Kuwa mwenye furaha ni uamuzi wako mwenyewe!

Ni mara ngapi umewahi kukutana na mtu aliyekukwaza kiasi cha kumtupa katika kapu la “watu wa hovyo” wasiostahili heshima kama binadamu? Umewahi kupatwa na tukio ambalo lilibadili kabisa mtazamo wako kuhusu maisha, watu na maisha kwa ujumla? Kwa nini watu kukata tamaa? Umewahi kuwaza kwa nini kinachomkwaza huyu si lazima kimkwaze yule?

Umewahi kuonana na mtu anayeshangaa inakuwaje “huyu bwana achukue uamuzi wa ajabu namna ile” wakati kilichotokea kinachukuliwa na wengi kuwa “ni jambo la kawaida”?

Natamani ukimaliza kusoma hapa uelewe kwamba sehemu kubwa ya matatizo tunayokabiliana nayo kama binadamu kila siku, tunayasababisha wenyewe. Na kwa yale tusiyo naudhibiti nayo, tunaweza kubadili mtazamo wetu kwayo, na hilo linaloonekana kuwa tatizo ama likawa si tatizo au likabadilika kuwa changamoto.

Wengi wetu tunapokumbana na vikwazo (ambavyo mara nyingi huwa ni watu, vile mambo yalivyo na matukio yanayokuwa katika namna tusiyoitegemea) hujenga mawazo kwamba vitu hivyo vi vibaya. Matokeo yake tunatumia muda mwingi sana kusononeka na hivyo kujikuta tukijiumiza sisi wenyewe zaidi na/au kuwaumiza wengine. Tunajikuta tukizalisha matatizo mengine ambayo kimsingi hatukuwa na sababu ya kuwa navyo, kwa sababu tu ya mtazamo.

Hasira, kukata tamaa, kuvunjika moyo, msongo wa mawazo na yote yanayofanana na hayo yanatupa ujumbe kwamba mwenye hayo anaamini kwamba yupo mtu, ama tukio, ama hali imemkosea! Hayo niliyoyataja huja kama matokeo ya mtazamo hasi. Huja kama matokeo ya tatizo letu wenyewe.


__________________________________________________
Mwanamke akifarijiwa baada ya tukio baya lililopoteza maisha ya watu kadhaa. Hapa tunaona tukio hilo hilo linapokelewa tofauti na watu hawa wawili. Picha: AP│Ilitumiwa mwanzo na telegraph.co.uk


Sijui kama unajua kuwa matukio yote yatokeayo katika uasili wake hayana uzuri ama ubaya? Una habari kwamba mengi kama sio yote anayoyafanya mwanadamu katika asili yake hayana uzuri ama ubaya? Unajua kuwa jinsi mambo yalivyo/situations katika uasili wake hayana ubaya wowote ama uzuri?

Pengine utaniuliza swali la kifalsafa: uzuri ni nini na unatofautianaje na ubaya? Ni bahati mbaya kwamba mazungumzo yetu ya leo hayana mwelekeo huo. Hata hivyo katika mipaka ya mazungumzo ya leo, uzuri tutaufafanua kama hali ya kupendeza wakati ubaya ni kinyume chake.

Kwa hiyo, hakuna kilicho katika uasili wake chenye uzuri ama ubaya. Naipenda kanuni hii, kwamba jinsi mambo yalivyo, watu, na matukio vyote hivyo ni neutral, havina uzuri wala ubaya! Uzuri ama ubaya wake hututegemea sisi! Hiyo ina maana kwamba ni mtazamo wetu sisi ndio huyageuza matukio, watu ama vile mambo yalivyo (situations) kuwa ama mabaya ama mazuri.

Nikifikiri kwa mtindo huo (kwamba uzuri ama ubaya wa lolote unanitegemea mimi na na sio kitu ama tukio) sikosi kugundua kuwa vingi vya vile vinavyonikesesha raha, utulivu na amani yangu vingeweza kabisa kufanya kazi tofauti kama ningebadili tu namna ninavyovichukulia.
Hebu fikiria ni misongo mingapi ya mawazo tunaisababisha wenyewe? Mara ngapi tumekosa amani na kukata tamaa kwa sababu tu “ya mtazamo wetu wenyewe”?
Mara ngapi tumejiumiza wenyewe kwa kuwawazia wapendwa wetu “ubaya” wasiokuwa nao kwa sababu tu tulijipa kazi ya “kuwabandika lebo ya ubaya”?

Najua yapo matukio ambayo kwa hali ya kawaida yanaweza kubadili kabisa “sripti” ya sehemu ya maisha yetu yaliyobaki. Matukio kama ya kufiwa na watu tuwapendao, kufukuzwa kazi na kadhalika. Lakini tunapotulia na kujibidiisha kubadili mitazamo yetu kwayo, twaweza kabisa kubaki na amani ya mioyo yetu na maisha yakaendelea!


Watoto wadogo huonekana kuwa na furaha kuliko watu wazima kwa sababu nyingi. Moja wapo ni kutokujua ubaya wa vingi vinavyowazunguka.

_______________________________________________________________________
Ipo orodha ndefu ya watu wanaotukosesha amani, tunaokosana nao kirahisi ama kukaripiana na kuvunjia heshima hadharani, ambao (kwa kubadili tu mitazamo yetu) tungeweza kabisa kuwapenda na kuishi nao kwa namna inayoweza kutushangaza sisi wenyewe!

Niliwahi kuishi na rafiki yangu mmoja siku za nyuma aliyekuwa na tabia za kunikera. Vingi vya alivyovipenda vilikuwa kinyume na yale yanayoitwa “maadili” yaani ethos. Majaribio ya mara kwa mara kuzungumza naye hayakusaidia kumbadili. Kila siku tuliyoishi naye ilioongezea hasira.

Ilinichukua muda kukubali kuwa yule rafiki yangu hakupenda kuwa vile alivyo. Kwamba alichokuwa akikifanya kilikuwa msukumo ulio nje ya uwezo wake mwenyewe. Hakupenda kuwa vile na hata kuamini alikuwa sahihi. Ni kwa kutambua hivyo, nikabaini kuwa kujaribu kumbadili hakutawezekana. Nikabaini kuwa anayo haki ya kuwa yeye. Na ni makosa mimi kujaribu kumgeuza yeye awe mimi.

Tangu kipindi kile, nilichokuwa nakiona awali kuwa kero kikabadilika kuwa sehemu ya maisha. Hatimaye nakumbuka ilikuja kuwa huzuni sana kuachana na rafiki yangu huyo tulipolazimika kutengana kimakazi. Kwa nini? Nilifanikiwa kubadili mtazamo wangu kwake na kusitisha “jaribio” la kumbadili yeye!

Huo ni mfano mdogo sana kutosha kukuelewesha namna ambavyo mara nyingi tatizo huwa kwetu tunaokwazwa, kuchukizwa na kuumizwa na wengine. Kwamba namna tunavyoyachukulia mambo huathiri sana “ubaya na uzuri wa jambo”.

Anza kuona uzuri wa watu wanaokuzunguka (hata kama itakubidi uutafute sana). Anza kuuchukulia udhaifu unaouona kwao kama tofauti baina yenu. Utashangaa.

Ni salama zaidi kuelewa kuwa mara nyingi watu hufanya mambo fulani kwa msukumo ulio juu ya uwezo wao. Msukumo huu ndani yetu hujengwa na vingi, kikubwa kikiwa ni mazingira tunayokutana nayo tangu dakika ile tunapozaliwa (malezi, dini/imani, marafiki nk) mpaka pale msukumo huo unapoota mizizi minene kiasi ya kutuongoza kutenda vile vinatenda!

Chukulia kuwa tofauti zetu si za hiari. Chukulia anayekuchukia hajapenda kukuchukia. Chukulia mengi ya yanayotokea kwa sababu ya uzembe wako, unayo nafasi ya kuyarekebisha.

Kumbuka amani na furaha yetu vyatutegemea sisi. Tusiwategemee wengine kutufanya tufurahi. Tupunguze matarajio kwa wengine. Tusiruhusu watu wengine kutunyima amani. Wajibu wa kujipa ama kujioondolea amani hauko kwa mwingine isipokuwa sisi. Uamuzi ni wetu wenyewe.

Maoni

  1. kaka big up it nimependa sana makala yako hii imenigusa kwa njia moja au ingine nimejifunza kitu hapa ubarikiwe sana na mungu akuwezeshe uendelee kutufunza asante

    JibuFuta
  2. Asante sana Anony na karibu sana

    JibuFuta
  3. Nimesoma sana kitabu cha Dalai lama na yeye anamsimamo kama wako na ushauri kama huo.
    Mimi mwanangu nikajaribu saana kuufuata ushauri huu, lakini mambo yakazidi, maaana huyu babu akazidi kuniona 'bwege' na kuzidisha matatizo ambayo yananitesa kimaisha.
    yeye hupenda wanawake, na kwa wakati mmoja anaweza kuhodhi zaidi ya watatu, sawa si ndio furaha yake, lakini sasa ina athir maisha yetu nyumbani kwa kukosa huduma muhimu tena nazungumzia malazi, kula, nguo na kadhalika, hiyo huduma nyingine nilisha ona hatari biashara nika funga. Hakujali sana kw vile yeye hana shida hiyo. Sasa hata mpango wa kuachana amekataa mimi niko tayari ili aendelee na tabia yake kwa vile nilishindwa kuibadili, na kuona napoteza muda wangu na kujinyima furaha maishani mwangu, kuliko kugombana na kununiana kila siku kheri ni mwache alivyo. simuulizi chochote ingawa anapata huduma zote pasi na hiyo moja bila yeye kutoa matumizi (mwenyewe nina kipato changu) sasa hapa utashauri vipi baba yangu? maana maji yeshafika kooni karibu na zama.

    JibuFuta
  4. Mtoa maoni hapo juu, asante sana kwa maoni yako. Sijawahi kusoma vitabu vya huyo uliyemtaja, nitafurahi kujua zaidi mawazo yake.

