiki maana yake ni kuelewa anavyojisikia, kujua maumivu na hofu alizonazo. Mtoto anayeeleweka hana sababu ya kudharau watu.

Urafiki na mtoto usitegemee kile anachokiweza. Urafiki na mwanao ni wajibu. Kumpenda mtoto kusiwe ‘mafao’ ya kufikia matarajio uliyonayo kwake. Mtoto anabaki kuwa mwanao hata kama hajafikia matarajio fulani.


Tatu, epuka kumsifia mtoto kupita kiasi. Sifa zinajenga utegemezi zisipotolewa kwa utaratibu. Msifie bila kumfanya ajione yeye ndiye bora kuliko wengine. Kila inapowezekana hakikisha anasikia ukiwasifia na wengine. Itamfundisha kuwa wapo wanaoweza pia kama yeye. 

Maoni

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Tumia Mbinu Hizi Kuelewa Unachokisoma -3

Haiba ni nini?

Ukuaji wa Kiakili na Kimwili kwa Mtoto wa Miaka 0 – 3