Wanavyokufahamu Watu Ndivyo Ulivyo?

PICHA: NCCPE


‘Jamaa ana madharau sana!’ alilalamika Lazaro.
‘Nani?’ alihoji Msafiri.
‘Si Peter?’
Uso wa Msafiri ulionesha mshangao. Hakufikiri Peter anaweza kuwa na dharau kama Lazaro anavyodai. Msafiri anamfahamu Peter mwenye tabia nyingine kabisa. Kwake, Peter ni rafiki,  mtu wa watu asiye na neno na mtu.
‘Peter huyu huyu ninayemfahamu mimi?’ Msafiri aliwaza kimya kimya akikumbuka namna Peter alivyomsaidia hivi majuzi alipokuwa na shida ya fedha. Hakuna rafiki aliyemsaidia isipokuwa Peter.

Hakupata kufikiri hata mara moja kwamba Peter angeweza kuwa dharau akaona aulize imekuwaje, ‘Kwa nini umefikiri hivyo Lazaro?’
‘Jamaa ana kiburi sana aisee. Nimepishana nae mjini kati jamaa kama hanifahamu vile. Na kile ki Vitz chake yaani kama hanioni vile!’
‘Labda hakukuona mkuu. Peter hayuko hivyo.’
‘Hapana alikuwa ananiangalia kabisa. Kaudhi sana jamaa. Tangu awe na hicho kigari kabadilika mbaya. Kijiweni haji tena. Anajifanya yuko busy.’

Msafiri haamini anachokisikia kwa Lazaro anayeonekana kuufahamu upande wa pili wa Peter. Je, nani kati ya Lazaro na anamfahamu Peter? Kwa nini Peter afahamike kwa sura zaidi ya moja?

Kubadilika badilika kwa tabia

Kwa nyakati tofauti, katika shughuli zako za kila siku, nawe kama Peter, unaweza kuwa na sura zaidi ya moja. Sura yako inabadilika badilika kulingana na mazingira uliyopo.

Unapokuwa nyumbani, kwa mfano, unaweza kuwa na sura ya baba mkali asiye na muda wa kumsikiliza yeyote. Watoto na mama yao, wanakuona kama mtu mkorofi, asiyejali majukumu yake kama mume na baba.

Lakini unapokuwa kazini, unavaa sura ya kazi na kugeuka kuwa mchapakazi hodari, mkali kidogo lakini anayefuatilia mambo kwa karibu. Wafanyakazi wenzako, tofauti na familia yako, wanakuona kama mtu mwenye bidii ya kazi, mwenye msimamo thabiti lakini mpenda watu.

Kanisani, pengine wanaokuona kama mtu asiye na bidii na mambo ya dini, mzembe, lakini mwenye upendo kwa waumini wenye shida. Kila wakati panapokuwa na uhitaji, unakuwa mwepesi kutoa msaada kwa fedha zako. Kwa namna hiyo, umejijengea taswira ya mtu mwadilifu mwenye upendo ingawa hapatikani kirahisi.

Kubadilika kunakidhi mahitaji yetu

Tabia zetu zinabadilika badilika kukidhi mahitaji ya mazingira tunayokuwemo. Watu wanaotuzunguka wanakuwa na matarajio fulani kwetu. Namna tunavyojiweka mbele zao, ni muhimu.

Chukulia umekutana na mtu unayejua atakayekusaidia kesho. Kwa kuwa unajua atasaidia kesho, msukumo wa kuwa mnyenyekevu unakuwa mkubwa.  Utaongea kwa lugha ya kistaarabu na uungwana ukijaribu kujenga sura ya mtu anayestahili kusaidiwa. Lakini unapokuwa na mtu unayejua hana hadhi wala msaada wowote kwako, ni rahisi kuonesha dharau.

Peter alifanya kitu kilichoonesha dharau kwa Lazaro, kwa sababu pengine, Lazaro hakuwa na msaada kwa Peter. Inawezekana kwenye macho ya Peter, hawa jamaa wawili Lazaro na Msafiri wana hadhi mbili tofauti. Pengine Peter alimhitaji zaidi Msafiri na hivyo akawa mwema zaidi kwake kuliko ilivyokuwa kwa Lazaro asiyemhitaji.

Tumeona kuwa tunachokifanya kwa watu kinategemea na mahitaji na matarajio yetu kwao. Kwa sababu hiyo, ni vigumu sana kufikiri unamfahamu mtu kwa sababu huwezi kujua kwa nini alifanya kile ulichokiona. Mtu anaweza kukusaidia, mathalani, kwa sababu anajua kesho na keshokutwa utamsaidia. Ikiwa atafahamu hutakuwa na msaada kwake, hawezi kukusaidia.

Tumewaona matajiri wanaotoa misaada mingi hadharani lakini hawako tayari kusaidia watu wanaowafuata kwa faragha. Watu hawa wanapotoa misaada, ni dhahiri lengo ni kujipatia heshima kwa jamii na sio kuwasaidia wanaopokea misaada hiyo.

Unawezaje kumfahamu mtu?

Hapa kuna mambo mawili ya kuzingatia. Kwanza, ni namna anavyowatendea watu anaojua fika kwamba hawana msaada wowote kwake. Kwa mfano, mwalimu anapozungumza kwa heshima na Mkuu wa Shule au Ofisa Elimu, hatuwezi kusema hiyo ndiyo tabia yake. Wema, unyenyekevu kwa mtu anayekuzidi si kipimo cha utu wako. Utu wa mwalimu huyu unaonekana pale anapokuwa na uwezo wa kuzungumza kwa heshima na unyenyekevu kwa mwanafunzi wake. Katika mazingira yake hiyo inakuwa ndiyo tabia yake kwa sababu hana maslahi anayoyatafuta kwa mwanafunzi wake.


Lakini pia, namna gani mtu habadiliki badiliki kulingana na mazingira, hiyo pia inaweza kuonesha kiwango chake cha kujitambua. Tabia tunazozionesha  hadharani zinapokwenda sambamba na yale tunayoyafanya tukiwa faragharani maana yake ndivyo tulivyo.  

Tabia yako unapokuwa kazini, inapooana na tabia yako ukiwa nyumbani au kwingineko kokote,  uwezekano ni mkubwa kwamba hivyo ndivyo ulivyo. Lakini unapobadili tabia kulingana na matakwa ya mazingira na watu wanaokuzunguka, uwezekano ni mkubwa kwamba tabia hiyo haianzii ndani yako. Ni namna fulani ya maigizo.

Maoni

  1. kazi nzuri sana ndugu Christian Bwaya. Post zako ni zaidi ya darasa. Najifunza mengi sana kupitia Jielewe blog . Ningependa kukukaribisha kutembelea blog yetu ya 90 Newz blog kwa elimu,buruani na habari za kila siku , pia kama utahitaji kupata muonekano mzuri na wa kisasa wa blog yako, wasiliana nasi kwa namba zilizopo ndani ya blog yetu. Ahsante

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Pay $900? I quit blogging

Heri ya mwezi mpya!