Unaweza Kumruhusu Mtoto Afuate Dini Apendayo?

PICHA: Pixabay



Ipo nafasi muhimu ya imani/dini katika malezi ya watoto. Imani si tu inamsaidia mtoto kujitambua, lakini pia ina nafasi ya kumtengenezea mtoto sauti kutoka ndani yake inayomsaidia kupambanua lililo jema na baya. Sauti hii inaitwa dhamira.

Utakuwa shahidi kuwa kuna mambo wakati mwingine unatamani kuyafanya lakini unajisikia hatia kuyafanya. Unaweza, kwa mfano, kuwa na uhuru wa kutaka kufanya chochote, lakini kuna sauti ndani yako ikakunyima ujasiri wa kukifanya. Hakuna anayekuona, hakuna anayekuhukumu, lakini kuna kengele ndani yako inakwambia kuwa unachotaka kukifanya sio sahihi.

Mwanasaikolojia wa kale anayeitwa Sigmund Freud aliita kengele hiyo ‘Superego’ kumaanisha mkusanyiko wa maelekezo tunayoyapata kwa watu wanaotuzunguka. Kwa kawaida, sauti na maelekezo hayo inayoumbika ndani yetu ndiyo inayoamua namna gani tunadhibiti matamanio yetu ya asili kama hasira na tamaa za mwili.

Imani, tafiti zinasema, ina kazi kubwa ya kujenga dhamira. Mtu mwenye dhamira iliyojengwa sawa sawa anakuwa na uwezo mzuri wa kupambanua lililo jema na baya. Kwa mfano, watoto waliolelewa kwenye misingi imara ya kiimani/kidini, wana uwezekano mkubwa zaidi wa kuwa na nidhamu, kufikiria mahitaji ya wengine, na hata kuchelewa kuanza kushiriki mapenzi ukilinganisha na watoto wasio na mizizi yoyote ya kiimani/kidini.

Nakumbuka nikiwa na umri wa miaka kama mitano na kuendelea baba yangu alikuwa na utaratibu tuliouchukulia kama desturi ya nyumbani. Kila jioni ilikuwa ni sharti mimi na wadogo zangu wawili tukutane nae sebuleni kufanya ibada ya pamoja. Katika ibada hizo, tuliimba, tulisali, na kusikiliza hadithi zilizotokana na mafundisho ya biblia.

Mzee alitumia hadithi kutufundisha mambo mengi yanayohusu imani na maadili. Kipindi hicho, miaka ya 80 hapakuwa na televisheni nyumbani isipokuwa radio. Hadithi hizo zilikuwa mithili ya tamthlia za leo zilizoanza tangu nyakati za uumbaji, Adamu na Hawa katika bustani ya Eden, historia ya Uyahudi ya kale mpaka maisha ya Bwana Yesu Kristo. Kila baada ya masimulizi hayo yaliyonukuu vifungu vya biblia, tulijifunza namna gani mambo hayo yalihusianishwa na maisha yetu kama watoto. Tulisisimuka kweli kweli kama watoto.

Sauti ya mzee haikuondoka kwenye ufahamu wangu. Kila mara katika utoto na ujana wangu ningeweza kumsikia akizungumza na mimi. Hata hivi leo, kuna nyakati ninapofanya maamuzi ya kimaisha, nakumbuka sauti niliyozoea kuisikia zaidi ya miaka 30 iliyopita. Hiki ndicho ambacho Sigmund Freud alikiita ‘superego.’

Hata hivyo, kuna changamoto ya kutofautisha dini na imani. Wakati imani ni maisha ya kiroho aliyonayo mtu, dini ni suala la kitaasisi zaidi. Ndio kusema unaweza kuwa na dini lakini ndani yako pasiwe na sauti dhahiri inayoongoza uhusiano wako na Mungu.

Wengi wetu tulilelewa kidini lakini si kiimani. Tulifundishwa kutii taratibu zinazoongoza dini zetu lakini hatukujua kwa hakika kile tunachokiamini.  Sasa tumekuwa wazazi, nasi tunafanya yale yale. Tunawarithisha watoto dini zetu na kusahau maisha yao ya kiroho. Matokeo yake, tunashuhudia watoto wengi wakifanya mambo yasiyo ya adili na tunashangaa imekuwaje.

Je, tunaweza kuwafundisha watoto wetu imani kwa maana ya kuwakuza kiroho badala ya kushika dini? Je, unaweza kumruhusu mwanao kutafuta imani nje ya dini yako?

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Pay $900? I quit blogging

Haiba ni nini?

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Heri ya mwezi mpya!