Sababu za Watu Kufanya Uchaguzi Mbaya wa Kazi



Uchaguzi wa kazi ni maamuzi anayoyafanya mtu kuanzia pale anapopata wazo la kazi anayotaka kuifanya mpaka anapostaafu. Haya ni maamuzi anayoyafanya mtu kutimiza ndoto zake kimaisha tangu anapokuwa masomoni; anapoomba kazi kwa mara ya kwanza na kuipata; anapobadilisha kazi na hata pale anapofikia umri wa kustaafu kazi.

Maamuzi haya yanaposhindwa kukidhi matarajio na kumfanya mtu asifurahie kazi yake, tunaweza kusema, hapo anakuwa amefanya uchaguzi mbaya wa kazi. Uchaguzi wa namna hii unaweza kusababisha mtu asiyotumie uwezo wake wote kazini, hali inayoweza kuleta kutokuridhika na kazi.

Kwa kuwa kutokuridhika na kazi kunaweza kusababisha mtu aache kazi, au aendelee kufanya kazi yake kwa manung’uniko, makala haya yanaangazia sababu tano kubwa zinazochangia watu kufanya uchaguzi mbaya wa kazi.

Kukidhi matakwa ya soko

Mwenendo wa soko ni sababu moja kubwa inayoathiri maamuzi ya kazi anayoyafanya mtu. Kwa kawaida, kazi zinazohitajika kwenye soko la ajira ndizo zinazowavutia watu wenye ndoto za kuajiriwa.

Hata hivyo, changamoto ya kuongozwa na soko ni pale mahitaji ya soko yanapobadilika ghafla kutokana na sababu mbalimbali ikiwepo mabadiliko ya kisera.

Hivi sasa, kwa mfano, karibu kila chuo kikuu hapa nchini kina program za ualimu. Kwa sababu ya mahitaji makubwa ya walimu mashuleni, wanafunzi wengi huona ni afadhali wasomee ualimu ili kujiweka kwenye mazingira mazuri zaidi ya kuajiriwa mara baada ya masomo.

Huko tuendako, hata hivyo, wahitimu wa ualimu wanaweza kuwa wengi kuliko mahitaji halisi tutakayokuwa nayo wakati huo. Katika mazingira kama hayo, wahitimu wengi wa ualimu watalazimika kutafuta ajira nyinginezo nje ya ualimu. Hali hii inaweza kuleta changamoto kwa wanafunzi walisomea ualimu kwa lengo la kupata ajira mapema.

Pamoja na umuhimu wa kuongozwa na mahitaji soko la ajira kufanya maamuzi, ni vyema kufikiri itakuwaje ikiwa hapo baadae soko la ajira halitahitaji ujuzi wako.

Kukidhi matarajio ya watu

Kuna kazi ambazo jamii huziheshimu kuliko nyinginezo. Mfano, kazi zenye kuhitaji ujuzi na maarifa maalum ambayo si watu wengi wanaweza kuwa nayo, huheshimika zaidi kuliko kazi zinazotegemea ujuzi wa jumla.

Aidha, mtu anayefanya kazi kama hizi huchukuliwa kama mtu mwenye hadhi ya pekee kwenye jamii na watu humpa heshima kama mtu mwenye ujuzi maalum.

Kwa kuwa binadamu kwa hulka yake anapenda heshima, ni rahisi kazi za namna hii kuwa chaguo la watu wengi hasa wasioutambua wito wao. Mara nyingi watu hawa hujikuta wakitamani kukidhi matarajio ya jamii kwa kuchagua kazi wanazojua zinaheshimika.  

Hata hivyo, mara nyingine, mtu anapofanya kazi kukidhi tu matarajio ya jamii anaweza kuishia kukosa furaha ya kazi hasa nyakati za changamoto.

Unapofanya kazi isiyoendana na wito wako, inakuwa rahisi kubaini unafanya kitu kisichokidhi matarajio yako binafsi mambo yanapokwenda kinyume na matarajio yako. Hali ya kuchoka huweza kusababisha kuacha kazi na kutangatanga kutoka kwenye kazi moja kwenda nyingine.

Kuiga waliofanikiwa

Kuna kijana mmoja alivutiwa sana na kazi za wakili mmoja aliyekuwa maarufu mwishoni mwa miaka ya tisini. Kwa sababu ya mafanikio makubwa aliyokuwa nayo wakili huyo, kijana yule aliamua kusomea sheria.

Baada ya kusomea sheria na hatimaye kufanya kazi za uhakimu kwa zaidi ya muongo mmoja, bado kijana yule anasema hajafikia mahali akajisikia utoshelevu wa kazi. Majuzi nilikutana naye akijaribu kufanya mipango ya kusomea kitu kingine kama jitihada za kutafuta utoshelevu.

Si jambo baya kuvutiwa na kujifunza kwa watu tunaofikiri wamefanikiwa kwenye kazi zao. Hata hivyo, unapoiga maamuzi ya mtu mwingine unahitaji kuchukua tahadhari.

Kila mtu ana upekee wake. Mtu anaweza kufanya vizuri kwenye eneo fulani la utaalam lakini hiyo isimaanishe kuwa na wewe ukifanya kitu hicho hicho utafanikiwa. Jitahidi kuuelewa upekee wako na elekeza nguvu zako huko.

Kupata kipato kikubwa

Upo ukweli kwamba moja wapo ya sababu kwa nini tunafanya kazi ni kutuwezesha kumudu maisha yetu. Kwa sababu hiyo, kazi zenye uhakika wa kipato kikubwa, huwa zinawavutia watu wengi kuliko kazi zenye heshima lakini hazina kipato kikubwa.

Si wakati wote, hata hivyo, suala la kipato huwa ni sababu iliyokamilika kueleza kwa nini tunafanya kazi. Yapo mazingira ambayo kazi inaweza kuwa na kipato kikubwa lakini haimfanyi mtu atumie uwezo na ujuzi wake kikamilifu.

Inapotokea mtu analipwa vizuri lakini haoni namna gani kazi hiyo inakwenda sambamba na vipaji na haiba yake, ni rahisi mtu huyo kuanza kujisikia kudumaa na hivyo kukosa furaha ya kazi.

Pamoja na kipato, angalia na sababu nyingine kama namna ujuzi, maarifa na uzoefu wako unavyotumika ikiwa utafanya kazi unayoichagua.

Ufaulu hafifu na uchumi duni

Katika mazingira yetu, kiwango cha ufaulu ndicho kinachoamua hatma ya mtu. Mtu mwenye ufaulu mkubwa wa masomo kwa kidato cha nne au cha sita ndiye anayekuwa na nafasi nzuri zaidi ya kufanya uchaguzi unaokidhi ndoto zake kuliko mwingine mwenye ufaulu usioridhisha.

Zipo kazi ambazo ili mwanafunzi apate nafasi ya kuzisomea na kuzipata, anahitaji kuwa na ufaulu mkubwa. Hizi ni zile kazi zenye kuchukuliwa kuwa nyeti mfano udaktari, sheria na uinjinia.

Ndio kusema, ufaulu dhaifu unaweza kuzima ndoto za mtu na kumfanya achague fani ambazo awali hakuwahi huzifikiria. Mtu, kwa mfano, anaweza kuamua kusomea sayansi ya udongo, si kwa sababu anaipenda lakini ndiyo inayopatikana kwa kutumia matokeo aliyonayo.

Pia, uwezo mdogo wa kiuchumi unaweza kuzima ndoto za maisha ya watu wengi. Jitihada za kupata mkopo wa elimu ya juu huchangia wanafunzi wasio na uwezo  kufanya maamuzi yasiyozingatia matamanio yao.


Ingawa ni kweli uchaguzi mbaya wa kazi unaweza kumgharimu mtu, bado hata hivyo, kuna nafasi isiyo na kikomo ya kurekebisha maamuzi yaliyokwisha kufanywa. Lililo muhimu ni kujua kile unachokihitaji.

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia