Laiti ningeweza kuisemea nafsi vizuri!

Natamani sana kuandika kila siku. Natamani ningekuwa na shughuli moja tu ya kusema yaujazayo moyo. Kusema na kusema. (Hakuna kitu nafurahia kama kuyatoa yaliyopo moyoni).
Huwezi kuyatoa kama hayapo huko yanakodhaniwa kutokea. Huwezi kusema kama huna cha kusema. Huwezi kuandika kama huna cha kuandika.

Mimi nina agenda moja kubwa: Kujielewa. Natafuta namna nzuri ya kuiweka agenda hii mahala pale. Kuisema mpaka isemeke.

Lakini tatizo kubwa ninalokabiliana nalo ni mwingiliano wa majukumu. Majukumu mengine hayasubiri kama ambavyo wengi wetu tunajua. Majukumu ya kitumwa tumwa hivi, kwamba tuwasikilize wenzetu watujaze yale yanayoitwa maarifa yapatikanayo katika taasisi ziitwazo 'shule'. Nadhani hatujafika mahala tukakubaliana kwamba majukumu haya yanaweza kusubiri. Hivyo ninawajibika kwayo, walau kwa sasa.

Pamoja na ukosefu wa muda (hivi kweli ni ukosefu ama udhaifu wa mpangilio wa muda?) wa kubwabwaja hapa, huwa nafidia kwa kujibwabwajia mwenyewe. Nadhani kujisemea kuna nguvu zaidi ya kuwaambia wengine. Najaza diary yangu kuandika yale ninayodhani yanagoma kubaki ndani - yanatamani kunitoka saa nyingine bila mpangilio. Ili niandike yale ninayojiambia na kujiuliza.

Kwa sababu kwangu mimi, kuandika ni kujiweka huru basi ni lazima nitaandika sana. Ninajipanga vizuri niseme kile ambacho najua fika kiko ndani yangu. Laiti ningeweza kuanzia leo!

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Pay $900? I quit blogging

Heri ya mwezi mpya!