Unavyoweza Kukuza Tabia Njema kwa Mwanao -4

Katika makala yaliyopita tumejifunza aina mbili za misukumo ya utovu wa nidhamu. Kwanza, tumeona mtoto huweza hufanya ukorofi kutafuta kusikilizwa. Anaposumbua na hata kudeka bila sababu, mara nyingi, anajaribu kutuambia kuwa hatujampa muda wa kuwa karibu naye. Anafanya hivyo kutafuta usikivu wetu.

Pia, tumeona wakati mwingine mtoto husukumwa na hisia za kutaka kulipiza kisasi. Kama ilivyo kwa mtu mzima, mtoto naye anazo hisia. Anaweza kuumizwa na kauli na matendo anayoyatafsiri vibaya. Jitihada za kupunguza maumivu yake huishia kuwaumiza na wengine.

Namna gani tunawasaidia watoto kuondoa tafsiri hizi potofu, huamua aina ya tabia watakazojifunza. Katika makala haya tunaangazia malengo mengine mawili yanayotengeneza msukumo wa kukosa nidhamu.


PICHA: NUBI Magazine
Kutafuta ushawishi asionao

Richard mwenye miaka nane hana adabu nyumbani. Hasikii anachoambiwa na yeyote isipokuwa anapotishiwa kwa kiboko. Juzi ameonywa na baba yake aache tabia ya kuzurura mitaani. Aliitikia, lakini leo pia ameendelea kuzurura.

Muda mwingi anagombana na mdogo wake. Ni mlalamishi na mara nyingi humshtaki mdogo wake kwa wazazi.

Anapokuwa shuleni, Richard ana sura tofauti. Nidhamu yake ni ya hali ya juu kwa walimu na wenzake. Ni vigumu kuamini Richard huyu anayeshindana na wazazi wake nyumbani ni mnyenyekevu na msikivu anapokuwa suleni. Kitu gani kinamfanya Richard awe mtukutu anapokuwa nyumbani?

Richard anajiona kama mtu asiye na ushawishi kwenye familia yake. Ujeuri anaojaribu kuufanya unamsaidia kufidia hali ya kukosa ushawishi anayojisikia ndani yake. Anafikiri kwa kujaribu kushindana na wazazi kunamhakikishia ushawishi anaohisi hanao.

Kwa kawaida, watoto kama walivyo watu wazima wanahitaji kuwa na mamlaka. Mamlaka ni ushawishi anaokuwa nao wa kusababisha kitu kikafanyika. Watoto wanapopewa fursa (inayolingana na umri wao) ya kujisikia kuwa wana ushawishi kwenye familia wanajiona wana mamlaka. Mfano, shughuli kama kuongoza ibada, kuombea chakula, kupanga ratiba zao kwa msaada wa wazazi zinawajengea imani kuwa wana mamlaka.

Richard anafanya vituko kwenye familia kwa sababu amekosa imani hiyo. Anagombana na mdogo wake mara kwa mara kwa sababu anahisi ndiye mwenye ushawishi. Maneno kama, ‘Unakoseaje wakati wewe ni mkubwa kuliko mwenzako? Acha ujinga’ yanamnyang’anya mamlaka anayodhani anayo.

Mtoto anayejihisi hana mamlaka ni mgomvi, hukejeli wengine, huwa na madai mengi, hulazimisha ukubwa kwa wengine. Vile vile, ana tabia ya kukubaliana na maagizo lakini hafanyi; mbishi na mkaidi; si msikivu na wakati mwingine huwa na dharau kwa watu wanaomzidi.

Kimsingi, anafanya yote hayo kwa lengo la kumnyong’onyeza mtu mwingine mwenye mamlaka kwake ili kumfanya ajione ‘hawezi kumfanya kitu.’ Kumtawala mtoto kupita kiasi kunaweza kuzaa hali hii. Unaposhindwa kumpa nafasi ya kutumia utashi wake, mathalani kuamua wapi akacheze, unamnyang’anya imani kuwa ana ushawishi kwenye familia.

