Raha ya kublogu ni uhuru wenyewe

Kwa mara ya kwanza nilisikia neno blogu kwa rafiki yangu aliyekuwa akijitolea kufundisha (volunteer) katika shule moja hapa nchini. Alinionyesha blogu yake na kwa kweli kama zilivyo za wazungu wengi, haikuwa na jambo la maana zaidi ya masimulizi ya hadithi zisizo na mashikio.

Nikafungua na yangu, ikifuata nyayo hizo hizo za porojo nyepesi nyepesi. Haikuwahi kuingia kichwani kwangu kwamba inawezekana mtu kuisoma. Nilikuwa na sababu nyingi. Kwanza, rafiki zangu wengi hawakuwa wamehamasika na matumizi ya teknolojia ya habari. Aidha, wachache walioipenda hawakuvutiwa na mambo ya habari habari, wao waliziita za kizee.

Nakumbuka tukitoka tuisheni za Makongo, tungeweza kupitia kwenye vioski vya mtandao (cafee) pale Mwenge kuchungulia hili na lile. Wakati mimi nikihangaika kusoma “templates” za blogu, wenzangu walikuwa, na mpaka leo, wanapenda kuangalia mambo flani ya ngono na udaku.

Lakini pili sikuwa na wazo kwamba blogu yaweza kuwa uwanja mpana wa kukutana na falsafa mbali mbali. Nilijua kwamba kwenye blogu huandikwa yale niliyoyaona kwenye blogu ya huyo rafiki yangu, mwandishi wa nyepesi nyepesi.

Pamoja na kuwa kwangu mwanafunzi wa Sayansi, watu tunaosemekana kuwa na uwezo mdogo wa kujieleza, nakumbuka kuwa na ugonjwa wa kupenda maandiko. Nakumbuka kuanzisha gazeti la shule ambapo mumo ningeweza kuanzisha mijadala ya kawaida iliyopata kuwa maarufu katika shule niliyosoma. Mwandishi mwenzangu sasa ni Mganga mtarajiwa.

Kupenda kwangu magazeti na kuandika andika hapo shuleni kulinikutanisha na makala za mtu mmoja aliyenivutia kwa kujadili mambo yaliyonisisimua sana. Alinifanya nisiache kutafuta nakala ya gazeti la Mwananchi kila Jumapili. Alikuwa ni fundi wa kueleza kwa unadhifu kile anachofikiri, kiasi kwamba wewe kama hadhira, hata kama ungekuwana haraka kiasi gani, usingedhubutu kuikatisha makala yake.

Alionekana kama mtu mwenye mwako wa moto ndani yake kuendesha ukombozi wa fikra za wanadamu wa jamii yake. Mwenye kusudi la kuwakomboa wenzake wengi kwa masuala mengi aliyodhani yanakwamisha kuendelea mbele. Nilipenda huduma yake hiyo.

Mtu huyo alikuwa Ndesanjo Macha. Ndesanjo alinivuta shati. Akateka akili na mawazo yangu. Nikafika mahali pa kuchana makala zake na kuzibandika kwenye ubao wa matangazo pembezoni mwa “gazeti” langu. Nilifanya hivyo nikijua kuwa wanafunzi wengi hawakuwa wakisoma magazeti. Hata hivyo, nikaja gundua kuwa zilikuwa zikiwatia uvivu mno jamaa zangu hao waliopenda kila kitu kwa “summary”.

Ndipo nikajikuta nikifanya mambo ya ajabu: Kuzisoma na kuchukua mawazo ya jumla na kuyatia katika “gazeti” langu. Ndesanjo Macha akawa mmoja wa wana safu wa “gazeti” hilo, mimi nikijipa “uhariri bubu” wa makala zake. Hata hivyo, huo ndio ukawa mwanzo wa mijadala isiyokoma katika mabweni ya wanafunzi wasomao Fizikia, Kemia na Baolojia pamoja na wengine wa Hisabati, vijana ambao jamii isingewatarajia kupenda mijadala ya kijamii. Watu ambao walijadili mofolojia ya mende na vyura, sasa waligeukia mambo ya siasa, utamaduni na jamii.

Basi, nakumbuka kufanya majaribio kadhaa ya kuandika makala katika gazeti kongwe la Rai. Nilikuwa nimevutiwa na hoja za Padri Karugendo. Pamoja na kuhangaika na posta mara nyingi, nakumbuka makala yangu kutokea si zaidi ya mara moja katika gazeti hilo. Ukweli ni kwamba sikupenda hata siku moja kuufanya uandishi kuwa taaluma yangu hasa, lakini ni ile hamasa tu ya kupenda mijadala ilinisukuma kujaribu kushiriki mijadala mingi hapa na pale kila palipopatikana nafasi.

