Kuogopwa kwa wanawake wenye mafanikio na dhana ya kichwa cha familia

NILIPATA fursa ya kushiriki mjadala mmoja kwenye mtandao wa Facebook leo mchana. Mjadala wenyewe ulianzishwa na Samuel Sasali, ambaye kwa maoni yangu ana uwezo mkubwa wa kuchokoza mada zinazohusu maisha yetu ya kila siku. Hoja iliyokuwa mezani ililetwa kwa njia ya mchoro unaoonesha changamoto anazokabiliana nazo mwanamke anapofanikiwa kielimu. Kwamba kadri mwanamke anavyokwea ngazi ya mafanikio ya kielimu, ndivyo wanaume wanavyozidi kumkimbia.

Tatizo ni wanaume au wanawake?

Kuna ukweli kwamba katika jamii yetu wanawake wenye elimu kubwa wanakuwa na wakati mgumu sana kupata mahusiano ya kudumu na watu wanaowatarajia wao tena kwa wakati. Na hata wanapoyapata wengi tunakubaliana kwamba mahusiano hayo mengi hukabiliwa na mawimbi na dhoruba za hapa na pale na wakati mwingine mahusiano hayo huharibika. 

Wanaume wanadai kuwaogopa wanawake hawa kwa sababu pamoja na urembo na unadhifu wa akili na mwili, inasemekana hawana nidhamu ya ndoa. Wanapopata elimu, inadaiwa hawawi tayari kuwa chini ya utawala wa mwanaume. Hiyo ndiyo hofu kuu ya wanaume inayowazuia kuanzisha na kudumisha mahusiano na wanawake wenye mafanikio iwe ya kielimu au kiuchumi.

Ukiangalia vizuri utaona kuna ukweli fulani kuwa wanawake wenye mafanikio mara nyingine hushindwa kuwa tayari kunyenyekea chini ya mamlaka ya mwanaume. Wakishafanikiwa, huanza kujiona wana haki ya kufanana nawanaume katika nyanja zote za kimaisha. Hali hii haitakiwi sana na wanaume wengi wanaohitaji kujiona ni kichwa halisi cha familia kwa maana ya kusikilizwa, kukubaliwa na kupewa heshima hata kama hawatimizi wajibu wake. Haya ndio mambo yanayotafsiriwa na wanaume kuwa ndio unyenyekevu.

Kwa nini anakimbiwa? Picha: Chanzo hakijulikani. Imetumika bila ruhusa
 Hata hivyo, dhana hii ina matatizo mengi. Kwa mfano, si wakati wote tatizo linakuwa ni la wanawake wenye mafanikio. Wapo wanawake wasio na mafanikio yeyote lakini wanawatisha wanaume. Ndio hizi wakati mwingine huwa ni hisia tu ambazo zikiaminiwa hugeuka kuwa kweli. Na kwa kweli ukichunguza kwa makini migororo mingi ya kimahusiano utagundua kuwa tatizo kubwa ni hali ya kutokujiamini waliyonayo wanaume na sio walivyo wanawake.

Ni ukweli kwamba wanaume wengi wana matatizo ya kuhusiana na nafsi zao wenyewe hali tunayoweza kuiita umaskini wa nafsi unaowafanya washindwe kuhusiana bila masharti na wanawake na wakati mwingine kuwabebesha wanawake mizigo wasiyostahili. Mfano moja wapo ni hili tunalolizungumza la kutishwa na mafanikio ya wanawake. Ni tishio hili la mafanikio ya mwanamke ndilo linalowafanya wanaume wengi kutafuta mahusiano na wanawake wasio na elimu, wenye utegemezi wa kipato ili waweze kuwatawala na kuwadhibiti. Wanatumia dhana ya kichwa cha familia kinyume na uhalisia.

Naomba sasa nioneshe kwa ufupi namna ambavyo tatizo haliwezi kuwa mafanikio ya mwanamke bali udhaifu wa mwanaume unaowafanya watishwe na mafanikio ya wanawake.

Kichwa cha familia

Tuanze na dhana ya kichwa cha familia inayopendwa mno na wanaume. Kuwa kichwa cha familia maana yake si ubabe wala udikteta wala uwezo wa kumdhibiti mwanamke bali uwezo wa kuwa mfano wa yale yanayopaswa kufanyika katika familia, uwezo wa kuonesha njia na kuweka mazingira sahihi ya wanafamilia kuhusiana vyema na nafsi zao na hivyo kuhusiana vyema wao kwa wao.

Kwa kutambulika kama kichwa cha familia, mwanaume ndiye anayepaswa kuwa mtu wa kwanza kuwa na mahusiano mema na nafasi yake mwenyewe. Hapaswi kuwa mtu mwenye mahusiano ya mashaka na nafsi yake, anayehangaika kutafuta amani inayotoka nje. Hiyo ni sawa na kusema mwanaume asiyejiamini wala kuwaamini wengine; mwanaume mwenye wasiwasi na nafsi yake mwenyewe; mwanaume anayetafuta furaha kwa gharama ya wengine, ataishia kuanzisha mahusiano kama jitihada za kuficha mapungufu yake kwa kutumia vibaya dhana ya kichwa cha familia.

Na kawaida, mwanamme wa jinsi hii hufikiri kuwa kichwa cha familia maana yake ni kuwa na fedha zaidi, elimu zaidi, akili zaidi, umri zaidi na kadhalika ili avitumie vyote hivyo kama silaha ya kujihami na tishio la mwanamke. Sasa mtu unajiuliza iweje mwanaume ambaye ni kichwa familia atumie elimu, fedha, hadhi, ujuzi, na kila aina ya mbinu kumdhibiti mwanamke? Huu si udhaifu? Hapa chini nitajaribu tusaili sifa tano za mwanaume mwenye mahusiano duni na nafasi yake, sifa zinazomfanya ashindwe kuwa tayari kulipa gharama za kuwa kichwa halisi cha familia na hivyo kujikuta akiwakimbia wanawake wanaojitambua. 

      1) Hapendi kukosolewa, ila ni mkosoaji mzuri
Mwanaume wa aina hii huwa anajua fika anao udhaifu fulani asiopenda wengine waujue. Kwa hiyo hapendi kukosolewa kwa sababu lugha ya kumkosoa hutuma ujumbe unaosisitiza hisia hasi za nafsi alizonazo tayari.Faraja yake ni kuona wengine wakikosolewa kwa hiyo ni shabiki wa kuwapiga vijembe na kuwafanya wengine wajisikie vibaya. Hawezi kujisikia vyema kuwasifia wengine. Anatishwa na furaha ya wengine. Hata hivyo, hatusemi kwamba mtu hatakaa akosoe. Lakini inapokuwa tabia, kwamba kila kitu lazima ukitolee makosa wakati huna suluhisho, tunajiuliza afya ya nafsi yako.

    2) Hutishwa na mafanikio ya wengine, hushindana bila sababu
Hapendi kuona wengine wanamzidi. Ni mtu wa kupambana na watu anaodhani wanatishia heshima yake. Wakati mwingine hushindana hata kwa vitu vidogo vidogo ambavyo usingedhani vinahitaji ushindani. Lengo ni kujitutumua kwamba na yeye anaweza. Ni kweli binadamu kwa asili ni mshindani lakini sio kwa kiwango cha kujenga kiambaza na watu ambao hata kihalisia hawakutishi na wakati mwingine hawana habari na wewe. 

     3) Mwongeaji/muwazi akifanikiwa, msiri asipofanikiwa
Hawa ni aina ya wanaume ambao ukiwa nao ni kama wanataka uwe msikilizaji wa majigambo yao. Mwanaume wa namna hii haishi kuongea/kusema. Na maongezi yake mengi ni mambo yake binafsi, "mimi nili, mimi nina, mimi nita, mimi sita". Ni kweli tunapenda mafanikio lakini si kwa kiwango cha kutamani kupata vipindi maalum kwenye televisheni kusema tulivyofanikiwa. Hata hivyo, si wakati wote mwanaume wa jinsi huwa muwazi. Mambo yanapokwenda asivyotarajia, huwa msiri. Na wakati mwingine hutumia uongo ili kuficha fedheha ya kuonekana hajafika anakokutaka au huwasingizia kuangushwa na wengine.

      4) Hakubali makosa yake, ana visasi na waliomkosea
Kama una rafiki wa kiume ambaye akikosea si mwepesi kukubali makosa, na tena wakati mwingine unalazimika kukiri mambo unayojua fika si makosa yako, basi huyo ndiye mwanaume tunayemzungumzia hapa. Ukikosea, ni mwepesi kulaumu na kurejea makosa ya nyuma. Hawa ndio watu wanaoweza kununa wiki nzima kama jitihada za kukwepa kuwajibikia makosa na kuukabili ukweli. Ni watu wa kulipa visasi na wakati mwingine wana vinyongo na watu.

       5) Ana wivu wa kimapenzi, ana dharau
Kutokujiamini kunamfanya awe mtu wa kushuku na kuhisi hisi uwepo wa mtu wa tatu anayevizia mahusiano yake hata kama yeye mwenyewe si mwaminifu. Ni shauri ya kutokujiamini kunakomfanya asiwe mwepesi kuamini mtu. Na wakati mwingine huwa na mahusiano ya kimapenzi na watu wengi kutafuta faraja bandia. Sasa ili kupambana na kutokujiamini kwake, wakati mwingine ni mtu anayependa sana kujitambulisha na watu wenye hadhi anayoitaka yeye. Watu maarufu. Hilo unaweza kulibaini ukiwa naye karibu kwa sababu hakawii kudharau watu anaowaona hawana hadhi anayoitaka yeye.

Gharama za kuhusiana na mwanaume huyu

Sijavipitia vielezi vyote kwa lengo la kufupisha makala. Kwa kifupi hali hii ya kutokujiamini, inayotokana na mahusiano mabovu na nafsi yake, huwa ni matokeo ya malezi na tajiriba za kimaisha zinazojenga mitazamo, imani na tabia zisizohimiza mahusiano sahihi na nafsi. Kumridhisha mwanaume wa namna hii, anayehangaika kuhusiana na nafsi yake mwenyewe, haiwezi kuwa kazi nyepesi. Na kwa kweli mwanamke anayeishi na mtu huyu ana jukumu kubwa la kulipa gharama ya kumfanya ajisikie vizuri kwa namna nyingi.

Kwanza, itambidi mwanamke asiwe na wasifu bora kumzidi mumewe. Asiwe amesoma, asiwe na pesa, asiwe maarufu, asiwe na kazi nzuri inayomzidi mwanaume na kadhalika. Ni kama tulivyoona kwamba mwanaume huyu huyatafsiri mafanikio ya wengine kama kushindwa kwake ikiwa ni pamoja na watu wake wa karibu. Na hii ndio sababu wengi huishia kuwa na mahusiano na wanawake wenye mafanikio yasiyozidi waliyonayo wao. Ndio maana unaweza kushangaa mtu ana PhD, amekutana na wanawake wangapi wasiofaa katika safari yake ya kielimu kiasi cha kuishia kuoa mwanamke asiyejua kuandika wala kusoma?

Kingine, kama utamzidi, fahamu utawajibika kuhakikisha kwamba hilo halionekani. Itakupasa kufanya jitihada za kumfanya ajione amefanikiwa, anajua, anaweza siku zote daima dumu. Kwa lugha nyingine usifurukute wala kuonesha una weledi fulani ndani yako. Hii si kazi rahisi hata kidogo na inadai gharama ya kujikana nafsi na hadhi yako, maana tunajua, binadamu tunafurahia mafanikio.

Hiyo ndiyo kusema, itakubidi kama mwanamke 'sahihi' kwake kukwepa mazingira ya kumkosoa. Hata unapohisi anakosea, itakulazimu kumwacha aendelee na makosa yake hata kama unajua yatawaathiri nyote. Lengo ni kuondoa uwezekano wa kumfanya ahisi anadharauliwa. Kama ni lazima kushauri, basi lugha iwe inamfanya aone maoni hayo ni yake na yamejengwa kwenye mawazo yake.

 Kadhalika, hisia zake za wivu zitakulazimu kumpa nafasi ya kukufahamu ipasavyo ili akuamini na kupunguza wasiwasi  wa kudanganywa au kuachwa. Hapa hatusemi mwanaume anayejiamini hahitaji uwazi kwa maisha ya mwanamke wake, lakini uwazi huu unavuka mipaka kiasi kwamba kama angekuwa na uwezo hutamani kukufuatilia kwa CCTV ili kujua uliko na unafanya nini na nani na dakika ipi.

Na kwa sababu tumeona ni mzito wa kusamehe na ni mtu wa visasi, hiyo ina maana kwamba kama 'mwanamke sahihi' utawajibika kuubeba msalaba wa lawama wakati wote hitilafu za kimahusiano zinapotokea. 

Ni sahihi mwanamke kubeba mzigo?

Kama tulivyoona, huu kwa hakika si mzigo mwepesi kwa mwanamke wa kawaida anayeingia kwenye mahusiano kwa matarajio ya kupata utoshelevu na mapenzi ya mume wake. Kumbuka, katika mahusiano, mwanaume ndiye anayewajibika kubeba ‘mzigo’ wa kuwajibika ili kuweka mazingira ya mwanamke kujisikia malaika. Huko ndio kuwa kichwa kwa maana halisi ya uongozi wa mahusiano. Lakini kwa hali ya kawaida, uongozi huu haiwezekaniki katika mazingira ambayo mume mwenyewe anayepaswa kubeba mzigo huo ndiye huyu tunayemjadili hapa.

Kabla sijahitimisha, niseme moja kwa moja kwamba kabla hujaanzisha mahusiano na mwanaume mwenye sifa tulizoziona hapa ni vyema kupata msaada wa kitaalam kumsaidia abadilike kwanza. Vinginevyo, utajikuta unabeba mzigo wenye uzito wa msalaba. Changamoto, hata hivyo, ni kwamba hata anaposhauriwa akamwone mtaalam wa tabia, hutafsiri ushauri huo kuwa dharau na kutokuamini uwezo wake. Hilo linashangaza kwa sababu huamini anajua hata kama hajui na jaribio lolote la kumwelekeza kwenye maarifa anayoyahitaji, atayatafsiri kama kudharauliwa. 

Katika kuhitimisha, tunaweza kusema mwanaume imara, mwanaume anayehusiana vyema na nafsi yake, mwanaume anayejitambua na kuelewa wajibu wake, hatishwi na uimara wala mafanikio ya mwanamke. Anapokuwa imara, mwanaume huwa na uwezo wa kulipa gharama za kuhusiana na mwanamke yeyote, bila kujali mafanikio aliyonayo mwanamke huyo. Ikiwa hivyo, hapata shida kuelewa kuwa silaha pekee inayofaa 'kumtawala' mwanamke yeyote ikiwa ni pamoja na yule mwenye mafanikio, ni kumpenda kwa bidii na kumwekea mazingira ya kujiona mtu mwenye kuthaminiwa kuliko chochote. Ni wanawake wachache sana wenye uwezo wa kupambana na sihala hii.

Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba mwanamke hahitaji kulipa gharama. La hasha. Mwanamke, kadhalika anahitaji kuhakikisha anajitambua, anahusiana vyema na nafsi yake na hivyo kutambua majukumu yake katika mahusiano, bila kujali mafanikio au kushindwa kwa mume wake.Vinginevyo, ni kweli, kadri anavyofanikiwa ndivyo anavyojiwekea mazingira ya upweke.

christianbwaya@gmail.com

Maoni

Zilisomwa zaidi wiki hii...

Mambo Yanayoweza Kugusa Moyo wa Mwanamke-1

Maana ya Saikolojia na Nafasi Yake Katika Jamii -1

Haiba ni nini?

Tabia za Mtoto wa Miaka 0 – 3 Kimahusiano na Kihisia

Uislamu ulianza lini?