Tunayopaswa Kuyafahamu Kuhusu Shule za Msingi za Bweni -2

Tulianza kujadili namna gani mazingira ya shule za bweni yanavyochangia kuwasaidia watoto wadogo kuimarika kiakili. Bonyeza hapa kama hukusoma makala hiyo. Tuliona shule za bweni zinaweka mazingira sisimushi yanayowajenga watoto kiufahamu zaidi kuliko wenzao wanaoishi nyumbani.

Mambo kadhaa yanaonekana kuchangia kukuza uwezo huu. Kwanza, tulitaja uwepo wa ratiba inayoongoza mtiririko wa shughuli za watoto wanapokuwa katika mazingira ya shule.

Mtiririko huu haukuonekana kwa watoto wa kutwa. Kwa mfano, watoto wa kutwa kwa kiasi kikubwa hawakuonekana kuwa na uhakika wa nini wanakifanya baada ya saa za shule. 

Tafsiri yake ni kuwa wazazi hawawezi mazingira yanayomsaidia kujua anafanye nini wakati gani. Kutokutabirika kwa ratiba kunaongeza uwezekano wa mtoto kufanya mambo yasiyomsaidia kitaaluma. Kwa mukhtadha huu, shule za bweni zinampa mtoto faida isiyopatikana nyumbani.

PICHA: unilever.com

Uangalizi unaoaminika

Uangalizi katika shule za bweni ulikuwa mzuri ukilinganisha na mazingira ya nyumbani. Uangalizi, katika mukhtadha huu, ni uwepo wa walezi wanaoaminika wanaohakikisha kuwa mtoto anapata mahitaji yake ya msingi kwa kipindi chote awapo shuleni.

Kwa upande mwingine, mazingira ya nyumbani yalikuwa na upungufu wa uangalizi. Wazazi hawakuonekana kupatikana vya kutosha na wakati mwingine walichelewa kufika nyumbani. Matokeo yake watoto waliangaliwa na watu wengine waliopatikana katika mazingira ya nyumbani au karibu na nyumbani.

Kutokuwepo kwa uhakika wa ungalizi nyumbani, kulilazimisha watoto wakati mwingine kuwa chini ya uangalizi wa watu wasio na mamlaka. Kukosekana kwa watu wenye sauti ya kutosha kuwaonya, kuliwaweka watoto kwenye hatari ya kufanya chochote warudipo nyumbani.

Mazingira ya kujifunzia

Aidha, shule za bweni zilionekana kuweka mazingira bora ya kujifunzia kwa watoto. Hapa tunazungumzia upatikanaji wa watu wazima wenye uelewa zaidi na utayari wa kuwapa watoto msaada wa kitaaluma uliohitajika baada ya saa za masomo.

Wakati watoto wa nyumbani waliweza kufanya shughuli zisizo za maudhui ya kitaaluma baada ya masomo kama vile kutazama televisheni na michezo isiyopangiliwa, wenzao wa bweni hawakuwa na nafasi ya kufanya shughuli zisizo na uhusiano na masomo.

Utaratibu wa shughuli za nje

Kadhalika, shule za bweni zilikuwa na utaratibu wa kuwaajiri wafanyakazi maalumu wenye wajibu wa kufanya shughuli za nje ya darasa kwa niaba ya watoto. Kazi ndogo ndogo kama kufanya usafi wa mazingira, kusafisha vyombo vya chakula, vyumba vya kulala na kufua nguo za watoto zilifanywa na wafanyakazi.

Watoto karibu wote walisema wanasaidiwa kufua nguo, kuogeshwa, kupiga mswaki, kutandika kitanda na hata kufanya usafi wao binafsi. Ingawa utaratibu huu ulionekana kudumaza uwezo wao wa kujitegemea kama tutakavyoona mbeleni, bado ulimsaidia mtoto kuelekeza jitihada kwenye masomo. Hata hivyo, ni dhahiri shule zilifanya hivyo kukidhi matakwa ya wazazi.

Mazingira ya nyumbani, kwa upande mwingine, yalimshirikisha mtoto kwenye shughuli nyingi za nyumbani. Mtoto wa kutwa, kwa mfano, alitumwa dukani, alifanya usafi wake binafsi kwa msaada wa watu wazima na alifanya kazi ndogo ndogo kulingana na mazingira yake.

