Wajibu wa Mzazi kwa Mtoto Kisheria -2


SHERIA ya Mtoto Na. 21 ya 2009 inamtambua mtoto kama mtu yeyote mwenye miaka pungufu ya 18. Sheria hii ilitungwa kukidhi matakwa ya makubaliano na mikataba ya kimataifa inayolenga kulinda haki, maslahi na ustawi wa mtoto.

Kimsingi sheria hii inaainisha wajibu walionao wazazi, walezi na jamii kwa ujumla kwa mtoto na inatoa mwongozo pale yanapojitokeza mazingira yanayohatarisha ustawi wa mtoto.

Kwa mujibu wa sheria hii, maslahi na ustawi wa mtoto ndio msigi mkuu wa maamuzi yoyote yanayofanywa na mtu, taasisi, mahakama ama vyombo vyovyote vya kimaamuzi.

Ndio kusema wazazi na jamii kwa ujumla wana jukumu la kuhakikisha mtoto analindwa dhidi ya namna zote za uonevu, udhalilishaji kijinsia, kikabila, umri, dini/imani, lugha, maoni ya kisiasa, ulemavu, afya, hali ya uchumi, anakotoka na hata ukimbizi.

Katika makala haya tunaangazia haki ya kwanza aliyonayo mtoto kisheria. Hapa tunazungumzia haki ya mtoto kupata utambulisho wake binafsi unaoeleweka.

Jina

Jina ni hatua ya kwanza ya kumpa mtoto utambulisho wake. Mara baada ya kuzaliwa, wazazi au walezi wanawajibika kumpa jina litakalomtambulisha kama binadamu aliyekamilika.

Sheria haijafafanua zaidi kuhusu jina la mtoto. Hata hivyo, ni dhahiri kuwa jina analopewa mtoto litakuwa sehemu ya maisha ya mtoto kwa muda mrefu. Ni busara jina hilo likazingatia maadili, staha na utu.

Uraia

Kadhalika, mtoto anayezaliwa na m-Tanzania ana haki ya kutambulika kama raia halali wa Tanzania. Njia moja wapo ya kumhakikishia haki hiyo, ni kumwandikisha kwenye mamlaka zinazotambuliwa kisheria ambazo ndizo zitakazompatia cheti cha kuzaliwa.

Kwa kutokuelewa, wazazi wengi hawajishughulishi kuhakikisha mtoto anapata cheti cha kuzaliwa. Ni vyema kuelewa kuwa mtoto atalazimika kuwa na cheti ili kupata haki zote anazostahili raia wa Tanzania kama vile elimu, huduma za afya, hati ya kusafiria na vitambulisho mbalimbali.

Wazazi

Utambulisho wa mtoto ni pamoja na kumwezesha kuitambua familia yake. Sheria hii inampa mtoto haki ya kuwafahamu watu waliomzaa. Ndio kusema, mtu yeyote anayemlea mtoto kwa sababu yoyote ile ana wajibu wa kisheria kumjulisha mtoto nani hasa ni mzazi/wazazi wake.

Inafahamika kuwa wapo akina mama waliowapata watoto wao katika mazingira yenye utata. Wakati mwingine wasingependa watoto kuwafahamu baba zao. Lakini fikiria unaishi bila kufahamu kwa hakika baba yako ni nani. Ni adhabu fulani ya kisaikolojia. Sheria hii imelizingatia hilo.

Kwa mujibu wa sheria hii, na bila kuingilia sheria nyinginezo, mtu yeyote hana haki ya kumficha mtoto baba/mama yake wa kumzaa. Kumfahamu baba na mama yake ni haki yake.

Familia tandaa

Sambamba na kuwafahamu wazazi wake halisi, mtoto pia ana haki ya kuitambua familia tandaa. Familia tandaa ni ndugu wa pande zote mbili, yaani upande wa baba na mama.

Ndio kusema mzazi au mlezi ana wajibu wa kuhakikisha mtoto anafahamu ukoo wake vizuri kama sehemu ya kulinda utambulisho wake. Mtoto awafahamu bibi, babu, shangazi, wajomba na ndugu wengine wa ukoo.

Kisaikolojia, mwanadamu anajiamini zaidi anapowafahamu ndugu zake. Fikiria unaishi na wazazi wako lakini hujui ndugu zako. Unaweza kuwaza mengi.  Ni vyema kila inapowezekana wazazi kufanya jitihada za kuwaunganisha watoto na ukoo wao. Kuna leo na kesho.


Inaendelea

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Pay $900? I quit blogging

Heri ya mwezi mpya!