Kujenga Uwezo wa Kufanya Maamuzi kwa Mtoto

Unajisikiaje mzazi unapogundua mtoto ameanza kujifunza tabia zisizofaa? Inaumiza, kwa mfano, kuona mtoto anaanza kujifunza wizi, kudanganya na hata kutokuwa na uwezo wa kujisimamia mwenyewe bila uangalizi wa karibu.   


Tafiti za malezi zinaonesha kuwa, kwa kiasi fulani, tabia hizi huchangiwa na kutokumpa mtoto nafasi ya kufanya maamuzi yanayohusu mambo yake mapema. Labda unaweza kujiuliza mtoto anaweza kufanya maamuzi gani katika umri ambao hata uwezo wake wa kufikiri bado ni mdogo?

Maamuzi ni kuchagua

Kufanya maamuzi ni kumpa uwezo wa kuchagua mambo rahisi kabisa bila kumfanya alazimike kufuata matarajio ya wengine ambayo pengine hayaendani na matarajio yake. Kwa mfano, kumpa mtoto nafasi ya kuchagua kifaa kipi angependa kukitumia kuchezea ni kumwezesha kufanya maamuzi yanayolingana na uwezo wake.

Maamuzi hujenga kujiamini

Kumfundisha mtoto kufanya maamuzi yake humjengea uwezo wa kujiamini kungali mapema. Kujiamini kumethibitika kumsaidia mtoto kuwa na subira hata atakapokuwa mtu mzima.  Kwa hakika, mambo mengi tunayoyafanya kama watu wazima yanategemea kwa kiasi kikubwa sana uwezo wetu wa kuwa na subira. 

Bila subira, kwa mfano, hatuwezi kudhibiti hasira, hatuwezi kuheshimu makubaliano na hata kuwa na nidhamu ya matumizi ya fedha. Kimsingi, subira ina nafasi kuwa katika maisha yetu na kwa kweli inatokana na uwezo wetu wa kufanya maamuzi. 

Picha: hoas.org


Utafiti wa ‘Marshmallow’

Mwanasaikolojia Walter Mischel aliwahi kufanya utafiti kupima nguvu ya maamuzi ya subira kwa watoto wa miaka minne. Mischel aliwapa watoto vitu vitamu viitwavyo marshmallow –mfano wa pipi kwa mazingira yetu –ili kuona kama watoto wangeweza kufanya maamuzi ya kujinyima kile wakipendacho kwa hiari yao. Watoto waliambiwa wangeweza kula pipi hizo kama wangetaka lakini kama wangesubiri mpaka atakaporudi wangepata ‘pipi’ zaidi kama takrima ya kujinyima.

Matokeo yalionesha watoto wachache waliweza kujizuia. Wengi walikula ‘pipi’ bila kungoja. Mischel aliwafuatilia watoto hao kwa miaka mingi baadae na kugundua wale waliongoja walikuwa na mafanikio makubwa shuleni na hata katika maisha.

Wenzao walioshindwa kufanya maamuzi ya kungoja hawakuwa na mafanikio na wengi waliishia kuwa na tabia zisizofaa kama wizi, matumizi ya dawa za kulevya na walipata matatizo katika mahusiano ya kimapenzi na kadhalika. Tafsiri rahisi ni kwamba kujengwa kimaamuzi mapema na kuwa na subira kunahusiana kwa karibu na mafanikio ya mtu.

Tunachoweza kufanya

Tunashauriwa kuwasaidia watoto kushiriki katika maamuzi madogo yanayolingana na umri wao tangu wakiwa wadogo. Kwa mfano, tunaweza kuwaruhusu watoto kuchagua nguo wanazopenda kuvaa, kuwashirikisha kupanga ratiba za michezo yao ili kuwafanya waweze kujiona kama watu wanaoweza kufanya maamuzi ya kujisimamia tangu mapema.

Kadhalika, tunaweza kuheshimu hisia za watoto wetu tangu wakiwa wadogo ili kuwajengea imani na uwezo walionao. Kwa mfano, wanaporipoti hisia za maumivu tusiwalazimishe kuamini vinginevyo kwa lengo la kuwafanya watulie. Kuwajengea uwezo wa kukubali hisia hasi walizonazo ni njia muafaka zaidi ya kuwasadia kukabiliana nazo na hukuza uwezo wao wa kuamua mambo yanayowahusu tangu wakiwa wadogo.

Kwa hakika, upo umuhimu mkubwa wa kuwasaidia watoto kufanya maamuzi yao kulingana na umri wao. Maisha yao ya utu uzima yatategemea sana namna wanavyofanya maamuzi. Tunao wajibu wa kuwakuza kimaamuzi tangu wanapokuwa wadogo. 

Unafahamu njia nyingine za kuwasaidia kukuza uwezo huu?


Niandikie: bwaya@mwecau.ac.tz, 0754 870 815

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Mambo ya Kuzingatia Unapoandika Wasifu wa Kazi (Curriculum Vitae)

Uislamu ulianza lini?

Tumia Mbinu Hizi Kuelewa Unachokisoma -3