Ni katika “ulevi” huu wa maandiko, ndipo nilipokutana na ukurasa wa Jikomboe. Ilikuwa ni siku moja nikisoma “Gumzo la Wiki”, nilipokutana na maandishi mwishoni mwa makala hiyo yakionyesha kuwa Mwandishi anayo blogu. Nilifurahi! Na huo ndio ukawa mwanzo wa mapinduzi mapya. Sikuwa na haja ya kusubiri makala moja baada ya juma. Nikabaini kuwa naweza kujipatia “mistari ya ufahamu” moja kwa moja katika jikomboe.blogspot.com. Lakini pia kujifunza zaidi kuhusu blogu kupitia masomo kwa wanablogu wapya. Basi ndio ukawa mwanzo mpya. Mwanzo wenye uhuru. Mwanzo wa ukombozi mpya wa fikra.

Siwezi kuacha kupata nakala ya gazeti la Mwananchi (hususani Jumapili), pamoja na kwamba waandishi wake wengi leo hii ni wanablogu wazuri. Kwani hata hivyo sikumbuki ni nakala ipi ya gazeti hilo nimewahi kuikosa tangu nimeanza kulisoma miaka mingi iliyopita.

Kublogu katika mazingira ya hapa nyumbani ni kazi inayohitaji moyo. Tunayo matatizo ya umeme. Lakini pia, gharama za huduma hii ni kubwa kwetu sisi wananchi wa kawaida na hasa “wa-kusoma”. Najua kuwa wapo wa- Tanzania wengi wangependa kublogu, gharama zinakuwa ni kikwazo kimoja wapo, kinachowazuia kufanya hivyo kwa
ufasaha.

Kwa mwanachi wa kawaida asiyefanya kazi katika Ofisi yenye mtandao, atagharimika sana “kuwepo on line” mara kwa mara. Gharama ni kizuizi kikubwa. Usishangae kuona mtu akitokomea kichakani na kurudi mtandaoni baada ya majuma kadhaa ya ukimya.

Lakini pia nimefanya utafiti bubu miongoni mwa vijana ninaohusiana nao hasa wale walio katika Taasisi za Elimu (ya juu kwa mfano) kwamba wanatumia muda mwingi sana katika kompyuta karibu kila siku. Lakini bahati mbaya ni kwamba wengi wao wanafuatilia mambo ambayo hayawaletei faida katika akili zao. Wanajilisha taka taka nyingi zisizo na msingi kwa sehemu kubwa ya muda wao. Hapa utaona ya kwamba lipo tatizo jingine zaidi ya kikwazo cha gharama za mtandao. Na hili linaweza kuwa kubwa kuliko tunavyofikiri.

Nimekuwa “balozi mdogo”wa blogu kwa wengi ninaokutana nao hasa vijana. Wengi wanajiunga pamoja na kikwazo cha muda wa huzihudumia, lakini inatia moyo kwamba wapo. Na si wachache. Lakini hata hivyo, inasikitisha kuwa wapo wanaojiunga na kuitumia blogu kwa malengo yasiyokusudiwa. Nakumbuka Ndesanjo amewahi kulieleza hili mara kadhaa. Kwamba blogu zitusaidie wa-Afrika kupeana changamoto. Tujikomboe.

Kujikomboa huku hakuwezi kuja kwa kujidai kuwa na mawazo yanayofanana. Kwamba kila anayetoa maoni chini ya makala yako, ni lazima aseme “ Naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja!...” Ni muhimu tutofautiane ili tujikomboe. Najua wapo hawapendi kuambiwa mbadala wa mawazo yao. Pengine kwa kuamini kwamba hawawezi kukosea! Hiyo ni sawa pia. Lakini, nadhani, ni vyema kukubali kukosolewa na wengine. Tofauti ya mawazo ni faida. Maana kwa kila mwanablogu mpya anayejiunga, tunaongeza tofauti ya mawazo na falsafa. Kila moja anakuja na mawazo yake.

Bahati mbaya wapo watu wanaokuja na tofauti kubwa ya mawazo kiasi cha kutia shaka. Yupo rafiki yangu mmoja, mwanafunzi wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano. Nilimweleza kuhusu blogu nikidhani angeweza kuwa changamoto sana katika jumuiya ya wanablogu kama alivyo MK. Kumbe nilifanya kosa. Bwana huyu kwa kutumia taaluma yake hiyo, akaamua kuanzisha blogu yenye kujaa mambo ya ngono yenye umaarufu wa kutosha katika Taasisi hiyo alimo, na inafurahiwa sana na wanafunzi. Ni ajabu kwamba wanafunzi hawa ni wasomi tena wa elimu ya juu. Na ndio waliotumwa na jamii kuhemea kwa manufaa ya jamii yenyewe.

Sipingi watu kufanya wanayoona ni sawa katika nafsi zao. Mwenye kupenda matusi ni haki yake atukane apendavyo. Mwenye kupenda kukashfu wenzake, aachwe afanye hivyo kwa uhuru. Kila mtu anao uhuru wa kufanya apendavyo kuridhisha nafsi yake.

Lakini kutumia muda mwingi kwa “starehe” ambazo hatudhubutu kujulikana kwamba tunazipenda, si jambo jema. Ingefaa teknolojia itumike kwa uhuru na uwazi kila inapobidi, kuliko kujificha kwenye gunia, na kuandika mambo ambayo usingependa watu wajue kuwa uliyeaandika hayo, ni wewe.


