Hatua za Kuchukua Unapojisikia Kuchoka Kazi




Kutokuridhika na kazi ni hali ya kujisikia hufikii matarajio yako kikazi. Matarajio yanaweza kuwa kiwango cha mshahara, kujisikia unafanya kazi ndogo kuliko uwezo ulionao, kazi kutokuendana na vipaji ulivyonavyo au hata kutokupata heshima uliyoitarajia.

 Kila mtu kwa wakati fulani hujisikia kutokuridhika. Kuna sababu kadhaa. Moja, ni kuwa na matarajio makubwa kuliko uhalisia wa kazi. Lakini la pili, kujilinganisha na watu wasiolingana na kazi unayoifanya. Unapoona wenzako wanafanya kitu tofauti na kile unachokifanya wewe inawezekana ukajisikia kuachwa nyuma hata kama kimsingi pengine unafanya vizuri.

Vyovyote iwavyo, zipo nyakati unaweza kujikuta huridhiki na kazi unayoifanya. Makala haya yanaangazia vichocheo vinne vya kuchoka kazi na hatua za kuchukua unapojikuta katika hali kama hiyo.
Huridhiki na mshahara
Ulipokuwa mwanafunzi uliota ndoto za kufanya kazi yenye mshahara mnono. Uliamini maisha yako yangebadilika ndani ya muda mfupi. Baada ya kupata kazi, unashangaa mambo ni kinyume. Unacholipwa hakilingani na matarajio yako.
Hapa sababu inaweza kuwa kukosa subira. Hakuna mafanikio yanayokuja kwa njia ya mkato kama vijana wa siku hizi wanavyoamini. Mafanikio katika mazingira ya kazi yanafuata hatua fulani. Unahitaji kuwa mvumilivu.
Lakini vile vile huenda kuna maslahi usiyoyaoona. Hata kama mshahara ni mdogo, pengine mwajiri wako anakupa usafiri kwenda na kurudi kazini; amekulipia nyumba; amekuweka mpango wa bima ya afya; anahakikisha unapata chakula cha mchana ukiwa kazini.
Mbali na mshahara huo mdogo, labda mwajiri anakupa fursa ya kwenda masomoni na pia unapata muda wa ziada kufanya mambo mengine. Haya yote unaweza kuona ni madogo lakini ukiyabadilisha kuwa fedha yanaweza kuwa nusu ya mshahara unaoutamani.
Ujuzi wako hautumiki
Moja wapo ya mambo yanayopunguza ari ya kazi ni kujisikia ujuzi ulionao hautumiki ipasavyo. Unalipwa vizuri lakini moyo wako hauridhiki na kazi unayofanya.
Labda una Shahada ya Biashara na Masoko, lakini majukumu yako ya kila siku ni yale yale na hayakupi changamoto. Kazi yako ni kupokea barua za wateja na kuzigonga muhuri. Unaichukulia hali hii kama udumavu na unatamani ungefanya kazi inayokupa changamoto.
Katika hili unahitaji kutafuta fursa nyingine za kutumia ujuzi wako kazini. Pengine kampuni ina shughuli nyingi za ziada ambazo ukiweza kuwa tayari unaweza kuzifanya.
Vipi kama ukianzisha wazo la chama cha akiba na kukopa? Kazi hiyo inaweza kukufanya ukatumia muda wako wa ziada kutumia maarifa yako ya Biashara na ukajisikia kuridhika.
Kadhalika, unaweza kuamua kufanya kazi nyingine za ziada zisizoathiri utendaji wako. Kuna fursa nyingi za ujasiriamali zisizokulazimu kuacha kazi na zikakufanya utumie vizuri zaidi ujuzi ulionao.
Lakini pia kuna suala la uzoefu. Unaweza kuamua kuwa mvumilivu ukaweza kupanda ngazi hapo kazini. Kubadilisha kazi kila baada ya muda mfupi, kunakufanya uendelee kuwa mtu asiyeweza kuaminiwa kwa nafasi za uandamizi.
Huoni fursa ya kukua
Umefanya kazi kwa miaka mitano kwenye kampuni kubwa inayokulipa vizuri lakini hujioni ukikua kiujuzi. Huwezi kwenda masomoni ukiwa kazini na pengine kampuni haina mpango wa kukusaidia kujiendeleza kiujuzi. Hali hii imekufanya ujisikie kuchoka, unajisikia kudumaa na huna hamasa tena ya kufanya kazi. Ufanyeje?
Tafakari kitu gani hasa kilikufanya ukapenda kazi unayoifanya hivi sasa. Kitu gani kilikuwa kinakuvutia kwenda kazini mwanzoni mwa ajira yako? Nini kimebadilika leo?
Unapokuwa katika mazingira kama haya ni rahisi kumlaumu mwajiri wako. Kumbuka mwajiri halazimiki kufikiri namna ya kukuendeleza na kukupa hamasa ya kujiendeleza. Hiyo ni kazi yako.
Kwa kuwa fursa ya kujiendeleza kimasomo mbali na ofisini haipo, fikiria kujiunga na masomo ya masafa. Jiandikishe kufanya masomo yako kwa njia ya mtandao; jiunge na vyuo vya karibu vinavyotoa masomo ya jioni au mwisho wa juma. Kwa namna hiyo unaweza kuendelea na kazi huku ukikuza ujuzi wako.
Kadhalika, jenga utamaduni wa kujisomea vitabu vinavyoendana na fani yako. Maarifa yanabadilika kwa kasi. Vijana wa leo wanaoingia kwenye ajira wanajua mambo mengi ambayo pengine wewe mkongwe hukujifunza. Usiposoma utaachwa nyuma na utendaji wako unaweza kuanza kupwaya.
Una ndoto za kazi nyingine
Inawezakana kazi unayoifanya leo hailingani na masomo uliyosomea. Ulikuwa na ndoto za kuwa mwanasheria lakini mazingira yalikulazimu kusomea Sayansi ya Siasa. Ingawa unafanya kazi kwa sasa, lakini moyo wako bado uko kwenye sheria.
Jambo la kukumbuka hapa ni kwamba si wakati wote tunapata kile tunachopanga. Si mara zote watu hufanya kazi zinazolingana na fani walizosomea. Unaweza kusomea Sayansi ya Siasa ukajikuta ukifanya kazi ya Ofisa Raslimali Watu. Unaweza kusomea Biashara na Masoko ukajikuta unafanya kazi ya Ualimu. Mambo hubadilika.
Ukweli ni kwamba elimu ya chuo hutupa maarifa ya jumla yanayoweza kutumika kwenye eneo zaidi ya moja. Mwalimu, kwa mfano, anajifunza utawala, siasa, mipango, uandishi wa miradi na maarifa mengine anayoweza kuyatumia kwenye eneo tofauti na Ualimu.
Mbali na maarifa na ujuzi mahususi, miaka unayotumia darasani inakufundisha ujuzi wa ziada ambao hatuufanyii mtihani. Mfano, namna ya kuwasiliana na watu, kutatua migogoro na watu msioelewana, uandishi wa nyaraka, nidhamu ya muda na ujuzi mwingine mwepesi.
Kila tunachokisoma kinatunufaisha kwa namna moja au nyingine. Hakuna ujuzi usio na maana yoyote hata kama huoni ukiutumia moja kwa moja. Pengine ni wakati wa kukubali kuwa mambo yamebadilika. Ulichotaka kukifanya sicho unachokifanya. Ndivyo maisha yalivyo.   

Hata hivyo, kama umejaribu kukuza ujuzi wako; umejiendeleza ukiwa kazini; umefanya jitihada za kujiongezea kipato na bado huridhiki na mazingira ya kazi, pengine ni wakati wa kujaribu kwingine. 

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia

Uislamu ulianza lini?