Thamani Yako Inategemea Namna Unavyowasaidia Wengine


PICHA: Lifehack

KUNA ukweli kwamba katika harakati za kutafuta mafanikio, unahitaji kuwa na uhusiano mzuri na aina fulani ya watu. Hawa ni watu wanaokuzidi kile unachotaka kukifanya na kwa namna moja au nyingine wanaweza kuwa msaada kwako kwa kukupa mtaji wa kutekeleza wazo lako, kukunganisha na nafasi za ajira zisizotangazwa hadharani au kukusaidia mawazo yatakayokupeleka mbele kimaisha.

Pamoja na uwezo mzuri wa kufanya vitu, vipaji na elimu, bado unahitaji msaada wa watu wengine kukufikisha kule unakotaka. Hata hivyo, kujenga uhusiano wenye tija na watu unaowahitaji si jambo linalokuja hivi hivi. Unahitaji tabia fulani zitakazowafanya watu wajione wanalo deni la kukusaidia. Usipozielewa tabia hizo, utajikuta katika mazingira ambayo unafahamiana na watu wengi wasiokuchukulia kwa uzito wowote.

Vijana wengi, hasa wanaoanza biashara na pengine wanaotoka kwenye familia zisizo na majina, wanatamani kupata watu wanaoweza kuwa msaada kwao. Wafanye nini ili kujenga mtandao imara na watu wanaoweza kuwa msaada kwao?

Jambo la kwanza ni kuelewa tabia za ubinafsi alizonazo binadamu. Sote kwa namna moja au nyingine tunajali zaidi maslahi yetu binafsi kuliko maslahi ya watu wengine. Hata pale tunapoonekana kuwajali wengine, ndani yetu, inawezekana kuna faida fulani tunayoipata.

Aidha, ubinafsi huo huo ndio unaotufanya binadamu tusipende shida. Hakuna mtu anapenda kuwa kwenye mazingira yanayomwuumiza. Hii ni kweli hata kwenye uhusiano wetu na watu. Kila binadamu hujilinda asijikute kwenye mazingira ya kutumiwa na watu wengine bila faida. Kinachojenga urafiki wa karibu, kwa mfano, ni vile watu wawili wanavyosaidiana kupunguziana shida badala ya kuumizana.

Kwa hivyo, ukitaka kuwa na uhusiano imara na watu, hasa wale wanaokuzidi, epuka kuonekana unawaongezea shida kwenye maisha yao. Usimfanye mtu akajihisi anatumiwa zaidi kuliko anavyopata kwako. Ukifanya kosa hilo utaonekana mzigo.

Kuna mambo mengi unaweza kuyafanya bila wewe kujua na ukaanza kuonekana mzigo kwa watu. Mfano, ni kuwa mtu wa kulalamika. Unapolalamika maana yake huna majibu ya matatizo unayoyaongelea. Watu waliofanikiwa, hawapendi kusikia mtu anayetumia nguvu nyingi kuongelea shida badala ya ufumbuzi.

Pia, unapokuwa na tabia ya kutaka kupata misaada na vitu kwa watu kuliko vile unavyochangia kutatua changamoto zao, watu hawatatamani kukutana na wewe. Sababu ni kwamba wanapokuona hawakuoni wewe, bali wanaona mzigo. Hakuna mtu anapenda mizigo.

Kwa bahati mbaya, binadamu huwa tunavutia watu wanaofanana na sisi. Kwa mfano, unapokuwa na uso wenye tabasamu, ni rahisi watu unaokutana nao kukuonesha tabasamu. Unapokasirika, unawafanya wanaokuzunguka wakasirike pia. Ndivyo ilivyo hata kwenye mambo mengine. Unapoonekana huna mwelekeo, utawavutia watu wasio na mwelekeo. Ukiwa mzigo, utavutia mizigo mingine. Wale unaotamani wakusaidie, watakukimbia.

Ukitaka kuaminiwa na watu wa muhimu wanaokuzidi, unahitaji kuanza kuwa tofauti kwa lugha na matendo yako. Kwanza, onekana kama mtu wa maana kwa mavazi, lugha yako, na mwenendo wako. Ni habati mbaya binadamu tunapokutana na watu wapya, tuna tabia ya kukadiria thamani zao kwa kutumia vigezo vinavyoonekana.  Hakikisha unaonekana mtu nadhimu, timamu, anayeaminika.

Pili, jitahidi uwe na kitu unachoweza kuwapa watu badala ya kusubiri ufanyiwe. Kwa mfano, unapoongea na watu wa muhimu, wape nafasi wakuambie mambo yao zaidi kuliko unavyowaeleza mambo yako. Watu wenye hadhi ya juu wanapenda kufahamika kwamba wanaheshimika. Wape nafasi hiyo.

Kadhalika, usiwe na haraka ya kutaka misaada. Kila inapowezekana, onesha namna unavyoweza kutumia kile ulichonacho kuwa jibu la matatizo ya watu.

Thamani yako ni vile vitu unavyoweza kuwapa watu. Uwezo ulionao wa kutatua matatizo yanayowakabili watu wanaokuzunguka. Thamani yako ni ujuzi ulionao, maarifa na busara ambayo watu wengine wanaweza kunufaika nayo.

Ikiwa unataka watu wavutwe kwako, jenga thamani yako. Fikiria namna unavyoweza kuwasaidia kufikia malengo yao. Kukosa fedha na raslimali kusikufanye ushindwe kuwa na thamani. Wasaidie watu kupata ufumbuzi wa matatizo yao. Kufanya hivyo kutaongeza thamani yako. Na kadri thamani yako inavyoongezeka, ndivyo watu watakavyokuheshimu na kukuona kama mtu wa maana. 

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Pay $900? I quit blogging

Haiba ni nini?

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Heri ya mwezi mpya!