Kukosa Ajira Kusikufanye Ukose Kazi



Inakadiriwa kuwa kati ya watu 800,000 na 1,000,000 hapa nchini wanaingia kwenye soko la ajira kila mwaka. Hawa ni vijana wanaomaliza masomo yao kwa ngazi mbambali za elimu au wale wanaokosa nafasi ya kuendelea na masomo katika mfumo rasmi wa elimu.

Mfumo wetu wa elimu unachuja wanafunzi kwa kuangalia sifa za ufaulu wa mitihani. Ili mwanafunzi aweze kuendelea na masomo kwa ngazi inayofuata, analazimika kupata sifa mahsusi. Anapopungukiwa sifa hizo, hulazimika kurudi mtaani kutafuta namna anavyoweza kuendesha maisha yake.

Bahati mbaya kwa kundi hili kubwa linalochunjwa ni kwamba ajira nyingi rasmi zimeendelea kutumia elimu kama kigezo muhimu. Mwajiri anapotangaza nafasi za kazi kitu cha kwanza anachokiulizia ni cheti. Hata kwa kazi za ufundi zisizohitaji taaluma kubwa, bado mwombaji anaweza hulazimika kuwa na sifa fulani za kitaaluma ambazo wakati mwingine hazisaidii kuboresha kazi.

Hali si tofauti sana kwa wale wateule wachache wanaobahatika kuhitimu ujuzi rasmi unaotambuliwa na vyeti. Uwezo wa uchumi wetu kutengeneza nafasi mpya za ajira zitakazokidhi mahitaji ya vijana hawa bado ni mdogo. Serikali ambayo ndiye mwajiri mkuu, kwa mfano, haijaweza kuajiri kwa miaka miwili. Pia, tunaambiwa biashara nyingi katika sekta binafsi zinafungwa.

Katika mazingira kama haya, ni dhahiri tatizo la ukosefu wa ajira litaendelea kuwaathiri watafuta ajira wengi hapa nchini bila kujali ikiwa wanao ujuzi rasmi ama la.

Makala haya yanalenga kuwasaidia watu ambao, kwa sababu moja au nyingine, wanatafuta ajira na bado hawajafanikiwa kuzipata. Tunaangazia jitihada kadhaa wanazoweza kuzitafanya kutatua tatizo badala ya kusubiri ‘mfumo’ uwatafutie majibu. Swali kuu litakalotuongoza ni, unapokosa ajira maana yake ni nini?

Nafasi za ajira hazitoshi

Tuanze na dhana ya soko la ajira. Soko ni utaratibu wa kuuza na kununua. Mwajiri anapotafuta mtu mwenye ujuzi wa kumsaidia kutoa huduma zake, ni mnunuzi. Mwajiriwa anayetafuta mtu wa kununua ujuzi wake, anakuwa muuzaji sokoni. Hawa wawili wanategemeana. Mmoja anazo raslimali, aghalabu za fedha, kumwezesha kununua ujuzi na mwingine anao ujuzi anaofikiri unahitajika.

Kwa bahati mbaya, uhusiano huu kati ya muuzaji na mnunuzi wa ujuzi una ukomo wake. Kama tulivyotangulia kuona, uwezo wa waajiri kutengeneza nafasi za ajira hautoshelezi mahitaji halisi sokoni. Hali hii husababisha ushindani mkali ambao mara zote huliathiri kundi kubwa litakaloachwa bila ajira.

Waathirika wakubwa kwenye ushindani huu mkali wa soko, ni watu wanaoamini hawawezi kuishi bila kuuza ujuzi wao kwa waajiri. Suluhisho ni kubadili mtazamo. Badala ya kufikiri namna ya kuuza ujuzi wako kupitia ajira, jaribu kufikiri namna ya kuutumia ujuzi wako kufanya kazi itakayosaidia kuendesha maisha yako.

Kutokuajirika kwa watafuta kazi

Upande wa pili wa mjadala wa ukosefu wa ajira ni ukosefu wa sifa miongoni mwa watafuta kazi. Madai ya waajiri wengi ni kwamba watafuta kazi wengi hawakidhi vigezo vya kazi. Kwa mfano, zipo nafasi zinazotangazwa mara kadhaa, na usaili unabaini hakuna mwenye sifa kati ya walioomba.
Wakati mwingine baadhi ya waajiri hulazimika kutafuta watu kutoka nje ya nchi kujaza nafasi ambazo zimeshindikana kuzajwa na kundi kubwa la watafuta kazi wanaodaiwa kukosa sifa.

Suluhisho la kutokuajirika, ni watafuta kazi kufanya jitihada za kukuza ujuzi badala ya kufikiria ubora wa vyeti na ufaulu wa darasani. Upo ukweli kwamba vyuo vyetu vinazalisha wahitimu wenye nadharia zisizo na uhusiano wa moja kwa moja na ufumbuzi wa matatizo yanayoikabili jamii yetu.

Huu ni ushauri kwa wanafunzi. Badala ya kufikiria kupata alama za juu kwenye mitihani, ipo haja ya kuanza kufikiri namna gani utaweza kutumia maarifa hayo unayojifunza darasani. Ukiweka kuweka bidii kwenye ujuzi badala ya maarifa, utajiweka kwenye nafasi nzuri ya kufanya kazi bila kulazimika kutafuta ajira.

Fursa za kazi haziishi

Kila tatizo linaloikabili jamii yetu ni fursa ya kazi. Ukiweza kuwa na ujuzi unaokusaidia kutatua tatizo fulani unaloliona kwenye jamii, unajiweka kwenye nafasi ya kupata kazi.

Bahati mbaya ni kwamba jamii yetu inakabiliwa na kila aina ya matatizo yanayoendelea kuzalishwa kila uchao. Matatizo haya ni fursa za kazi zisizo na kikomo kwa kila anayetafuta kazi.

Changamoto, hata hivyo, ni uwezo wa kutazama namna unavyoweza kutumia ujuzi ulionao kutatua matatizo. Fanya ujasiriamali wa ujuzi kama umebahatika kupata ujuzi rasmi. Endesha semina kwa jamii kuwasaidia watu kupata majibu ya changamoto walizonazo. Hiyo ni kazi ambayo hakuna mtu anaweza kukunyima.

Pia unaweza kutoa huduma zinazohitajika na watu wanaokuzunguka. Fikiria, kwa mfano, mtu aliyeanzisha wazo la vyoo vya kulipia mjini. Alitazama tatizo, akaona fursa. Huo ndio unaitwa ujasiriamali na inaweza kuwa njia ya uhakika kuelekea kwenye mafanikio makubwa kuliko kutafuta ajira.

Kisingizio cha vijana wengi ni mtaji. Ukweli, hata hivyo, ni kwamba fedha hufuata mtaji wa wazo na sio kinyume chake. Ukiwa na wazo linaloeleweka, wenye mtaji wa fedha watakuunga mkono. 

Tumia vipawa ulivyonavyo

Kila binadamu amewekewa vitu vya pekee ndani yake. Hata kama hujafahamu kipaji ulichojaliwa na Mwenyezi Mungu, hiyo haiondoi ukweli kwamba ndani yako umebeba raslimali muhimu ya mafanikio yako.
Kiwango cha elimu ulichonacho hakiamui kiwango cha mafanikio utakayoyapata. Elimu isiyokwenda sambamba na kukuza vipaji ambavyo tayari unavyo, inaweza kuishia kutukatisha tamaa.

Aidha, soko la ajira linapokuamulia mwelekeo wa kazi unayopaswa kuifanya,  tatizo la ajira haliwezi kukoma. Mahitaji ya soko yakibadilika, watu wanajikuta hawana kazi. Kuna umuhimu elimu ijenge kwenye msingi wa vipaji vya watu ili kutatua tatizo la ukosefu wa ajira.

Ushauri kwako uliye kijana. Ukiweza kuvibaini vipaji ulivyonavyo, ukaelekeza nguvu zako kuvitumia, hutakosa kazi hata katika mazingira ambayo nchi inakabiliwa na ukosefu mkubwa wa ajira. Kazi yako inaishi ndani yako. Usiitafute nje.

Maoni

  1. Sina zla zaidi Bali niseme asante

    JibuFuta
  2. Sina zla zaidi Bali niseme asante

    JibuFuta
  3. Asante Stephen Mligo na Richmal Vibes kwa kuwa wadau muhimu wa blogu yetu. Proud of you!

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Pay $900? I quit blogging