Watu Wasikupotezee Lengo

PICHA: Steemit

Huenda kuna kitu kimekatisha tamaa leo. Huna matumaini tena. Kile unachokitarajia hakionekani kutokea. Umeanza kufikiri kubadili mipango yako. Ujumbe wangu kwako ni mfupi. Usikate tamaa.

Januari 2014 nilikuwa mwanafunzi. Matokeo ya Course Work kwenye somo moja yalipobandikwa nilikuwa nimefanya vibaya sana. Kilichoniumiza zaidi nilikuwa mtu wa tatu au wa pili kutoka mwisho. Hakuna kitu kibaya kama kujisikia kilaza unapojilinganisha na wenzako. Sikujua namba ya mtu yeyote lakini nilikuwa na uhakika nimekuwa wa mwisho. Nilikakata tamaa sana hasa kwa sababu somo lenyewe nililipenda na nilitumia muda wa kutosha kulisoma na kulielewa. Nakumbuka siku hiyo nilikwenda Library nikashindwa kabisa kusoma. Mawazo, "Msuli wote ule kweli?"

Katika nyakati kama hizi maneno unayoyasikia kutoka kwa wanaokuzunguka yana nguvu kubwa ya ama kukunyong'onyeza na kukumalizia au kukuinua. Baadhi ya niliokuwa nasoma nao waliona hiyo ndiyo ilikuwa fursa ya kunidhihaki hasa kwa sababu nilikuwa natumia muda mwingi Library. 'Wachambuzi" wakataka niamini kosa langu lilikuwa kusoma sana.

Somo hilo nililokuwa nimeshika mkia nilikuwa nimefanya vizuri sana kwenye Presentation. Mwalimu alisifia sana kazi yangu na alinitumia kama reference mara nyingi darasani. Kufeli kulijaribu kuonesha mwalimu alikuwa amenipendelea na kunipa sifa nisizostahili. Wakati mwingine kinachokutesa kinaweza kuwa hakipo zaidi ya historia. Unaumizwa na mazuri yaliyowahi kukutokea na unajisikia mtu mwenye bahati mbaya kuharibu historia yako.

Nakumbuka wengine waliniambia, "Kwenye mambo haya ni vizuri kumtegemea Mungu." Walimaanisha nimefeli kwa sababu simtegemei Mungu. Wengine wakaniambia, "Ni vizuri kusoma na wenzako. Kushinda East Africana (Library) sio kufaulu." Maneno kama hayo yalininyong'onyeza.

Niliamua kufanya kitu kimoja. Nikaamua kupuuza mashambulizi hayo ambayo niligundua hayakuwa na lengo la kunisaidia. Nikarudi ndani yangu. Nikajiuliza nimekosea wapi? Kwa nini nimeshika mkia pamoja na kufanya wajibu wangu kikamilifu? Je, nisingeshinda East Africana ningefaulu kama 'washauri wangu'? Nikajitia ujasiri. Nikajiambia kwa ujasiri, "Kuna UE," kisha nikaendelea kusoma kwa bidii na kujituma kinyume na ushauri niliokuwa naupewa na waheshimiwa wachambuzi wa matokeo. 

Nikafanya mtihani wa mwisho. Nilikuwa na matumaini. Baada ya takribani mwezi 'Class Rep' alinipigia simu jioni moja. 
"Kaka hongera sana." 
"Kuna nini mkuu?" nilimwuuliza nikijiandaa kusikia habari njema. 
"Nimetoka kwenye kikao cha kupitisha matokeo. Kwenye course zote hapa SOED (Shule Kuu ya Elimu ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam) aliyefanya vizuri zaidi katoka kwetu. Ndio wewe. Umetisha kaka." 

Sikujua kuna watu wanafuatilia matokeo kiasi kile. Lililo muhimu kwa wakati huo ni kuwa nilipata kicheko cha mwisho baada ya kuvumilia maumivu ya kuwa mkia kwa muda. Nilikuwa nimefanya vizuri sana.

Maisha yana vingi vya kukukatisha tamaa. Kile kile kinachokufanya ujitume na kufanya kazi kwa bidii, ndicho hicho hicho kinaweza kukugeuka na kukukatisha tamaa usipokuwa mwangalifu. Muhimu ni kwamba mambo yanapokwenda mrama usikubali kusalimu amri. Usiwape nafasi 'washauri' wakuoneshe utaalam wao. Kuna watu wengi hutumia fursa hiyo kukumaliza hata kama kwa haraka haraka unaweza kufikiri wanakufariji. 

Katika nyakati ngumu, ni muhimu sana usipoteze lengo. Kinachoonekana kuwa aibu kinaweza kugeuka kuwa somo muhimu kwa mafanikio yaliyoko mbele yako. Usikubali kupoteza lengo. Usiruhusu mtu akuambie maneno yanayokupoteza lengo.

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Pay $900? I quit blogging