Kumfundisha Mtoto Kuwajibika, Kufanya Kazi

Kumjengea mtoto uwezo wa kuwajibika ni wajibu muhimu sana wa wazazi. Bila kuweka mkazo mapema katika kukuza uwezo huu, mtoto anaweza kuwa mtu mzima asiyefahamu kufanya majukumu mengi ya msingi na ya kawaida. Mtoto aliyefundishwa kuwajibika hujiona ana wajibu wa kushiriki shughuli za ndani bila kujali jinsia yake. 

Katika makala haya, tunaangalia namna unavyoweza kumsaidia mtoto wako kujifunza kuwajibika angali mdogo na hivyo kujenga uwezo wa kumudu majukumu ya msingi kadri anavyoendelea kukua.

Umuhimu wa kujimudu na kuwajibika

Kujimudu ni uwezo wa mtoto kufanya kitu bila msaada mkubwa wa watu wengine. Kwa mfano, mtoto anayejimudu ni yule anayeweza kutembea mwenyewe, kulala bila kukojoa kitandani, kula mwenyewe, kuoga, kunawa, kupiga mswaki, kupaka mafuta, kuvaa nguo na kadhalika.

Kuwajibika, hali kadhalika, ni kuwa tayari kufanya majukumu bila kuwasubiri wengine. Ni kinyume cha uvivu na kutegea. Kadri mtoto anavyokua kimwili na kiakili, uwezo wa kujimudu huongezeka na ndio unaomfanya aweze kukabiliana na mazingira yake bila utegemezi. Kujimudu kunaenda sambamba na uwezo wa kujiamini.

Amudu mwili wake

Ingawa uwezo wa mtoto kumudu mwili ni wa kuzaliwa nao, kuna mambo yanayohitaji uongozi wa mzazi ili kujifunza. Kumudu haja ndogo, kwa mfano, kunahitaji msaada kama kumkumbusha mtoto kujisaidia kabla hajalala, kuweka muda maalum wa kumwamsha akajisaidie nyakati za usiku, hatua ambazo humsaidia mtoto kupunguza mkojo unaosababisha aloweshe kitanda awapo usingizini

Afanye usafi wake mwenyewe

Ni vizuri mtoto akaanza kujifunza kujisafisha mwenyewe tangu akiwa mdogo. Kwa mfano, tangu akiwa na umri wa mwaka mmoja, mtoto anaweza kuzoeshwa kutumia mswaki kusafisha meno kwa lengo la kumfanya ajenge mazoea ya kupiga mswaki.

Kadhalika, kadri anavyokua, anaweza kuanza kujifunza kujisafisha baada ya kujisaidia. Unapomfundisha kujisaidia kwenye sehemu maalum na kwa muda maalum, kwa mfano, msaidie ajue kujitawaza kadri anavyoendelea kukomaa kiakili.

Anapofikia umri wa miaka minne, mtoto anaweza kuanza kujifunza kufua nguo zake za ndani, soksi na leso kwa msaada wa watu wazima. Pia anaweza kuanza kujifunza kutandika kitanda chache, hata kama hataweza kufanya kwa ustadi. Lengo kubwa la kumshirikisha kazi hizi ni kumjengea ari ya kuwajibika mapema.
Kumpa mtoto nafasi ya kufanya kazi za nyumbani ni kumfundisha kuwajibika. PICHA: Sayuni

Kushiriki kazi za mikono

Shauku ya watoto kushiriki kazi za mikono huanza tangu wakiwa wadogo. Kwa mfano, mtoto wa miaka miwili au mitatu anaweza kabisa kutaka kudeki, kuosha vyombo na kushiriki kazi za jikoni hata kama haziwezi. Tunahitaji kuwapa fursa ya kujiona wanaweza kusaidia majukumu ya nyumbani kwa uangalizi wetu.

Hata wanapokuwepo watu wanaoweza kufanya kazi nyingi katika familia, ni vizuri kuwapa nafasi watoto kushiriki kazi ndogo ndogo nyumbani kuwajengea utamaduni wa kufanya kazi. Wapangie ratiba ya kufagia, kuosha vyombo, kumwangilia maua, wafundishe kufua nguo zao wenyewe. Kufanya hivi kamwe si kuwatesa wala ‘kuishi maisha ya kimasikini’ bali kuwafundisha kuwajibika pasipokuwategemea kupita kiasi watu wengine.


Tunapowasaidia watoto kujimudu na kujitegemea, kwa hakika tunawajenga kuwa watu watakaowajibika ipasavyo katika familia zao na jamii kwa ujumla. Uwepo wa watu wengine wanaoweza kufanya majukumu ya watoto katika familia, usifatufanye tuwanyime fursa watoto kujifunza maisha halisi watakayoyaishi kama watu wazima.

Niandikie: bwaya@mwecau.ac.tz, 0754 870 815

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia

Pay $900? I quit blogging