    Nikushukuru kwa mfano wa tatizo halisi uliouleta hapa. Kwamba, kubadili mtazamo wa namna unavyoliona tatizo hakukusaidia kulitatua tatizo husika! Nikiri kwamba tumezungumzia sababu za KUTOKUWA NA FURAHA na sio kutatua hivyo vinavyotunyima furaha. Hiyo hata hivyo haimaanishi kana kwamba ni ku-deny uwapo wa tatizo, hasha. Hiyo ilimaanisha kubeba jukumu la kujitafutia furaha yetu wenyewe katikati ya vingi vituondoleavyo furaha!

    Katika suala ulilolileta, kinachoshabihiana na maudhui ya leo ni wewe kushughulika na furaha yako mwenyewe. Kubeba wajibu wa amani yako mwenyewe, pasipo kutegemea "mabadiliko yoyote" kutoka nje (kwa mwenzako). Kwa maana nyingine, kukwepa kujidhuru kwa hasira, kuvunjika moyo, msongo wa mawazo na kadhalika kunakotokana na tatizo lililopo!

    Kufanya hivyo hata hivyo, hakutarajiwi kutatua tatizo lililopo (la mwenzio "kufurahia mahusiano nje ya uhusiano")!

    Ili kutatua tatizo hilo, itatupasa kwenda hatua zaidi ya kumtafutia "mgonjwa" wetu huyo matibabu ya kubaini chanzo hasa cha tabia hiyo (ambayo sisi twaiona mbaya, lakini yeye anaifurahia) ili kujua kwa nini anafanya anachokifanya. Kisha baada ya hilo (mgonjwa) atasaidiwa kuiona tabia hiyo kwa ubaya tunaouona sisi, na namna anavyoweza kuachana nayo!

    Kwa hiyo utaona "tiba" ya tatizo hilo inahitaji utaalamu zaidi kuliko matarajio na hukumu!

    Ninachoweza kukushauri kwa sasa ni kuonana na mnasibu nasaha (daktari wa tabia) akusaidie kuchunguza ugonjwa huo unaomsumbua mwenzako.

    Tukitaka basi kutumia maudhui ya mada ya leo katika suala lako, twaweza kusema yafuatayo:

    Kwanza yakupasa kumwona mwenzako kama mtu anayeyafanya hayo yote kwa msukumo ulio nje ya matakwa yake mwenyewe! Hili ni gumu kulikubali lakini ndio uhalisia! Ushahidi wa hili ni namna ambavyo mazungumzo ya kawaida yanavyoshindwa kutatua tatizo. Pili, yakupasa kumchukulia kama mgonjwa anayehitaji matibabu kuliko lawama na shutuma; Kiisha (kama nilivyotangulia kusema) utafute huduma ya matibabu ya tabia husika!

    Nasubiri kusoma mawazo ya wasomaji wengine katika hili! Asante sana.

    JibuFuta
  5. Mkuu sitaki kuharibu hili darasa maana umemaliza ila narejea tu hiyo sehemu ya mwisho;``Kumbuka amani na furaha yetu vyatutegemea sisi. Tusiwategemee wengine kutufanya tufurahi. Tupunguze matarajio kwa wengine. Tusiruhusu watu wengine kutunyima amani. Wajibu wa kujipa ama kujioondolea amani hauko kwa mwingine isipokuwa sisi. Uamuzi ni wetu wenyewe.
    Duuh, umemaliza mkuu! Shukurani

    JibuFuta
  6. Kwa mtu mweye uwezo, ni upumbavu mtupu kununa au kujisikia vibaya kwa kuwa Sheik Fulani bin Fulani amekasirishwa na mambo yangu.

    Lakini kwa mtu mdogo na asiekuwa na uwezo wowote, lazima atatetemeka na kuhuzunika eti amemgadhabisha Sheikh!


    Labda swali hapa, Mkuu, ni hili: SISI WENYE UWEZO, TUNAWASAIDIAJE WANYONGE ILI NAO WAPATE UHURU WAO JUU YA FURAHA NA DHAMIRI YAO?

    JibuFuta
  7. Mkuu Phiri, asante kwa changamoto hii muhimu.

    Nadhani unazungumzia tatizo la kutokujiamini. Mtu kujichukulia chini (low self esteem) kiasi cha kukosa furaha ya kufanya kile anachopenda yeye na badala yake kutumia muda mwingi kuwapendeza wengine. Huu ni ugonjwa.

    Hebu niwasikilize wasomaji wengine wachangie.

    JibuFuta
  8. Emu Three, asante sana kwa kupitia hapa. Darasa letu la kubadilishana maoni lisilo na mwalimu.

    JibuFuta
  9. Nice blog and good information

    JibuFuta
  10. i like it this blog information

    JibuFuta
  11. Thanks you for good information

    JibuFuta
  12. Ahsantee saanaaaa,
    Kwa ujumbe mzurii umenifunza kitu katika maisha yangu.

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia

Pay $900? I quit blogging