Ni kweli kwamba sasa hatulazimiki tena kusubiri wahariri kutuamulia ni nini tukisome katika magazeti yao ya habari (za uongo). Kile kiambaza cha mawazo-huru kwa sisi wananchi wa kawaida, hakipo. Wote tu wahariri wa habari zetu wenyewe. Mbadilishano wa taarifa kati ya mwandikaji na wasomaji wake ni wa hali ya juu. Hilo halina ubishi.

Lakini je, tuko tayari kukabiliana na changamoto-huru, au tunataka kuendeleza ile dhana ya mhariri hakosoleki? Je, tuko tayari kuvumilia mawazo ya watu wengine ambayo mara nyingine yatakuwa tofauti sana na vile tuvijuavyo? Je, tuko tayari kuihubiri teknolojia hii hata kwa watu ambao wanaitumia kinyume nyume? Je, tuko tayari kumsaidia yeyote anayekwenda kombo kwa uwazi, na kumrejesha wkenye mstari wa mapambano? Hiyo ndiyo changamoto tuliyonayo.

Maoni

  1. Yaap hongera saaana mzee, mambo yako kama ulivyosema kwa hakika umeamua kujitosa mzima mzima katika fani nimekukubali.

    Kitu kimoja umekihilight vijana kupenda kubrowse kurasa za ngono aisee hiyo ni kweli kabisa hakuna ubishi, hii ni dhahiri na kama vijana hatutaachana na hili tutajikuta tukitumikia ngono za mtandaoni badala ya kuvuna maarifa.

    Ni wajibu wetu mimi wewe, yule na mwingine na kadhalika kulishughulikia hili.

    JibuFuta
  2. Charahani,
    Asante sana kunitembelea. Ni muhimu kila mmoja afaanye wajibu wake kutangaza mambo lukuki ya maana yanayoweza kupatikana mtandaoni. Hii tabia ya kupoteza wakati tu mtandaoni wakati nchi yetu ni masikini, nadhani umefika wakati tuipige vita kwa nguvu.

    Nnajua Charahani unafursa kubwa ya kufanya hili kuliko wengi wetu tunaoibia ibia vibanda vya mtandao.

    JibuFuta
  3. Swala la ngono kutafutwa mtandaoni ni jambo linaloongoza dunia nzima.Chakusikitisha ni pale linavyo tawala na kuzuia udadisi wa mambo mengine mtandaoni. Mimi naamini jambo hili linawadaka sana watu kwa kuwa ni jambo ambalo jamii zilizo nyingi hapa duniani haliongelei ngono kiuwaziwazi.Hivyo watu wana imagination za ajabu ajabu ambazo wanajaribu kupata majibu katika njia hii mpya ya mtandao. Mimi naamini asilimia kubwa ya watu huacha au kupunguza kabisa udadisi wa ngono baada ya kugundua hakuna cha ajabu sana wakionacho.Hivyo cha muhimu ni kukumbushana tu kuwa maisha na maswali mengine mengi yamkabiliayo binadamu yana majibu mengi tu mtandaoni kama mtu ni mdadisi.Na naamini wote tunamambo mengi tutakayo kujua zaidi ya ngono ambayo twaweza kupata majibu mtandaoni. Lakini nashukuru kuna blogu yako Bwaya ambayo hunishibisha maarifa. Asante!

    JibuFuta
  4. Kitururu kasema kweli kuhusu watu kupunguza kasi ya kufuatilia masuala ya ngono mtandaoni baada ya muda fulani. Utafiti kuhusu tabia za matumizi ya mtandao unaonyesha kuwa watu wanapoanza kutumia teknolojia hii hukimbilia kwenye mambo ambayo huonekana kuwa ni mwiko katika jamii kama kutazama picha za ngono. Halafu baada ya muda wanachoka na kuhamia kwenye mambo mengine. Sio wote. Ila tabia za watumiaji wengi wa mtandao zinaonyesha hivyo. Hata kama hawaachi kabisa, basi huwa kuna kupunguza kasi na kuanza kutazama mambo mengine yaliyoko kwenye kisima hiki cha elimu na habari.

    JibuFuta
  5. Christian umenikumbusha mambo ya kale! Enzi za Mkwizu, mwalimu wetu wa Chemistry: "Nyie vijana msifajifanye mnajua...kondoo wanamjua mchungaji...fuateni mafundisho ya mchungaji wenu".

    Juzi nilikutana naye bsi kumbe analikumbuka sana lile darasa. Nasikia hapajawahi kuwapo wazo la gazeti kama mlivyokuwa mkifanya na Mwimbe, tulipoondoka ndio ikawa basi.

    Umenikumbusha siku ile umekuta jamaa wamefungia gazeti la Rai "vile vimbuzi"
    (unavikumbuka?) basi ikawa sheshe. Nimejifunza vingi kwa maisha yale.

    Nimesoma hii story nkakumbuka ile column ya huyu jamaa ambaye kumbe yuko mtandaoni kajaa tele. Nshapata mahala pa kutulia.

    Tuwasiliane.

    Monita wako,
    PCB class.

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Uislamu ulianza lini?

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia