Mbinu za Kumshirikisha Mwanafunzi Katika Ujifunzaji


PICHA: United Nations

Majuzi niliwatembelea walimu wanafunzi waliokuwa wakiendelea na mazoezi ya ufundishaji. Mafunzo kwa vitendo yana umuhimu wa kipekee katika maandalizi ya walimu.

Katika kipindi hiki, mwanafunzi anapewa fursa ya kutumia maarifa aliyojifunza darasani katika mazingira halisi ya kazi. Kwa mwalimu, kama mimi, hiki ni kipindi cha kutathmini uwezo wa mwanafunzi wa ualimu kumudu majukumu yake.

Moja wapo ya vipindi vingi nilivyopata bahati ya kuhudhuria ni Baiolojia kidato cha III kilichokuwa kikifundishwa na mwanafunzi wangu wa mwaka wa II.

Baada ya kufanya utangulizi wa somo lake, mwalimu huyu mwanafunzi aliwaelekeza wanafunzi wake kukaa katika makundi ya watu watano watano kusudi wafanye majadiliano.

Majadiliano ni mbinu muhimu ya ufundishaji inayowawezesha wanafunzi kujifunza. Kama tulivyosema kwenye makala yaliyopita, kupitia majadiliano, mwanafunzi hupata fursa ya kusikiliza mtazamo tofauti kutoka kwa wenzake.

Aidha, majadiliano ni mbinu shirikishi inayolenga kumfanya mwanafunzi awe mhusika wa moja kwa moja katika ujifunzaji.

Pengine kwa kutambua umuhimu wa ushirikishwaji huu wa wanafunzi, mwalimu yule aliwaonesha wanafunzi wake mchoro wa jicho wenye herufi zinazoonesha sehemu mbalimbali za ndani ya jicho.

‘Naomba kwenye makundi yenu mjadili majina ya sehemu za jicho kwa kutumia herufi hizi zinazoonekana,’ aliwaelekeza wanafunzi wake na kuendelea, ‘mkishajadili mniambie kila herufi inawakilisha nini.’

Ingawa mwalimu aliwapa wanafunzi muda wa dakika 10 kukamilisha mjadala huo, kilichonishangaza wanafunzi hawakuweza kujadili chochote.  Walionekana dhahiri wakisubiri muda uishie ili wapate majibu kutoka kwa mwalimu.

Pengine kwa kuhisi wanafunzi wake ‘wanamwangusha’ kwa kumfanya aonekane hajaweza kuwashirikisha wanafunzi wake, mwalimu huyu alimua kupita kwenye makundi akiwasaidia wanafunzi kupata majibu sahihi.

Ushirikishaji wenye manufaa wanafunzi

Kimsingi mwanafunzi wangu huyu aliyekuwa akijifunza kazi hakufanya tofauti na yanayofanywa na walimu mashuleni.

Walimu wengi, kama ilivyokuwa kwa mwanafunzi wangu, hupata shida kujua ni wakati upi mwanafunzi ashirikiane na wenzake na anaposhirikiana na wenzake afanye nini.

Matokeo yake mwalimu hujikuta akiwafunga wanafunzi ufahamu wasijue nini cha kufanya kwa sababu hajaweza kuwawekea mazingira ya kujadili kitu kinachoeleweka.

Ili ushirikishwaji uwe na manufaa, ni vyema mwalimu ampe ampe mwanafunzi mtaji wa taarifa za msingi kuhusu jambo analokusudiwa kulijadili. Kazi ya mwanafunzi inakuwa ni kuchambua na kutafuta majibu ya maswali yake kwa kutumia nyenzo alizonazo.

Mfano, badala ya kuwaambia wanafunzi wajadili sehemu za jicho, kama alivyofanya mwalimu wangu yule, ingefaa awape nyenzo zilizosheheni taarifa za macho kisha awape swali linalowaongoza kutafuta majibu kwa minajili ya kuwawezesha kubungua bongo zao kwa ushirikiano.

Aidha, angeweza kuwauliza wanafunzi wake swali ambalo lingewasaidia kutumia uzoefu walionao tayari bila kulazimika kutumia rejeo fulani ili kazi ya mwalimu iwe ni kujenga kwenye kile ambacho tayari wanafunzi wanakifahamu.

Kwa kufanya hivyo, wanafunzi wasingebaki wakishangaa wasijue nini cha kufanya kwa sababu tayari wana kitu mahususi kinachowasaidia kuendesha mjadala wenye mwelekeo unaoeleweka.

Tofauti za wanafunzi

Wanafunzi wanatofautiana uwezo na vile wanavyoweza kujifunza. Kwa mfano, wapo wanafunzi wanaojifunza kirahisi kwa kusikiliza na kuona.

Hawa wanatumia zaidi masikio na macho yao kufyonza taarifa wanazokutana nazo darasani. Uelewa wao unategemea namna gani wanaweza kumsikiliza na kumwona mwalimu darasani kuliko kujisomea wenyewe.

Pia, wapo wanaojifunza vizuri zaidi kwa kuongea. Hawa wanahitaji kusema, kwa maana ya kujadiliana na wenzao ili waweze kuchakata maarifa. Bila kujadili wanakuwa na wakati mgumu kuelewa.

Lakini pia wapo wanaotegemea kutenda na kushughulisha viungo vya miili yao ili waelewe. Bila kutenda, kushika, kutumia inakuwa vigumu kwao kuelewa.

Uelewa wao, kwa kiasi kikubwa, unategemea namna gani wanatumia mikono yao, miguu yao na hata kutembea tembea kama namna ya kushiriki kile wanachojifunza.

Namna gani mwalimu anayefundisha darasani anazingatia tofauti hizi? Je, mwalimu anawezaje kufikia mahitaji ya kipekee ya kila mwanafunzi ndani ya kipindi cha dakika 40?

Badala ya kukazana kuelezea dhana kwa hotuba pekee, mwalimu hawezi kuwafanya wanafunzi wakaongea, wakatumia michezo, wakaona, wakagusa?

Kutumia nyenzo tofauti

Tofauti hizi za ujifunzaji zinamlazimu mwalimu kutumia nyenzo tofauti za maarifa. Kwa mfano, mwalimu anaweza kutumia vitabu kama nyenzo yenye maelezo kina kwa kile anachokusudia kieleweke.

Wanafunzi wanaposoma vitabu wanapata nafasi ya kuzama kwa undani kupata maelezo ambayo pengine mwalimu hatakuwa na muda wa kuyagusia.

Hata hivyo, pamoja na uzuri wake, vitabu vinaweza kuwasaidia baadhi ya wanafunzi hasa wale wasio na ugomvi na usomaji wa kina.

Kwa hiyo, pamoja na kutumia vitabu, mwalimu anahitaji kufikiria nyenzo nyingine kuwafikia wanafunzi wengine. Kwa mfano, penye uwezekano, mwanafunzi ashiriki kwa kubuni michezo inayoweza kuwasaidia wanafunzi wanaojifunza kwa kutenda kuliko kusoma.

Pia, mwalimu anaweza kufikiri kutumia picha za mnato na video kama namna ya kuwasisimua wanafunzi kujifunza. Faida ya kutumia picha na video ni mwanafunzi kuona kwa uhakika kile kinachozungumzwa.

Kwa mfano, mwalimu anayefundisha ‘sehemu za moyo’ anapokuwa na nyenzo za picha halisi za moyo anamrahisishia mwanafunzi kazi ya kujenga taswira ya kitu kinachozungumzwa.

Mwanafunzi anayeona kitu halisi, ni tofauti na mwenzake anayeambiwa tu kitu asichojua kinafananaje. Nguvu atakazotumia kujaribu kutengeneza picha ya kile anachofundishwa inaweza kuhujumu uelewa wake.

Binafsi nimekuwa nikitumia mbinu ya kuonesha vipande vya filamu kwa wanafunzi wangu. Mbali na kuwasisimua kufuatilia kile wanachohitaji kujifunza, nimeona namna nyenzo hizi zinavyowasaidia wanafunzi kujifunza kwa wepesi zaidi.

Kukabiliana na changamoto

Naelewa shule zetu zina changamoto kubwa ya vifaa. Ninapoongelea kutumia filamu, naelewa shule zetu nyingi hazina umeme na hivyo kuzungumzia teknolojia ni sawa na kuwadhihaki walimu wanaofundisha kwenye mazingira haya.

Hata hivyo, mazingira haya magumu bado si kisingizio cha mwalimu kuendelea kung’ang’ania mbinu za kimazoea katika ufundishaji.

Kwa mfano, badala ya kutumia muda mwingi kuandika ‘notes’ ubaoni, kwa nini mwalimu asitumie muda huo kuwafanya wanafunzi wahusianishe somo lake na maisha yao ya kila siku? Je, mwalimu hawezi kufikiri namna ya kuendesha mjadala mpana badala ya kuishia kuhutubu?

Mwalimu anahitaji ubunifu kutengeneza zana za kufundishia kwa kutumia vifaa vinavyopatikana katika mazingira yake.
Mfano, badala ya kuilalamikia serikali kwa kutokumpelekea tufe, mwalimu anaweza kutumia kibuyu, rangi na mbao na akapata mfano wa tufe.


Ndio kusema, pamoja na changamoto nyingi zinazokabili shule zetu, bado upo uwezekano mkubwa kwa mwalimu aliyefuzu kubuni nyenzo mbalimbali zitakazomsaidia kuwashirikisha wanafunzi wake. 

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia