Unavyoweza Kukuza Tabia Njema kwa Mwanao -1

Fikiria mwanao ana umri wa miaka kumi na minane na anaondoka nyumbani kwenda kujitegemea. Je, ungependa awe mtu mwenye tabia zipi? Ungependa mwanao anapoondoka nyumbani kwako kwenda kuanza maisha mapya awe mtu wa namna gani? Sifa zipi, ujuzi upi, haiba ipi ungependa imtambulishe akiwa mtu mzima?

Jiulize, wakati mwanao anaanza maisha ya ndoa, ungependa mwenzi wake aone tabia zipi kwake? Kama ni ajira, ungetamani awe na sifa zipi zitakazomsaidia kufanya vizuri kazini? Ungependa aishi namna gani na watu?

Katika mazungumzo yangu na wazazi, nimekuwa nikiwaomba wanitajie sifa wanazoamini watoto wao wanazihitaji ili kuwa watu wenye furaha, wanaoishi vizuri na wanaoweza kutegemewa na jamii.

Sifa zinazojitokeza mara nyingi zaidi ni kujiheshimu na kuheshimu wengine, uaminifu, uadilifu, uwajibikaji na bidii ya kazi. Nyingine ni moyo wa kiasi na nidhamu, ushirikiano na watu, ujasiri, uvumilivu na uwezo wa kutatua changamoto za kimaisha. 

Inawezekana kwa uzoefu na mazingira tofauti uliyonayo, orodha yako inaweza kuwa na sifa tofauti na hizi zilizotajwa. Hata hivyo, pamoja na tofauti zinazoweza kujitokeza, bado kuna uwezekano kuwa sifa hizo hazitakuwa mbali sana na hizi zilizotajwa.


Nafasi muhimu ya malezi

Imejengeka dhana kuwa mtoto huzaliwa na tabia zake. Kwamba jitihada za mzazi zina nafasi ndogo ya kujenga tabia fulani anazotamani mwanae awe nazo. Athari ya mtazamo kama huu ni mzazi kujipunguzia wajibu kwa imani kuwa ‘tabia ya mtoto ni kazi ya Mungu.’

Hata hivyo, bado wazazi wenye mtazamo huu hufanya jitihada fulani za kuhakikisha watoto wanajenga tabia njema. Watoto huadhibiwa, hukaripiwa na wakati mwingine hulazimika kusikiliza maelekezo ya kimaadili kama jitihada za kuwanyoosha wawe vile wazazi wanavyotamani wawe.

Pamoja na kutambua ukomo wa jitihada za kimalezi katika kujenga tabia njema, bado ni dhahiri malezi yana nafasi kubwa. Tabia wanazokuwa nazo watoto zinategemea namna wanavyolelewa tangu wakiwa wadogo.

Mbinu tulizozizoea

Pamoja na kuwa wazazi hutamani watoto wao wawe na tabia njema, mara nyingine mbinu tunazotumia kufikia lengo hilo huweza kutengeneza matatizo ya kitabia yasiyotarajiwa. Mbinu zilizozoeleka hulenga kufanyia kazi kile tunachojisikia kama wazazi kuliko kushughulikia kile alichokikosa mtoto ambacho kimsingi ndicho kilichomfanya akosee.

Makosa ya kitabia wanayoyafanya na watoto mara nyingi hulenga kufidia kile wanachohisi kukikosa kwetu wazazi wao. Kwa mfano, mtoto anayejisikia kutengwa, hutumia mbinu ya kudeka na kulia akitafuta kusikilizwa. Kwa kuwa mzazi hajajiuliza kwa nini mtoto analia lia bila sababu, hukerwa na tabia hii na kuamua kumchapa.

Mzazi anapomchapa ana nia njema kabisa ya kuhakikisha kuwa mtoto anajenga tabia zinazokubalika katika jamii. Lengo la adhabu inayotoelewa na mzazi ni kujaribu kumnyoosha mwanae afanane na matarajio aliyonayo. Lakini adhabu hiyo inapotolewa bila kuelewa msukumo ulio nyuma ya kile kilichofanywa na mtoto, tatizo jipya linaweza kuzalishwa.

Kwa mfano, mtoto anafanya vurugu kwa lengo la kupata usikivu wa mzazi. Badala ya kusikilizwa, mzazi anaongeza adhabu. Katika mazingira haya, mtoto anaweza kukosa imani na uwezo wa mzazi kuyaelewa matatizo yake. Badala ya kujenga tabia njema, akajenga hisia za kisasi na uasi dhidi ya mamlaka ya mzazi.

Aidha, mbinu nyingine tunayotumia wazazi ni ile ya kuwapa watoto ‘mawaidha’ yanayoelekeza kile tunachofikiri wanapaswa kukifanywa. Tunafanya hivi kwa nia njema ya kumjengea mtoto tabia iliyo njema.

Hata hivyo, utaratibu huu wa kutegemea ‘mahubiri’ mara nyingi hauleti matokeo yanayokusudiwa. Mzazi wa namna hii anaweza kushangazwa na usikivu hafifu anaokuwa nao mwanae. Kwamba pamoja na mzazi kutumia muda mwingi kumwelekeza mwanae namna ya kuwa mtu mwema, akashangazwa na matokeo. Mtoto anakuwa kinyume cha matarajio.

Changamoto ya kutegemea ‘mawaidha’ ni kuwa wakati mwingine hayafanikiwi kujibu matatizo halisi ya mtoto. Mfululizo huu wa ‘mahubiri’ ya kimaadili una hatari ya kumfanya mtoto asione sababu ya kuyafuatilia. Wakati mwingine  mtoto hujikuta anajenga upinzani wa kichini chini dhidi ya kile anachoambiwa.

Matokeo yanaweza kuwa mabaya zaidi inapotokea mzazi haishi kile anachokifundisha. Hali hii humfanya mtoto akose imani na maadili ‘yanayohubiriwa’ na mzazi. Kwa namna hii, mzazi anajikuta akipoteza mamlaka yake kama mzazi mwenye sauti inayosikika moyoni mwa mtoto.

Mbali na kufunza maadili, wazazi wengine hutumia mbinu ya kuminya uhuru wa watoto. Mzazi wa namna hii humlinda mtoto kupita kiasi akifikiri kwa kufanya hivyo anamwokoa na hatari anazoweza kukabiliana nazo. Mtoto anajikuta hana nafasi ya kuchagua zaidi ya kufuata kile kinachoamuliwa na mzazi.

Moja wapo ya athari ya kuwadhibiti mno watoto ni kuwafanya wakose uwezo wa kufanya maamuzi sahihi bila kutegemea mwongozo wa watu wengine. Mtoto wa namna hii hawezi kuwa na maamuzi yanayoanzia ndani yake. Hufanya kitu kwa sababu anafikiri ndicho kinachotarajiwa na wanaomzunguka. Mtoto huyu anapopata uhuru, mathalani kwenda shule ya bweni, hugeuka na kufanya mambo ambayo mzazi anaweza kushangaa kuyasikia.

Msingi wa makuzi ya tabia

Tukitaka kujenga tabia njema kwa watoto wetu, tunahitaji mbinu tofauti. Tunahitaji kuchochea chemichemi ya tabia zinazochipua kuanzia ndani. Tunahitaji mbinu zinazofanya mabadiliko ya tabia yaanze mioyoni mwao na sio kuwafanya walazimike kufanya yale wanaojua tunahitaji kuyafanya.

Tukitaka kumnyoosha mtoto awe na tabia njema zinazoanzia ndani yake, tabia zitakazoambatana naye hata atakapokuwa mtu mzima, tunahitaji kuanzia kwenye mahitaji yake.

Tunahitaji kumfanya mtoto ajione anaeleweka. Tusipoweza kumfanya mtoto akajisikia anaeleweka, hatuwezi kufanikiwa kumjengea tabia njema. Ili tuweze kumjengea hali ya kueleweka, tunahitaji kuwekeza katika ukaribu. Ukaribu maana yake ni ule urafiki unamfanya mtoto asijikie kuwa mtu wa thamani mwenye nafasi muhimu katika maisha ya mzazi wake. Ukaribu huu, kati ya mtoto na mzazi wake, ndio msingi wa tabia njema kwa mtoto.


Inaendelea

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Pay $900? I quit blogging

Heri ya mwezi mpya!