Unahitaji Nidhamu ya Fedha Kujikwamua Kiuchumi

PICHA: usaa.com

Juma lililopita tuliongelea uwezekano wa mfanyakazi kujikwamua kiuchumi. Kubwa ni nidhamu. Unapokuwa na nidhamu ya mshahara, unaongeza uwezekano wa kuwa na usalama wa kifedha.

Swali linaweza kuwa, ‘Kinachomfanya mfanyakazi akose nidhamu ya fedha ni nini?’ ‘Inakuwaje mchuuzi mdogo wa bidhaa awe na nidhamu ya fedha kuliko Afisa wa Serikali?’

Majibu ni mengi. Moja ni uhakika wa kipato. Kwamba [mfanyakazi] una uhakika wa kupata mshahara mwisho wa mwezi hilo pekee linaweza kutosha kukuondolea nidhamu ya fedha.

Mjasiriamali/mchuuzi anaweza asiwe na uhakika huu. Kutokuwa na uhakika na kipato kunamwongezea umakini wa kutumia vyema kile anachokipata.  Kwa mfano, lazima ahakikishe kile alichonacho kinazalisha kumpatia faida itakayomsaidia kuendeshea maisha yake.

Hapa ndipo ilipo tofauti baina ya wafanyakazi na wajasiriamali. Mfanyakazi unaweza kutumia kila senti unayopata kwa matumaini ya kupokea mshahara mwisho wa mwezi.

Mchuuzi hawezi kuthubutu kufanya hivyo. Kwake, kile alichonacho ni mbegu ya kupanda kumpa uhakika wa kesho.

Kwa hiyo utaona mazingira ya kazi uliyonayo mfanyakazi hayakulazimishi kuwa na nidhamu. Ili uweze kujenga nidhamu hiyo unahitaji kufanya kazi za ziada. Usipofanya maamuzi ya dhati, ongezeko lolote la mshahara haliwezi kukupa unafuu wa maisha.

Makala haya yanapendekeza mbinu nne unazoweza kuzitumia kukabiliana na ukosefu wa nidhamu ya fedha. Mapendekezo haya manne yanadai mabadiliko makubwa ya tabia.

Ishi kwa bajeti

Kuishi kwa bajeti ni kufanya matumizi yaliyopangwa kabla. Kinyume chake ni ufujaji. Mtu ‘mfujaji’ hutumia kadri mahitaji yanavyojitokeza. Hapangi namna gani atatumia fedha zake.

Ni dhahiri ‘kufuja’ ni kazi rahisi kuliko mipango. Maisha yanayoongozwa na bajeti yana gharama ambayo si wengi tunaweza kuwa tayari kuilipa. Lakini kwa kuwa unataka kuona tija ya mshahara wako, lazima uwe tayari kulipa gharama hiyo.

Pangilia mwelekeo wa mapato yako kabla hujayapata. Jenga utaratibu wa kuweka kumbukumbu ya mapato na matumizi yako kila mwezi. Tabia hii inaitwa nidhamu. Mtu mwenye nidhamu huweka utaratibu mzuri wa kujiwajibisha.

Unapokuwa na utaratibu wa kujua wapi fedha zako zinaelekea na nini ufanye kurekebisha mwelekeo, huo unaitwa uwajibikaji. 

Ongozwa na sera ya fedha

Niliwahi kukutana na bwana mmoja aliyeniuliza swali gumu, ‘Sera gani inaongoza matumizi ya fedha zako?’ Nilidhani anatania. Nilifikiri mtu binafsi hawezi kuwa na sera inayotawala fedha zake. Baadae nilijifunza somo muhimu.

Sera ya fedha ni mwongozo wa matumizi ya fedha zako. Unapokuwa na sera unarahisisha kazi ya kuainisha kipaumbele cha mapato yako.

Bila kuainisha kipaumbele chako itakuwa vigumu kwako kujua namna gani unaweza kutumia kile kidogo ulichonacho kukamilisha malengo unayojiwekea.

Kwa mfano, unaweza kuwa na sera ya kuhakikisha matumizi yako ya kawaida (chakula, mavazi, nauli, burudani) hayachukui zaidi ya asilimia 20 ya mapato yako kwa mwezi.

Kadhalika, kulingana na kipato chako, unaweza kuamua asilimia 30 ya mapato yako lazima iekezwe kwenye akiba wakati asilimia 10 ikielekea kwenye sadaka au hisani kwa wenye shida. Vyovyote iwavyo kulingana na kipato chako, asilimia hizo zinaweza kuongezeka au kupungua kukidhi mazingira uliyonayo.

Pia, kwa kuwa tunaishi kwenye jamii inayotegemeana, unaweza kuwa na sera ya kutumia si zaidi ya asilimia 10 kuwasaidia ndugu na jamaa katika nyakati za shida na raha. Huu ni mfano wa sera binafsi ya fedha unayohitaji kuiandaa kulingana na mazingira yako.

Ondokana na madeni

Kukopa, kwa hakika, si jambo baya. Huwezi, kwa mfano, kufanya biashara kubwa bila kutumia fedha za mkopo. Ndivyo wanavyofanya wafanyabiashara wakubwa.

Tofauti na wafanyabiashara, wafanyakazi walio wengi hukopa kugharamia mtindo wa maisha ya kila siku. Kinachokopwa kinatumika kufanyia manunuzi ya vitu vya kawaida, kisha mshahara unatumika kulipia deni lisilozalisha chochote.

Kwa namna hii, wafanyakazi wengi wamejikuta wakigeuka kuwa watumwa wa mzigo mzito wa madeni. Huwezi kupiga hatua za maana bila kujikwamua kwenye madeni ya namna hii.

Ikiwa unaishi na madeni mabaya, weka mpango wa kuondokana na madeni haraka iwezekanavyo. Sambamba na hatua hiyo, epuka kujiingiza kwenye madeni yasiyo na sababu. Utaratibu wa kuweka ukomo wa matumizi kabla hujapata kipato chako unaweza kukusaidia kuepuka madeni. 

Wekeza kuongeza kipato

Kilio cha wafanyakazi wengi ni kukosekana kwa mtaji unaotosha kuwekeza. Hata hivyo, wapo waajiri huwadhamini wafanyakazi wao kupata mikopo kwenye taasisi za fedha. Kama una fursa hiyo, tumia mkopo kufanya uwekezaji mdogo kujiongezea kipato.

Lakini hata kama fursa hiyo haipo, bado unaweza kutumia kanuni ya kuweka akiba inayoweza kukutengeneza mtaji. Tuchukulie mfano mshahara wako ni Sh 600,000 kwa mwezi. Ukiamua kutenga kiasi cha Sh 50,000 tu kwa mwezi utakuwa na Sh 600,000 baada ya miezi 12.

Lakini pia unaweza kuboresha kanuni ya kuweka akiba kwa kuongeza kiasi fulani kisichobadilika kwa kila mwezi unaofuata.

Kwa mfano, baada ya kufanikiwa kuweka Sh 50,000  mwezi huu, unaongeza Sh 10,000 kwa mwezi ujao na kufanya kiasi utakachokitenga kiwe Sh 60,000. Mwezi unaofuata unaweka Sh 70,000, Sh 80,000 na kuendelea.

Ukiufuata utaratibu huu kwa miezi 12 utakuwa umejiwekea akiba ya Sh 1,260,000. Hiki si kiasi kidogo kwa mshahara wa Sh 600,000 kwa mwezi. Ikumbukwe kwa mshahara huo unaweza kujibana na kuweka akiba zaidi.


Kikwazo kingine kwa wafanyakazi ni woga wa hasara na aina ya biashara wanayoweza kufanya. Mambo mawili hapa. Kwanza, buni huduma inayoweza kutatua tatizo la watu wanaokuzunguka. Mahitaji na changamoto za watu wanaokuzunguka ndiyo fursa kwako.

Pili, usiogope kushindwa au kuibiwa. Vaa ujasiri uwe tayari kujifunza kwa kushindwa. Tunajifunza kwa makosa.

Maoni

  1. Ni somo zuri sana watu wengi kweli wanakosa nidhamu ya pesa na wengine wanakuwa na woga wa kula hasara ila kuna mtaalamu mmoja (Robert Kiyosaki) anasema kwamba wasomi wengi wanakuwa na woga wa kufeli kutokana na jinsi walivyokuwa wamepitia mafundisho ya walimu wao kwamba walikuwa wakiambiwa usiposoma utafeli ,basi imekuwa hivyo hata katika maisha yao wanaogopa kufeli na yule ambae hajasoma sana anakuwa na nidhamu ya pesa kwa sababu hana ile dhana ya kufeli katika Saikolojia take.

    JibuFuta
  2. Ahsante San Mr Christian Bwaya kwa makala hii

    JibuFuta
  3. Ahsante San Mr Christian Bwaya kwa makala hii

    JibuFuta
  4. asante sana kwa makala hii

    JibuFuta
  5. asanteh sana nitafwata ushauri wako

    JibuFuta
  6. Safi Sana! Nimekutana na somo hiliimenifunza mengi,hasa kuhusu kupanga bajeti kabla ya kupata mshahara/kipato,pia uwekaji wa akiba.

    JibuFuta
  7. Asante Sana kiongozi SoMo zuri Sana hili mungu akutangulie

    JibuFuta
  8. SoMo zuri Sana hongera Kwa elimu yako umetufumbua macho wahanga wengi ni wafanyakazi kwani elimu tunayosoma darasani imetuingia tofauti kisaikolojia kuwa kufeli ni kosa

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Pay $900? I quit blogging