Je, Walimu na Wazazi Wanazungumza Lugha Moja Kujenga Maadili ya Watoto?

PICHA: Godot13


SUALA la maadili limezua mjadala mrefu katika siku za hivi karibuni hasa baada ya wanasiasa kupinga wasichana wajawazitokuendelea na masomo yao kwa sababu ya ujauzito. Kauli hizo zilipingwa vikali na wanaharakati wenye msimamo wa kuwatetea watoto wa kike. Hoja yao ni kwamba kumnyima msichana fursa ya kupata elimu kwa kosa la kuwa mhanga wa mfumo holela usiomjenga msichana kimaadili ni kutokuyatazama mambo katika upana wake.

Tunapozungumzia maadili ya wanafunzi, kimsingi hatukwepi kusaili ushirikiano wa karibu kati ya wazazi, walimu, wanasiasa na jamii kwa ujumla. Jitihada za kujenga maadili katika ngazi ya familia, kwa mfano, lazima zioane na jitihada kama hizo katika eneo la shule. Ikiwa tunataka kweli kujenga kizazi cha watoto wenye maadili, lazima kuhakikisha juhudi za wazazi zinakwenda sambamba na juhudi zinazofanywa na walimu. Panapotokea mazingira ambayo wazazi na walimu wanapishana mbinu, ni vigumu kujenga kizazi cha watoto wenye maadili.

Utafiti uliofanywa na Dk Daniel Mngarah wa ChuoKikuu cha Dodoma na kuchapishwa na Jarida la “Global Journal of Human Social Sciences” Toleo la 17, Na.4 la 2017 unaweza kutupa picha halisi ya ushirikiano uliopo kati ya wazazi na walimu. Kwa mujibu wa Dk. Mngarah, ushirikiano baina ya wazazi na uongozi wa shule umekuwepo kwa muda mrefu ingawa lengo limekuwa ni taaluma ya wanafunzi. Kamati za shule zinapoitishwa, kwa mfano, hoja kuu imekuwa ni ‘namna ya kuinua ufaulu wa wanafunzi.’ Suala la maadili ni kama halijapewa kipaumbele katika mipango na sera za elimu.

Hata hivyo, tafiti mbalimbali zinaonesha kwamba maadili yana nafasi kubwa katika safari ya kujifunza aliyonayo mwanafunzi. Ni dhahiri mwanafunzi mwenye nidhamu na usikivu, anakuwa kwenye nafasi nzuri zaidi ya kujifunza.

Katika utafiti huo, pamoja na mambo mengine, Dk Mngarah alilenga kuchunguza ikiwa walimu na wazazi wana mtazamo unaofanana katika kujenga maadili ya wanafunzi na athari ya mitazamo hiyo katika kushughulikia nidhamu ya wanafunzi. Matokeo ya utafiti huo muhimu yanaonesha hali ya kushangaza kidogo. Kwanza, walimu wakuu walidai hapakuwa na ushirikiano unaoeleweka baina ya shule na wazazi. Wazazi, kwa mfano, walidaiwa kupinga juhudi kubwa zilizokuwa zikifanywa na uongozi wa shule katika kujenga nidhamu ya watoto. Adhabu zilipotolewa, wazazi walikuja juu na kuzitafsiri kama kisasi kati ya walimu na wanafunzi wanaoadhibiwa.

Mkuu mmoja wa Shule anatoa mfano wa mzazi aliyefika shuleni hapo kumshtaki mwalimu aliyekuwa amemwadhibu mwanafunzi kwa utovu wa nidhamu. Inavyoonekana, mwanafunzi alikuwa ameadhibiwa kwa tabia yake ya kutoroka shule na kwenda kuonana na rafiki yake wa kiume pale kijijini. Mwanafunzi huyu alipoadhibiwa, alikwenda kushitaki kwa mzazi kwamba walimu wana chuki naye. Mzazi alipofika shuleni, ilibidi mwalimu na mwanafunzi husika waitwe. Kwa kuwa mwalimu alikuwa ana hakika na kile alichokuwa anakisema, aliomba begi la mwanafunzi lipekuliwe. Begi lilipopekuliwa, zilikutwa nguo ‘za nyumbani’ zilizokuwa zinavaliwa muda wa kutoroka unapowadia. Baadae ilifahamika kwamba mwanafunzi huyo alikuwa mjamzito.

Walimu, kwa upande wao, walionekana kutilia mkazo zaidi kwenye ufaulu wa wanafunzi kuliko tabia na mienendo yao. Mwalimu mmoja ananukuliwa akisema, “Nimeajiriwa kufundisha. Hiyo ndiyo kazi yangu. Sioni sababu ya walimu kuhangaika na masuala ya maadili wa wanafunzi. Wazazi wenyewe ndio hawa na wakuu wa elimu wanataka matokeo makubwa.” (Tafsiri ni yangu). 

Walimu hawakuonekana kushughulika sana na masuala ya maadili isipokuwa kwa utashi wa mwalimu mmoja moja. Kwa upande wao, wazazi walionekana kulichukulia suala la maadili kama wajibu wa akina mama zaidi kuliko wa familia. Wanaume waliamini kazi yao ya msingi ni kuhakikisha familia inapata mahitaji ya kila siku. Suala la malezi liliachwa mikononi mwa akina mama.


Utafiti huu unatusaidia kuelewa changamoto inayotukabili kama jamii. Kwanza, mfumo wetu wa elimu unaonekana kusahau kumjenga mtoto katika maeneo yote ya kimaisha. Lakini pili, inaonekana hakuna uelewa wa pamoja baina ya wazazi na walimu linapokuja suala la maadili kwa watoto. Shule zinasisitiza kufaulu masomo, na wazazi nao wanaendelea na shughuli wanazofikiri ni muhimu. Hali hii ni kikwazo cha jitihda za kujenga maadili. 

Umefika wakati elimu ya maadili si tu iwe sehemu ya mfumo wa elimu bali isisitize mabadiliko ya tabia kuliko uelewa pekee. Kadhalika, jamii nzima ishirikishwe katika juhudi za kuwalea watoto kimaadili badala ya kusubiri kutoa matamko matatizo yanapotokea. 

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Tumia Mbinu Hizi Kuelewa Unachokisoma -3

Haiba ni nini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia