Mabadiliko ya Kijamii Yanavyoathiri Malezi -1

PICHA: The Conversation


TUNAISHI katika nyakati ambazo maarifa kuhusu malezi ya watoto vinapewa umuhimu. Sambamba na ongezeko la mijadala ya malezi katika majukwaa mbalimbali, malezi yamevutia hisia za watafiti wengi kuliko ilivyopata kuwa. Kila siku, kwa mfano, zinachapishwa tafiti nyingi kuchunguza changamoto za malezi ya watoto.

 Jambo hili linaweza kumtia wasiwasi mfuatiliaji makini wa mambo. Unaweza kuhoji, ‘Kulikoni msisitizo huu mkubwa katika malezi?’ ‘Mbona wazazi wetu hawakuelimishwa namna ya kulea na hawakushindwa kutulea vizuri?’

‘Kwa nini pamoja na kuwepo kwa kila namna ya maarifa ya kimalezi kwa wazazi wa kisasa bado tumeendelea kushuhudia kuporomoka kwa maadili kwa watoto wetu?’ Maswali haya ni ya msingi na hayawezi kuwa na majibu mepesi.

Hata hivyo, lililo dhahiri ni kwamba jamii yetu inapitia mabadiliko makubwa ya kijamii yanayoathiri mfumo uliozoeleka wa malezi. Tutazame mabadiliko kadhaa na namna yanavyodai gharama kwenye eneo la malezi.

Wazazi kutokuishi pamoja

Tunaishi kwenye nyakati za mabadiliko makubwa ya mfumo wa maisha.  Mtindo wa maisha tunayoishi hivi leo unaathiri kwa kiasi kikubwa namna tunavyolea watoto wetu. Kwa mfano, siku hizi ni jambo la kawaida kwa wazazi kutumia muda mrefu mbali na familia zao. Kazi zinachukua muda mrefu wa wazazi kuliko ilivyopata kuwa hapo zamani.

Wakati zamani katika familia nyingi za kawaida baba na mama waliishi sehemu moja, siku za leo ni kawaida, kwa mfano, kusikia mume anaishi Dar es Salaam, wakati mama anafanya kazi mkoani Singida.

Katika mazingira haya, wazazi hawa wanaweza kukutana kwa nadra na hata kuchukua miezi kadhaa kabla mzazi mmoja hajapata muda wa kwenda kusalimia familia yake inayoishi mbali nae. Jambo hili halikuwahi kuwa sehemu ya maisha ya familia katika siku za nyuma.

Kadhalika, ndoa nazo zimekuwa na mitikisiko kuliko ilivyokuwa zamani. Misukosuko ya ndoa inafanya watoto ama waishi na mzazi mmoja au wazazi wawili wasioelewana.

Ajira kwa wanawake

Siku za nyuma mama alikuwa ndiye mlezi mkuu. Katika familia nyingi za kawaida, wanawake walioolewa waliitwa  ‘mama wa nyumbani.’ Kazi yao kubwa ilikuwa kubaki nyumbani muda mwingi kulea watoto. Wanawake wengi, kwa kawaida, hawakuwa na kazi nyingine zaidi ya kuwatunza watoto.

Kazi ya kutafuta kipato iliachwa kwa wanaume. Watoto walilelewa kwa karibu sana na mama tangu wakiwa wadogo mpaka walipofikia umri wa kuondoka nyumbani na kujitegemea. Hapakuwa na changamoto ya nani abaki nyumbani kuwaangalia watoto.

Mambo yamebadilika hii leo. Akina mama wameondoka nyumbani kuungana na wanaume kuongeza kipato cha familia. Dhana kuwa mwanamke ni ‘mama wa nyumbani’ inafutika. Akina mama wanafanya ujasiriamali, wanajihusisha na shughuli ambazo hapo zamani zilionekana kama haki ya wanaume.

Mwanamke kufanya kazi, kwa hakika si jambo baya. Jitihada za kuwasomesha watoto wa kike zinaenda sambamba na fursa ya kiajira sawa na mwanaume. Ndio kusema, kama mwanaume anaweza kuajiriwa, haileti maana kufikiri kuwa mwanamke anapaswa kubaki nyumbani kufanya kazi za ndani kama ilivyokuwa imezoeleka hapo zamani.

Katika ajira wanawake wameonesha uwezo wa kumudu majukumu yao sawa na wanaume. Karibu kila sekta hivi sasa wapo akina mama. Wanawake wanaonesha uwezo mkubwa. Wanashika madaraka makubwa makazini na wanafanya vyema, tena mara nyingine, kuliko wanaume.

Hata hivyo, mafanikio haya ya akina mama kikazi yametikisa maeneo mengineyo ya kijamii. Malezi ni eneo moja wapo kubwa lililokumbwa na tetemeko kubwa tangu akina mama walipoanza kuondoka nyumbani kuelekea makazini.

Kufifia kwa familia tandaa

Katika baadhi ya makabila, mwanamke ndiye aliyekuwa na jukumu la kuitunza familia. Ingawa mwanamke hakuwa na ajira rasmi, bado alitarajiwa kujituma katika shughuli zinazoingiza kipato cha familia. Mwanamke alishinda shambani akilima na pia alitafuta soko la mazao ya kilimo ili aweze kuilisha familia.

Hata hivyo, shughuli hizi za mwanamke hazikuathiri wajibu wake mkuu wa malezi. Kulikuwa na familia tandaa, ndugu wa ukoo, waliomsaidia kufanya majukumu ya nyumbani wakati yeye akiendelea na shughuli zake nyingine mbali na nyumbani.

Wakati mama akisafiri kwenda kuuza mazao mjini, kwa mfano, nyumbani walibaki ndugu waliomwangalia mtoto. Mama hakuwa na wasiwasi na usalama wa mtoto kwa sababu alijua amemwacha mtoto wa baba mkubwa, binamu au shangazi waliomjali mtoto wake kama ndugu.

Haya mawili, yalifanya suala la malezi kuwa jambo lisilo na changamoto kubwa. Kwamba baba akiwa kazini, mama alikuwepo nyumbani. Ikitokea mama naye anawajibika kufanya kazi nje na nyumbani, ilikuwepo familia tandaa kuhakikisha mtoto analelewa ipasavyo. Hata hivyo, ukaribu huu wa familia tandaa unaendelea kufifia. Kwa sababu kadhaa, imeanza kuwa nadra kuishi na watoto wa ndugu.

Upatikanaji holela wa taarifa

Ninakumbuka mara ya kwanza kuangalia televisheni. Wakati nakua, hatukuwa na fursa ya kutazama vipindi vya televisheni zaidi ya maigizo ya kwenye Radio Tanzania. Mambo ya mtandao wa intaneti hayakuwepo. Kwa vijana wadogo waliopenda ‘udaku’ yalikuwepo magazeti ambayo hata hivyo yaliishia kuchekesha. Hapakuwa na magazeti yanayoanika taarifa ambazo zingeleta usumbufu kwa vijana ambao umri wao ulikuwa bado.

Katika mazingira kama haya, mzazi hakulazimika kuzungumzia mambo fulani fulani kwa vijana wanaobalehe. Hapakuwa na shinikizo kubwa la mzazi kuwa karibu na kijana wake kuratibu taarifa zisizostahili. Mambo mengi yalifahamika katika umri husika tofauti na ilivyo sasa.

Sasa hivi mtoto mdogo anayejua kusoma na kuandika anaweza kuwa ‘Facebook’, ‘Whatsapp’ bila mzazi wake kujua. Humo, mtoto anaweza kukutana na taarifa zinazomzidi umri. Upatikanaji holela wa taarifa umeibua changamoto mpya ya malezi kwa wazazi wachanga. Katika mazingira yenye mchanganyiko wa changamoto kama hizi, wazazi wanatumia muda mwingi kupanda ngazi za mafanikio wakiamini watoto wako salama.


INAENDELEA

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Tumia Mbinu Hizi Kuelewa Unachokisoma -3

Haiba ni nini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia