Nani Awezaye Kutuletea Mabadiliko Tunayoyataka?

Ukisikiliza mazungumzo ya wa-Tanzania  –iwe vijiweni, mitaani, mitandaoni ama kwingineko –ni wazi wengi wetu tunayo hamu ya mabadiliko. Tuna shauku ya zama mpya. Shauku hiyo ya mabadiliko imetufanya wengi wetu tutumie muda mwingi kutafuta watu tunaohisi ‘wanatukwamisha.’ Ni hivyo kwa sababu tumejijengea dhana kwamba ili kupata mabadiliko tunayoyataka tunahitaji watu maalum wenye uwezo wa ‘kutuletea maendeleo’. Kwa hiyo ni kama tunasubiri wakombozi fulani fulani waje kutubadilishia mfumo tunaoamini ndio tatizo.

Mfumo ni nani?

Wananchi wengi tunapozungumzia mfumo tunafikiria ‘yanayofanywa na wenye mamlaka ya kutuletea maendeleo/mabadiliko.’ Tunafikiri tatizo letu kubwa ni watu wengine na hivyo mara zote tunajiweka upande wa kuwalaumu. Tunadhani ikiwa wengine (wenye mamlaka) wangefanya yale tunavyotamani yafanywe basi hali ya mambo ingebadilika. Kwa hiyo mara zote tunakuwa na orodha ndefu ya watu wa kuwanyooshea kidole isipokuwa sisi wenyewe.

Kwa mfano, mwalimu anapofelisha wanafunzi wake analaumu ‘mfumo wa elimu.’ Anatumia nguvu nyingi kuthibitisha kwamba tatizo haliwezi kuwa yeye bali watu wengine anaowaita mfumo. Kwake, tatizo ni mitaala isiyofaa, serikali isiyofanya wajibu wake, wanafunzi wasio na sifa na kadhalika. Analaumu wengine.

Ndivyo tunavyojadili matatizo yetu. Kila anayeshindwa kufikia matarajio ya jamii au anayedhani mambo hayaendi ipasavyo jibu ni jepesi: mfumo. Wananchi (tunaoitwa wa kawaida) tunashinda vijiweni ‘kuchambua’ namna siasa zetu zinavyoturudisha nyuma. Tunatumia masaa mengi kuwalumu watu tusiowajua. Tunaishi kwenye mazingira machafu lakini hatuchukui hatua kwa sababu ‘mfumo’ wa kusafisha takataka zilizotapakaa kwenye makazi yetu haufanyi kazi. Tunasubiri ‘mfumo’ uje utuzolee takataka zinazoathiri maisha yetu. Tusipowaona ‘watu wa mfumo’ wanaoweza kutupa matumaini ya kutatua matatizo yaliyo ndani ya uwezo wetu basi tunakata tamaa.

Hatuwezi kuchukua hatua zilizo ndani ya uwezo wetu?

Natambua umuhimu wa hicho tunachopenda kukiita mfumo. Natambua umuhimu wa viongozi wetu kuongoza harakati za kuhamasisha utatuzi wa changamoto zinazotukabili. Hata hivyo, pamoja na umuhimu wa mfumo, napendekeza sisi wananchi kutambua umuhimu wa kuchukua hatua zilizo ndani ya uwezo wetu kuleta mabadiliko tunayoyataka. Tubadilike.

Kuchukua hatua maana yake kabla ya mwalimu kulalamikaia mfumo wa elimu, ajiulize yeye amefanya wajibu wake ipasavyo? Amejibidiisha kutatua changamoto za wanafunzi zilizo ndani ya uwezo wake? Kama mwalimu anashindwa kushughulikia matatizo madogo yanayowazuia angalau wanafunzi wake kumi kuelewa somo lake, anawezaje kuzungumzia matatizo ya mfumo wa elimu wa nchi nzima? Kwa nini, kwa mfano, kwa kushirikiana na uongozi wa shule, kijiji na kata anamoishi, asijenge mfumo unaweza kufanya kazi darasani kwake? Hili haliwezekani?


Wananchi wakishiriki kusafisha mazingira yao. Picha: wazalendo25.blogspot.com
Ukweli ni kwamba kila mwananchi anaweza kuleta mabadiliko anayoyataka ikiwa atatambua na kutimiza wajibu wake kikamilifu. Hili linahitaji kubadili mtazamo. Kwa kubadili mtazamo na kuamua kuanza kuchukua hatua badala ya kutafuta makosa ya wengine, tunaweza kuleta mabadiliko. Hatuwezi kubadili chochote kwa kushinda kwenye mitandao ya kijamii, vijiweni, korido za maofisi kulalamikia watawala tunaowaona kwenye televisheni. Tunaweza kuleta mabadiliko makubwa kwa kila mmoja wetu kutambua mchango wake katika kuleta tofauti anayoitaka.

Viongozi wetu wa mitaa/vijiji/kata tunawajua na tunaweza kuwafuatilia kwa karibu. Tunaweza kushirikiana nao kufikiri namna bora ya kujenga mfumo utakaofanya kazi kwenye maisha yetu halisi. Sote kwa pamoja kuanzia chini tunaweza kushirikiana kujenga vimfumo vidogo vidogo vya kubadilisha hali ya mambo katika maeneo tunayoishi. Tukifanya hivyo, tutarahisisha kazi ya wale tuliowapa dhamana ya kujenga mfumo wa kitaifa utakaoakisi mifumo tuliyojenga sisi wenyewe kuanzia chini. Hayo ndio mabadiliko ya kweli. Mabadiliko ya mtazamo.
Twitter: @bwaya

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Pay $900? I quit blogging

Haiba ni nini?

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Heri ya mwezi mpya!