Pamoja na faida ya mtoto kushiriki shughuli hizi, hata hivyo ni dhahiri zilichukua muda ambao ungeweza kutumiwa kwa shughuli za kimasomo.
Izingatiwe kuwa ulinganisho huu ulifanywa kwa kutumia watoto wa shule ile ile ingawa walitengwa kwenye makundi ya kutwa na bweni kuwezesha kufanya ulinganisho kwa ufasaha.

Dhana ya kujitegemea

Kujitegemea ni ujuzi wa kufanya shughuli zinazolingana na uwezo wa mtoto bila kuhitaji msaada mkubwa wa watu wazima. Kwa mfano, mtoto anapoweza kupiga mswaki bila kutegemea usaidizi wa watu wanaomzunguka, tunaweza kusema, hapo anajifunza kujitegemea.

Kinyume chake ni mtoto kushindwa kuwa na ujuzi wa kufanya vitu vingi vinavyomwezesha kumudu mazingira yake. Hapa tunazungumzia kujiogesha, kujipaka mafuta, kuosha vyombo, kufua nguo, kuvaa viatu, kufunga kamba za viatu na stadi nyingine za kila siku.

Aidha, kujitegemea kunakwenda sambamba na uwezo wa mtoto kumudu viungo vya mwili wake kumwezesha kufanya kile anachotaka kukifanya kwa muda muafaka. Kwa mfano, mtoto mdogo anapojifunza ni muda gani anaweza kujisaidia kulingana na mahitaji ya mazingira alimo, hapo tunasema, mtoto ameanza kujitegemea.

Kujitegemea, kimsingi kunajegwa na kuimarishwa na mazingira ya kimakuzi. Mlezi au mzazi anahitaji kujenga mazingira sisimushi yanayomjengea mtoto uwezo wa kujiamini na kufanya vitu vinavyolingana na umri wake.

Ni muhimu kuzingatia kuwa ujuzi anaojifunza mtoto unaimarika kadri umri wake unavyoongezeka. Mtoto wa mwaka mmoja, mathalani, hawezi kufanya yanayofanywa na mtoto wa miaka mitatu. Hata hivyo, kwa msaada wa karibu, mtoto aliye tayari kimwili na kiakili huanza kujifunza ujuzi muhimu anaouhitaji kwa maisha yake.

Shule zinadumaza stadi za maisha?

Kwa haraka, mtu anaweza kufikiri shule za bweni zinasaidia kujenga stadi za maisha kwa mtoto. Hata hivyo, hali halisi ni tofauti. Mazingira ya shule za bweni yanaonekana kuwa na uwezekano mkubwa wa kudumaza uwezo wa watoto kujitegemea na kujifunza stadi za maisha kuliko mazingira ya nyumbani.

Watoto wengi wa bweni hawana uwezo wa kufanya shughuli nyingi za msingi bila msaada wa watu wazima. Kwa mfano, katika utafiti uliotajwa, wengi hawakuwa na uwezo wa kujifanyia usafi binafsi bila usaidizi wa walezi wao.

Kadhalika, tabia ya kulowanisha vitanda iliripotiwa zaidi kwa watoto wa bweni kuliko wenzao wanaoishi nyumbani. Idadi ya watoto walioripotiwa kukojoa vitandani ilikuwa kubwa kwa upande wa bweni kuliko wale wanaolala nyumbani.

Ikumbukwe kuwa hapakuwa na msisitizo wowote kwa watoto hawa wa shule za bweni kushiriki shughuli za mikono kama wenzao walioishi nyumbani wala ukaribu wa kutosha kati ya walezi na watoto. Shughuli karibu zote za mikono zilifanywa na watu maalum. Ingawa lengo linaonekana ni kuwafanya watoto waelekeze juhudi zaidi kwenye taaluma, kwa kiasi kikubwa, matokeo yake yalikuwa ni kudumaza uwezo wa watoto kujitegemea na kujifunza stadi za maisha.


Inaendelea

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia

Pay $900? I quit blogging