Hakuna Ulazima wa Kushinda Kila Majadiliano

PICHA: Elly Prior

Chukulia mnajadiliana jambo na rafiki yako. Inaweza ikawa ni mtandaoni, nyumbani, ofisini au mahali kwingineko. Katika mazungumzo yenu unabaini hamuelewani. Kile unachoona ni sahihi, sivyo anavyoona mwenzako. Kila mmoja wenu anajaribu kutetea upande wake kuliko anavyoelewa mtazamo wa mwenzake.

Unadhani kipi ni sahihi kufanya katika mazingira hayo? Je, ni busara kuendelea kuthibitisha ulivyo sahihi hata kama ni dhahiri mwenzako hayuko tayari kukuelewa? Unajisikiaje mwenzako akikuonesha haukuwa sahihi?

Mara nyingi tunafikiri kushindwa na kutokuwa sahihi ni udhaifu. Tunapambana na wasiotuelewa kwa mabishano na majibizana kwa lengo tu la kuonesha tulivyo kwenye upande sahihi.

Unazungumza ili kushinda?

Nakumbuka siku moja nilishiriki mjadala mmoja kwenye mitandao ya kijamii. Katika mjadala huo, kulikuwepo na pande mbili zinazotofautiana kimtazamo. Kadri mjadala ulivyoendelea, niligundua hapakuwa na jitihada za pande mbili hizo kuelewana. Kila upande ulisimamia hoja zake kwa lengo la kushinda ‘mdahalo’ badala ya kupata mtazamo mbadala.

Ndivyo tunavyofanya hata nyumbani. Tunapoongea na wenzi wetu, wakati mwingine, ndani yetu tunatafuta kushinda. Tunafikiri kushinda ndio alama ya uimara na msimamo. Mume anajenga hoja kutafuta ushindi na mke naye anajitetea kutafuta kusikika. Kila mmoja anazungumza ili ashinde. Hakuna anayetafuta kumweelewa mwenzake.

Kushinda kunabomoa

Mazungumzo ya kutafuta mshindi hayaleti uwezekano wowote wa maelewano. Mara nyingi mazungumzo ya namna hii huenda sambamba na hisia. Katika mjadala nilioutaja hapo awali, mwisho wa mjadala ule wa mtandaoni washiriki waliishia kuzodoana, kusemana na kuitana majina. Hakuna aliyekuwa tayari kushindwa kwa sababu lengo lilikuwa ni kushinda.

Kwa kawaida, mtu anayetafuta ushindi anapogundua anashindwa ni rahisi kukasirika. Hasira ni silaha ya kujihami na fedheha ya kushindwa. Bahati mbaya, watafiti wanasema, unapokuwa na hasira huwezi kujishughulisha kuelewa mwenzako anafikiri nini.

Pia, kushinda kunaweza kuwa chanzo cha maumivu makubwa ya kihisia kwa anayeshindwa. Kwa kawaida,  anayetaka kushinda hawezi kujali hisia za mwenzake. Lengo lake ni kumdhibiti mwenzake kwa gharama yoyote hata ikibidi kwa kejeli na dharau dhidi ya hoja na utu wa mwenzake.

Ushindi unaopatikana katika mazingira kama haya haujengi. Wakati aliyeshinda akifurahia kuwa sahihi, aliyeshindwa anabaki na majeraha moyoni. Kwa kuwa kushindwa ni adhabu kwa wengi wetu, ushindi unaishia kutengeneza kiambaza cha kihisia kati ya aliyeshinda na aliyeshindwa.

Tujiulize, je kuna ulazima kushinda kila unapojadiliana jambo na mtu mnayetofautiana? Kama ni lazima, haiwezekani nyote wawili kushinda? Kama wote kushinda haiwezekani, hamwezi kujadiliana bila kutafuta mshindi?

Ushindi ni kusikiliza

Najaribu kufikiri uwezekano wa mtu kusema kile anachofikiri ni sahihi bila kumlazimisha mwenzake afikiri kama yeye. Naamini hili linawezekana. Lakini ili iwezekane, ni muhimu mtu huyu awe tayari kusikiliza kile kinachosemwa na mwenzake akifahamu kuwa na mwenzake naye anaweza kuwa sahihi kwa namna yake.

Najua yapo mazingira watu hulazimika kuwashawishi wengine kufuata upande wanaofikiri ni sahihi zaidi. Lakini ushawishi huu unakuwa na tija ikiwa unafanyika katika mazingira ya kirafiki. Ushawishi unaofanywa bila kutumia nguvu, bila kupuuza mtazamo wa anayeshawishiwa, una nafasi ya kujenga zaidi kuliko ushindi unaopatikana kwa mabavu na ujuaji.

Kuna nyakati ushawishi mzuri zaidi ni kushindwa. Kama unayeshindana naye haonekani kuelewa, mwache ashinde. Unapomwacha mwenzako unayefikiri hayuko sahihi ashinde, unampa nafasi ya kujiona anaheshimiwa. Mtu akishakukuheshimu, anaweza kukusikiliza vizuri wakati mwingine mtakapozungumza.

Kadhalika, wapo watu hupenda kuwashinda wengine kwa kunyamaza. Kunyamaza huwa ni hasira ya kujisikia kushindwa. Huna sababu ya kuendelea kujibizana na mtu anayekazana kushinda. Busara ni kumwacha atulie. Hasira zikipungua, tafiti zinasema, mtu huwa kwenye nafasi nzuri ya kuelewa kuliko anapokuwa amekasirika. 

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Pay $900? I quit blogging

Heri ya mwezi mpya!