Mwalimu Anavyoweza Kukuza Uelewa wa Mwanafunzi

PICHA: Sunday Adelaja



Dhima kuu ya elimu iliyo bora ni kuzalisha raia wenye sifa ya udadisi. Hawa ni raia wanaofikiri kwa makini, wanaohoji mazoea, wasioridhishwa na majibu yaliyozoeleka na wenye ari ya kutafuta majibu ya changamoto zinazoikabili jamii yao.

Hatua ya kwanza ya mwanafunzi kuwa mdadisi ni kuelewa kile alichojifunza. Mwanafunzi asiyeelewa maudhui ya somo, hawezi kuwa na fursa ya kufanya udadisi.


Yapo mambo kadhaa yanayoweza kuifanya elimu ikuze udadisi. Mosi, ni mtalaa wenye ubora. Mtalaa ni mkusanyiko wa mambo yote, ndani na nje ya darasa, yanayomwezesha mwanafunzi kupata maarifa na ujuzi unaomsaidia kujitambua kibinafsi na kuitambua jamii anamoishi.

Mtalaa ni mwongozo wa jumla, wenye malengo mapana ya kumwuumba raia mwenye sifa fulani zinazokidhi mahitaji ya jamii husika.

Kimsingi, mtalaa ni matamanio ya jumla ambayo, ili yawe na maana, lazima yakutane na vipaji binafsi vya mwanafunzi kumfanya atambue wajibu alionao katika jamii sawa sawa na vipaji alivyonavyo.

Pamoja na ukweli kuwa mtalaa unahitaji kumwekea kijana mazingira ya kutambua vipaji vyake na nafasi aliyonayo katika jamii, kazi kubwa inabaki kuwa kwa mwalimu.

Mwalimu kama mtafsiri wa maudhui

Mwalimu ndiye mwenye wajibu wa kutafsiri malengo mapana ya mtalaa na kuyaoainisha na mazingira halisi anayoishi mwanafunzi. Bila mwalimu, mwanafunzi ataishia kupata maarifa na ujuzi wa jumla usiomsaidia kuona mchango wake mahususi katika jamii.

Ili mwalimu aweze kufanya kazi hiyo nyeti lazima awe na sifa fulani. Sifa ya kwanza na muhimu ni kuwa na weledi na ari ya kumjengea mwanafunzi uwezo wa kudadisi. Bila mwalimu mwenyewe kuwa mdadisi haiwezekani kutarajia matokeo tofauti na vile alivyo yeye mwenyewe. 

Ndio kusema, haitoshi kuwa na mtalaa bora kwa maana ya kuwa na malengo mazuri yanayogusa matatizo halisi ya jamii. Tunahitaji kuwa na utaratibu mzuri wa kusimamia utekelezaji wa mtalaa tukilenga kumsaidia mwanafunzi kujenga shauku ya kujifunza, kiu ya maarifa na njaa ya kudadisi.


Katika makala haya ninalenga kuonesha namna gani mwalimu aliyefuzu anaweza kutumia maudhui ya mtalaa huu kujenga tabia ya udadisi kwa wanafunzi wake.

Uzoefu wa Opportunity Education

Ninatumia uzoefu wa Shirika lisilo la Kiserikali liitwalo Opportunity Education Foundation linalofanya shughuli zake hapa nchini kwa ushirikiano wa karibu na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na Taasisi ya Ukuzaji Mitalaa (TIE).

Shirika hili linaendesha mradi unaoitwa Next Generation Learning (NGL) ambao kimsingi unajaribu kuboresha mbinu za kufundisha maudhui ya mtalaa wetu. Mradi unafanya kazi ya kutafsiri maudhui ya mtalaa wetu katika lugha inayorahisisha uelewa.

Kazi hii inafanywa na walimu wa shule zetu waliopata mafunzo maalum kuandaa mfululizo wa masomo yanayoandaliwa kutokana na mtalaa wetu na mazingira yetu.

Sambamba na kutafsiri maudhui ya mtalaa wetu, NGL wametengeneza mfumo wa ufundishaji na ujifunzaji wanaousimamia wao wenyewe kwenye shule teule. Mradi huu ambao tayari umeshaonesha mafanikio, unatumia kanuni kuu tano ambazo naamini mwalimu yeyote anaweza kuzitumia.

Katika makala haya, tutagusia kanuni mbili kuu ambazo ni kuoanisha maudhui yanayofundishwa darasani na maisha halisi anayoishi mwanafunzi na pili, kuchochea shauku ya mwanafunzi kuuliza maswali.

Kuoanisha maudhui na maisha

Tumekuwa tukifundishwa maudhui ambayo kwa kweli wakati mwingine hatuelewi tutayatumia wapi. Nakumbuka, kwa mfano, nikiwa kidato cha V kwenye somo la Fizikia tulifundishwa hesabu ndefu za namna ya kutafuta muda utakaotumiwa na tone la mwisho la maji kudondoka kwenye bomba la maji linalofungwa.

Hatukuelewa kwa nini ilikuwa ni lazima kusumbua akili kufanya hesabu hizi ngumu zisizotatua tatizo lolote kwenye maisha yetu ya kila siku.

Ufundishaji wa namna hii, kwa hakika, ulitukatisha tamaa sisi mwanafunzi kama wanafunzi kujifunza kitu ambacho hatuoni faida yake katika maisha yetu ya kila siku.

Mradi wa NGL umeonesha mfano wa namna tunavyoweza kuondoa hitilafu hii. Kupitia uandaaji wa mfululizo wa masomo yanayotafsiri mtalaa kwa lugha nyepesi (quests), mwanafunzi anasaidiwa kuelewa kwa nini anahitaji kujifunza kile anachotakiwa kujifunza.

Kupitia mfumo wao wa ujifunzaji, NGL wanajaribu kufikiri namna gani kile kinachofundishwa darasani kinaweza kugusa maisha ya kawaida ya mwanafunzi. Mwanafunzi anapoona uhusiano wa moja kwa moja kati ya maudhui anayojifunza na maisha yake ya kila siku anakuwa na ari kubwa ya kujifunza.

Anachojifunza mwalimu hapa ni kwamba ni muhimu kutafuta namna ya kuhusianisha somo lake na maisha ya mwanafunzi.

Mwanafunzi anapoelewa kwamba kile anachojifunza kinahusiana na maisha yake ya kawaida, inakuwa rahisi kwake kupanua uelewa wake kuliko pale anapojifunza kitu asichojua kitamsaidiaje.

Kwa mfano, mwalimu wa Kemia anapofundisha somo la mada (matter) anahitaji kufanya kazi ya ziada kumsisimua mwanafunzi aone namna maarifa ya mada yanavyoweza kumsaidia katika maisha yake ya kila siku.

Kuchochea maswali kwa mwanafunzi

Walimu wengi hawafundishi kuchochea uelewa. Kazi ya walimu imekuwa ni ‘kuhubiri’ maarifa na mwanafunzi anachukuliwa kama mtu ‘mtiifu’ anayesubiri kupikiwa kila kitu na mwalimu. Kazi pekee ya mwanafunzi inabaki ‘kumeza’ kile anachoambiwa. Hana fursa ya kuuliza wala kuhoji.

Aidha, shule zetu ‘zinazofaulisha sana’ kimsingi zinajitahidi kuhakikisha mwanafunzi anafahamu kwa hakika nini cha kukariri. Walimu wa shule hizi wanafanya bidii kubwa kuwaimbisha wanafunzi kile wanachojua kitaulizwa kwenye mtihani.

Mradi wa NGL unajaribu kukabiliana na changamoto hii. Mwanafunzi anajengewa uwezo wa kujiuliza maswali ya msingi kuhusu hicho anachojifunza badala ya kutegemea majibu yaliyopikwa na mwalimu.

Msisitizo hapa ni kumfanya mwanafunzi awe na uwezo wa kuibua maswali ya msingi yanayochochea udadisi wake katika masomo. Mwanafunzi anayewekewa mazingira ya kujiuliza maswali na kushiriki moja kwa moja katika kutafuta majibu, anakuwa na uwezo wa kudadisi kuliko mwenzake anayeshiriki ‘kumeza’ maarifa.

Kwa hivyo, mwalimu lazima afanye kazi ya kuibua maswali yanayohusiana na kile anachokifundisha ili wanafunzi waweze kujifunza kwa mfumo wa kutafuta majibu wao wenyewe. Mradi wa NGL unatuthibitishia kuwa mwalimu akiwezeshwa anaweza kutafsiri mtalaa huu unaodaiwa kuwa haufai kuibua kiu ya kutafuta majibu.

INAENDELEA


Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Pay $900? I quit blogging

Heri ya mwezi mpya!