Hali hii huzaa mashindano ya chini chini kati ya mzazi na mtoto. Mzazi anaogopa kumpa mtoto nguvu ya kufanya chochote. Mtoto naye anatamani kuwa na sauti angalau kwa mambo yanayomhusu. Anapokosa sauti, mtoto anajenga upinzani.  Mtoto wa namna hii anayejisikia kubanwa, hufika mahali pa kutishia mamlaka yako kwa kukataa kufanya unachomwagiza.

Kumwadhibu mtoto anayetishia mamlaka ya mzazi ni kuendeleza tatizo. Namna nzuri ya kumsaidia mtoto wa namna hii ni kumfanya ajisikie mshindi. Kukiri makosa yako kunaweza kurudisha imani yake kwako. Hili, hata hivyo, si jambo rahisi.

Kwa wazazi wengi, kukiri kosa ni sawa na kujidhalilisha. Wanafikiri mtoto akijua umekosea, atajenga kiburi. Matokeo yake wanaendelea kushindana kwa kutoa adhabu ambazo kimsingi zinaongeza uadui. Wakati mwingine jibu ni kuwa tayari kushuka chini na kuachia kiasi cha mamlaka yako.

Kujiona hawezi

Tunazaliwa na hitaji la kujiona tunaweza. Ili mtu ajisikie anaweza, lazima kwanza aweze. Anapoweza kufanya kitu kwa mafanikio, anajenga hali ya kujiamini. Mtu anayejiamini anakuwa tayari kujaribu kufanya vitu vipya bila wasiwasi wa kushindwa.

Watoto wanaoamini hawawezi mara nyingi wanakuwa na wasiwasi na uwezo wao. Mazingira ya kimalezi yamewakatisha tamaa. Ndani yao inatoka sauti inayonyong’oneza, ‘Unaweza kufanya nini mtu kama wewe? Huwezi chochote!’

Mtoto wa namna hii huonyesha alivyokata tamaa kwa namna mbali mbali. Anaweza kujitenga na wenzake; hayuko tayari kujaribu chochote na wakati mwingine huwa na tabia ya kujitamkia maneno yenye kuthibitisha kuwa yeye ni mtu dhaifu.

Tutumie mfano wa Bakari mtoto wa miaka tisa. Bakari hapendi kufanya vitu bila kuambiwa. Mara nyingi ataamka na hakumbuki kupiga hata mswaki mpaka aambiwe. Akila ataacha vyombo pale pale mpaka mama amkumbushe kuviondoa. Kwa umri wake ungetegemea akiamka ajiandae aende shule. Lakini hata kuamka ni mpaka awepo mtu wa kumkumbusha. Kwenda shule ni ugomvi kwa sababu hataki kuachana na wazazi. Ukimwangalia kwa haraka, unaweza kusema ni mvivu na goigoi.

Ukiwauliza wazazi wake, wanakwambia wanampenda sana. Muda mwingi wako naye na hawamwachi. Mama yake anajitahidi kumfanyia karibu kila kitu. Anamfungia kamba za viatu, anamchania nywele na kila kitu. Saa ya kufanya kazi za nyumbani anazopewa shuleni, mama na baba watashindana kumsaidia hesabu zote.

Wazazi wanafanya yote hayo kwa nia njema. Wanampenda Bakari. Wana matarajio makubwa kwake na wanajitahidi kuhakikisha kuwa mwanao hapati shida.

Mara chache ambazo Bakari anajaribu kufanya kitu, wazazi wanakuwa wepesi kugundua makosa. Bakari anapokuja na alama 70, mama na baba watakuja juu. Wanahitaji kuona 95 kwenye mtihani ujao.

Bakari amejikuta akijenga fikra potofu kuwa hawezi. Ingawa wapo watoto wengine ukiwaambia hawawezi ndio kwanza wanajenga hamasa ya kukuthibitishia kuwa wanaweza, kwa Bakari hali ni tofauti. Matarajio makubwa ya wazazi ambayo katika hali halisi hayafikiki, yanamfanya ajihami kwa kutokujaribu. Bakari hasaidiwi kwa kusimangwa. Msaada anaouhitaji ni kutiwa moyo kuwa anaweza.

Kwa ushauri elekezi kwa masuala ya malezi na makuzi niandikie: christianbwaya@gmail.com, 0754-870-815


Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia