Je, Kazi yako Inakuza au Inadumaza Wito Wako?




Inawezekana unafanya kazi ambayo hukuwahi kufikiri kama siku moja ungeifanya. Labda unadhani hukuchagua vizuri kipi cha kufanya, au pengine mazingira yalikulazimisha kushika kilichokuwa kinapatikana.

Kwa upande mwingine, inawezekana pamoja na kuipenda kazi yako, unahisi kuna namna fulani ya udumavu. Hupati fursa za kupanda ngazi kiutendaji na umeanza kujihisi unapoteza wito wako.

Vyovyote iwavyo, bado kuna tumaini. Unaweza kabisa kufanya kazi unayojua fika haiendani na wewe, lakini hatua kwa hatua, ikakutengenezea jukwaa zuri la kuumba vizuri wito wako.

Hapa ninakuletea uzoefu utakaokusaidia kujitathmini na pengine kuchukua hatua muhimu katika kuchochea ule uwezo wa pekee ambao Mungu ameuhifadhi ndani yako.

Unafanya kazi yenye staha?

Mratibu wa Ukuuzaji wa Ujuzi wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) Dar es Salaam, Bw. Albert William Okal anaeleza namna gani mazingira yako ya kazi yanavyoweza kukuza wito wako:

“Hakuna kitu kama uchaguzi mbaya wa kazi. Kila kazi unayofanya inaweza kuwa sahihi kwako ikiwa tu mazingira yake yanawezesha kukuza ujuzi. Ukiweza kujifunza namna nzuri ya kufanya kazi yako, ukagundua aina ya majukumu unayoyafanya kwa ufanisi zaidi, unaweza kabisa kuigeuza kazi usiyoipenda kuwa na tija badala ya kukimbilia kubadilisha kazi (tafsiri ni yangu.)”

Okal anafafanua, “Tukichukulia wito kama uwezo wa kukuza ujuzi na uzoefu wa kazi, maana yake lazima tufanye kazi kwenye mazingira yanayotufanya tupate utoshelevu."

"Nafikiri mtu anayefanya kazi inayompa uhuru wa kutumia maarifa na ujuzi wake; kuheshimiwa na kutambuliwa kwa juhudi anazoweza kazini; nafasi ya kujifunza na kujiongeza, mazingira yanayompa nafasi ya kufanya makosa na kumruhusu kujifunza kupitia makosa hayo, uwepo wa ujuzi stahiki kwa ajili ya kazi hiyo; hayo yote kwa pamoja yanaweza kuwa fursa ya mtu kuboresha wito wake.”

Uzoefu wa Bw. Okal unatufunza mambo mawili makubwa. Kwanza, hata kama unafanya kazi unayoamini haikuwahi kuwa chaguo lako, huna sababu ya kukata tamaa. Kazi yako ya sasa inaweza kuwa daraja la kukuza ujuzi wako na kukufikisha kule unakotaka kwenda.

Hilo, hata hivyo, linategemea ubora wa mazingira ya kazi. Mbali na juhudi zako binafsi, mwajiri naye ana wajibu wa kukupa ushirikiano na msaada wenye lengo la kukuwekea mazingira bora ya kazi.

Ndio kusema kazi yoyote inayokupa uhuru wa kubuni mambo mapya, kujifunza na kutumia ujuzi mpya, inaweza kukusaidia kuendelea kujitambua na hivyo kuufikia wito wako.

Unajifunza ujuzi mpya?


Wakati mwingine unaweza kukata tamaa kwa sababu wenzako wanabadilisha kazi mara kwa mara na wewe umeendelea na kazi hiyo hiyo kwa muda mrefu. Je,hiyo inaweza kuwa na maana ya udumavu kazini?

Albert William Okal ana mawazo tofauti: “Aina ya majukumu unayofanya sambamba na nafasi unayopata ya kujifunza na kukuandaa kwa majukumu makubwa zaidi inaweza kuwa sehemu ya kukua kazini. Mwalimu, kwa mfano, anaweza kuendelea kuwa mwalimu lakini majukumu yake yakawa yanabadilika kadri anavyojifunza ujuzi mpya. Kutoka kuwa mwalimu asiye na majukumu, anaweza kuwa Mkuu wa Shule, Mkaguzi wa Shule au Afisa Elimu. Huyu huwezi kusema amedumaa kikazi.”

“Lakini pili, ni muhimu ufanyaji kazi nao uboreshwe. Unaweza kufanya kazi hiyo hiyo lakini ukajifunza ujuzi mpya wa namna ya kutekeleza majukumu yako. Hapo huwezi kusema kazi yako imekudumaza. Mfano mfanyakazi aliyekuwa anasambaza mizigo kwa mguu, anapofikia hatua sasa anatumia baiskeli au pikipiki kufanya majukumu yale yale, hiyo pia ni ishara ya ukuaji. Kigezo cha tatu, kwa maoni yangu ni tija ya kipato. Kazi inayokukuza lazima iende sambamba na ongezeko la kipato.”

Ndio kusema, kwa mujibu wa Bw. Okal, unapokuwa kwenye mazingira ambayo namna yako ya kufanya kazi haibadiliki, muda unaenda unatumia njia zile zile kufikia malengo yale yale, tafsiri yake inaweza kuwa udumavu kazini.


Unatumia vipawa vyako?

Kwa upande wake, Lonyamali Morwo Mkurugenzi Mtendaji wa MultiSkills Business Consultancy ya Arusha, anafikiri kazi inayokukuza lazima ikuwezeshe kutumia vipawa vyako:

“Kila mtu amezaliwa na kipaji fulani. Sote kwa namna moja au nyingine kuna kitu tumeitiwa kukifanya. Swali kubwa tunalohitaji kulijibu ni ikiwa tunafanya kazi kufuatana na vipawa vyetu au basi tu tumelazimishwa na mazingira tunayojikuta nayo kazini?” anauliza na kuendelea, “Ukitaka kufanikiwa katika maisha ni lazima kutambua kipawa chako. Haijalishi unafanya kazi ya kuajiriwa au umejiajiri, suala la muhimu ni je, unapenda unachokifanya?”

Bw. Morwo  anaamini maswali matatu yanaweza kutusaidia kujitathmini. Anasema: “Ni muhimu kujihoji. Je, ninachokifanya ndicho nilichoitiwa kufanya? Je, ninachokifanya ndicho ninachokipenda? Je, kinachokusukuma ndani yako ni nini, kipawa ulichonacho au wajibu uliopewa na mwajiri?” Kinyume na hapo kazi unayofanya inaweza kuwa inadumaza wito wako.

Ushauri

Lonyamali Morwo anashauri,  “Lenga kujenga kipawa chako kupitia kazi unayofanya. Fanya kitu unachokipenda na chenye msukumo wa kutoka ndani ya nafsi yako. Ukifanya kitu kisichotoka ndani yako utafanya kwa uzito kumridhisha aliyekuamuru ukifanye na hiyo itakuwa ni kutimiza wajibu.”

Kwa upande wake, Albert William Okal anasema huna sababu ya kuhama hama kazi kukuza uwezo wako: “Jipe muda kukaa kazini ulete tofauti inayoonekana hata kama hupati kipato kikubwa. Epuka kuacha kazi ndani ya muda mfupi kwa kisingizio cha kutafuta maslahi zaidi. Kwa namna hiyo utakuwa unajijenga kiuwezo na ufanisi wako utaongezeka (tafsiri ni yangu).”

Tunajifunza thamani ya uzoefu na ujuzi kazini. Kadri unavyopata ujuzi mpya kazini ndivyo unavyojitambua vizuri zaidi. Ukijitambua na kujituma, kazi yoyote unayoifanya sasa ina nafasi ya kukujenga kwa maana ya kukujaza uwezo mpya utakaokusaidia kuufikia wito wako.

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia